Sunday, 29 April 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-60

Asalam aleykum,

Miongoni mwa habari ambazo zinatikisa kwa sasa hapa Uingereza ni dhamira ya mjukuu wa Malkia,Prince Harry,ya kutaka kwenda kwenye uwanja wa vita huko Irak.Harry ambaye kwa sasa ni afisa katika jeshi la nchi hii ameonyesha bayana kuwa lazima aende kushiriki kwenye vita hiyo ambayo tayari imeshagharimu mamia ya maisha ya askari wa Uingereza.Wiki iliyopita kulikuwa na tetesi kwamba Harry “alichimba mkwara” (alitishia) kwamba iwapo hatapelekwa huko Irak basi ataachana kabisa na jeshi.Pia mwishoni mwa wiki kulikuwa na taarifa inayodai kuwa bibi yake Harry,Malkia Elizabeth,angependelea kumwona mjukuu wake akienda vitani hasa kwa vile tukio hilo lingeiletea sifa sana familia hiyo ya kimalkia.Baba mdogo wa Harry,Prince Andrew alishiriki kwenye vita kati ya Uingereza na Argentina kugombea visiwa vya Falklands.Lakini tofauti na hali ilivyokuwa wakati wa vita hiyo,safari hii majeshi ya Uingereza yanakabiliana na adui wa aina tofauti:jeshi lisilo rasmi ambalo miongoni mwa silaha zake kuu ni mashambulizi ya kujitoa mhanga na kuchukua mateka (baadhi ya mateka hao walichinjwa na kuonyeshwa “laivu” kwenye mtandao).

Gazeti moja la mwishoni mwa wiki liliripoti kuwa Waziri wa Ulinzi Des Browne amejivua lawama na kuliacha suala la Harry kwenda Irak kuwa mikononi mwa jeshi la nchi hii.Wachambuzi wa vita vya Irak wanatamka bayana kuwa upo uwezekano wa mjukuu huyo wa Malkia kuishia mikononi mwa vikundi vya wapiganaji (insurgents) kama mateka au kibaya zaidi akaishia kuuwawa,suala ambalo wanadai litakuwa na madhara makubwa sana kwa siasa za Uingereza.Na tayari vikundi vya “insurgents” vimeshatangaza kuwa “Harry ni mlengwa wao namba moja,na ataandaliwa mapokezi rasmi,kabla ya kurudisha mwili wake kwa bibi yake (Malkia) ukiwa hauna masikio.”Tisha toto?Labda,lakini hawa jamaa sio wa kupuuzwa kwani pamoja na Joji Bush kuamua kuongeza wanajeshi wake zaidi ya 20,000 bado wanaendelea kuteketea takriban kila siku.Wiki iliyopita imeshuhudia takriban wanajeshi wa Kimarekani 20 wakiuawa kutokana na mashambulizi yanayofanywa na “insurgents” hao.

Prince Harry anasema kuwa tishio la usalama wa maisha yake huko Irak sio kigezo cha kumzuia yeye kwenda kuitumikia nchi ambayo siku flani katika mahesabu ya kifamilia anaweza kuwa mfalme wake.Anadai kuwa maisha yake hayana thamani tofauti na yale ya askari wengine walioko uwanja wa mapambano au wale waliokwishapoteza maisha yao huko nyuma.Hata hivyo,wapo wanaoona “ushujaa” huo wa Harry ni kitu cha hatari sana kwa vile iwapo kweli “insurgents” wataelekeza nguvu zao zote ili kumteka au kumuua kuna hatari ya askari wengi zaidi kuhatarisha maisha yao kwa ajili ya mtu mmoja (Harry).Kadhalika,ipo hofu kuwa iwapo Harry atatekwa au kuuwawa basi utakuwa ni ushindi mkubwa sana kwa “insurgents” na makundi ya kigaidi kama Al-Qaeda pengine zaidi ya “ushindi” wao wa mashambulizi ya Septemba 11,2001 huko Marekani.

Jingine kwa leo ni changamoto nayoitoa kwa wale wote waliosoma shule ya sekondari ya Tabora Boys.Duniani kote huwa kuna shule,vyuo au taasisi ambazo kwa namna flani haviwezi kutenganishwa na historia ya nchi husika.Mie nilifika hapo mwaka 1990,nikakaribishwa kwa kwata moja kali sana iliyodumu kwa wiki sita.Enzi hizo kulikuwa na mchepuo wa kijeshi,na shule hiyo ilikuwa “maalumu” hasa.Hizo wiki sita za “ngarambe ya ukaribisho” zilipoisha nilijiskia mkakamavu katika kila namna,kimwili na kiakili.Nidhamu ya hapo ilikuwa ni ya kijeshi hasa utadhani uko TMA Monduli,na badala ya yunifomu sie tulikuwa tunavaa kombati za khaki (akinadada wa Tabora Girls nao walikuwa ndani ya kombati kama sie kwani shule yao nayo ilikuwa na mchepuo wa jeshi).

Nilibahatika kuchaguliwa kuwa “Chifu” wa wanafunzi.Kwenye shule za “kiraia” Chifu alikuwa sawa na “Kaka Mkuu” (Head Prefect).Nilikuwa na “mikasi” kadhaa mabegani kuashiria cheo changu kama ilivyokuwa kwa viongozi wengine waliokuwa chini yangu.Najiskia msismko flani nikikumbuka enzi hizo.Hapo kulikuwa hakuna mambo ya “shikamoo mwalimu” au Goodmorning/goodafternoon Sir/madam” bali ni mwendo wa “Jambo afande.”Na sie viongozi tulikuwa tukiitwa maafande pia.Halafu kama nyota ya jaa iliamua kuuwakia ukoo wa Chahali,dada yangu Consolata aliyekuwa mwaka mmoja wa masomo nami alibahatika kuchaguliwa kuwa “Second Chief” huko Tabora Girls,na dada mwingine,Dinna nae alidaka uongozi wa “platuni” (halahala mnaoalikwa kwenye mahojiano Chanel 10,mtu atakaemletea za kuleta anaweza kupigishwa kwata hapohapo studio).Enewei,isijeonekana “tunajifagilia” bure,ngoja nirejee kwenye changamoto nayotaka kuitoa.Sekondari hiyo ya Tabora ina historia ya kipekee nchini.Ni sehemu ambayo Mwalimu alifundisha na viongozi kadhaa wa nchi yetu walipata elimu yao hapo.Nadhani hadi leo ule ubao unaoonyesha viongozi wa wanafunzi tangu “mwaka 47” bado upo (kama upo basi naamini jina langu nalo lipo hapo).Na kwenye ubao huo ndio utamaizi kuwa shule hiyo “imezaa” viongozi lukuki wa nchi yetu.

Niliwahi kusikia kuwa mchepuo wa jeshi umeondolewa shuleni hapo.Hilo ni jambo la kuhudhunisha sana kwa vile ule “ujeshi” ulikuwa ukijenga nidhamu flani ambayo ni adimu sana kuikuta kwenye shule ya kawaida.Wakati wa likizo kundi la wanafunzi lilikuwa likipelekwa msituni kwa ajili ya mafunzo ya kivita.Bila kutia chumvi,napenda kukupasha msomaji wangu mpendwa kuwa kwa kubahatika kupitia Tabora Boys nilifanikiwa kuongoza kikosi kwenye vita.Ofkozi,ilikuwa ni vita ya mfano tu lakini kwa namna maafande walivyokuwa wakiichukulia “siriaz” basi sie “wanajeshi” tulikuwa tunajiskia kama tuko Mtukula tukimwadhibu nduli Idd Amin.Na taaluma hiyo ilikuwa na faida yake tulipokwenda jeshi la kujenga taifa kwa mujibu wa sheria (siku hizooo).Tulijikuta tunapata ki-upendeleo cha namna flani kwa vile kama ni kwata za awali sie tulikuwa tumeshaiva kabla ya kutia mguu kwenye kambi ya JKT.

Sasa naomba kutoa changamoto kwa wale wote waliopitia shule hiyo kuhakikisha kuwa haipotezi sehemu yake katika historia ya taifa letu.Nina wazo ambalo bado nalifanyia kazi la kuunda kitu kama “alumni” ya namna flani (yaani jumuiya ya watu waliosoma mahala hapo).Najua hiyo si kazi rahisi kwa vile baadhi ya waliosoma hapo ni watu wenye majukumu makubwa kitaifa na pengine hawatakuwa na muda wa kujihusisha na jumuiya kama hiyo.Huku ughaibuni,watu hawajali nyadhifa zao linapokuja suala la kuienzi sehemu iliyowafikisha hapo walipo.Si ajabu ukakuta mkutano wa alumni wa taasisi flani ya elimu ikiwakutanisha mawaziri,wafanyabiashara wa kawaida na hata wale ambao mambo hayajawa mambo (majobless.Ndio,huku nako wapo majobless).Nafahamu kuwa kwa Bongo inaweza kuwa vigumu kidogo kwa kigogo kujichanganya na mtu ambaye sanasana jina lake likisikika kwenye chombo cha habari basi atakuwa anakabiliwa na kesi au katajwa kwenye tangazo la kifo,lakini tunaweza kusahau tofauti zetu za kimatabaka na kuangalia namna tunavyoweza kudumisha jina la “Tabora Skuli.”Pengine vuguvugu la namna hiyo linaweza kuhamia na kwenye shule nyingine za kihistoria kama vile sekondari ya Pugu na kwingineko.

Mwisho,nimevutiwa sana na jitihada za mwanamuziki wa kizazi kipya Ambwene Yesaya (AY) ambaye amezindua website yake hivi karibuni.Nilishindwa kujizuia kumpa pongezi zangu nilipoiona kwa mara ya kwanza,na yeye hakufanya “ubishoo” akatoa shukrani zake kwa pongezi na maoni niliyompatia.Website yake inapaswa iwe changamoto wa wasanii wengine hasa kwa vile mtandao ni kitu anbacho kinaweza kumtangaza mtu ulimwengu mzima iwapo mhusika atajituma ipasavyo.Kwa kuwaunga mkono vijana wetu wanaojiajiri wenyewe kwa kutumia vipaji vyao natoa ushauri kwa makampuni ya umma na ya binafsi “kuwapa tafu” wasanii kama AY kwa kuweka matangazo yao kwenye website kama hiyo.Nami ntawaunga mkono kwa kuweka links za websites zao kwenye blogu yangu.Nitumie lugha “ya wenyewe” kwa kusema “nakupa tano mwanangu AY.”

Alamsiki


KULIKONI UGHAIBUNI-59

Asalam aleykum,

Majuzi nimesoma habari flani kwenye gazeti la Daily Mail la hapa Uingereza kuhusu harakati za mwanamuziki wa kimataifa Madonna ambaye tayari amesha “adopt” mtoto mmoja huko Malawi.Inaweza kuwa habari njema kwa mtoto huyo kupata bahati ya kuingizwa kwenye familia ya mwanamuziki huyo maarufu na tajiri kabisa duniani.Nadhani hakuna mmoja wetu sie tulio hohehahe ambaye asingependa kuzaliwa kwenye familia ya vibopa,au kubahatika kurithiwa na familia tajiri.Kwa mtoto huyo wa Kimalawi hiyo ni sawa na bahati ya mtende kuota Jangwani.

Hata hivyo,kuna taarifa ambazo sio za kufurahisha kuhusiana na suala zima la Madonna kurithi watoto huko Malawi.Mwanamuziki huyo ni mfuasi wa dhehebu jipya la Kabbalah.Na kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana,amekuwa akitumia “upendo” wake kwa watoto wa Malawi kueneneza dini hiyo ambayo kwa kiasi flani imegubikwa na utata.Mwanamuziki huyo anamiliki vituo kadhaa vya kulelea yatima nchini humo,na inaelezwa kuwa vinaendeshwa kwa pamoja na wafuasi wengine wa madhehebu hayo ya Kabballah.Wapo wanaoona kuwa dhamira nzuri ya Madonna kuwasaidia watoto hao inapotezwa na hiyo ajenda yake ya siri ya “umisionari” wa Kabbalah.Kwa wengine,hiyo ni sawa na kumbukumbu za ukoloni ambapo wamisionari walitumia misaada yao kubadili imani za asili za watu.Ni sawa na kutoa msaada wenye masharti magumu,hasa ikizingatiwa kuwa Madonna na wana-Kabbalah wenzie wanatumia umaskini na uyatima wa watoto wa Malawi kuwaingiza kwenye madhehebu ambayo pengine wangekuwa na uwezo wasingetaka kujiunga nayo.

Tukiachana na Madonna,tuangalie mambo yalivyo huko nyumbani.Moja ya mambo ambayo yamenigusa sana wiki hii ni taarifa nilizosoma kwenye gazeti moja la kila siku la huko Bongo kuwa hivi majuzi kuwa Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Kisutu imewaachia mtuhumiwa mmoja aliyekuwa akikabiliwa na kesi ya mauaji na mwingine aliyekuwa akikabiliwa na mashtaka ya madawa ya kulevya yenye thamani ya shilingi milioni 250.Uamuzi huo wa mahakama umetokana na maelezo ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) ambaye aliamua kuachana na kesi hiyo kwa kutumia kipengele cha kisheria kiitwacho “nolle prosequi” (yaani mtuhumiwa hana kesi ya kujibu) lakini bila DPP kutoa sababu zozote.

Habari hii imenishtua kwa vile kwa mtizamo wangu nadhani DDP anawajibika kwa umma wa Watanzania.Yaani kwa lugha nyepesi,yeye ndiye mwakilishi wa Jamhuri kwenye mashtaka ambayo kwa namna moja au nyingine yanawaweka wananchi wa kawaida upande mmoja na watuhumiwa upande mwingine.Sasa anapoamua kutumia nguvu zake kisheria kufuta kesi bila kutoa maelezo anataka kutueleza nini?Hapa UK kuna mamlaka iitwayo Crown Prosecution Service (CPS) ambayo kwa namna flani ni kama ofisi ya DPP huko nyumbani.Ni kweli kuwa mamlaka hiyo imekuwa ikifuta baadhi ya kesi,lakini nyingi ya kesi hizo ni zile ambazo huhitaji hata kozi fupi ya sheria kutambua kuwa mtuhumiwa hana hatia ,na umma huwa unajulishwa kwanini CPS imeamua kufuta kesi husika.

Pengine tofauti ninayoiona kati ya CPS ya hapa na DPP wa huko Bongo ni kwamba hapa CPS inatoa maamuzi ya kitaasisi zaidi wakati kwa huko nyumbani maamuzi ya DPP yanaonekana kama ya mtu binafsi anayewakilisha taasisi.Kuna tofauti kubwa hapo.Lakini bila kujali tofauti hizo,nashawishika kuhofu kuwa DPP anaweza kuamua kumwachia mtuhumiwa kwa utashi wake binafsi,hasa ikizingatiwa kuwa hawajibiki kuelezea kwanini ameamua hivyo.Ikumbukwe kuwa kwenye kesi ya Dito,kauli za DPP (kama mtu binafsi) zilileta hisia kuwa Mheshimiwa huyo anatumia u-Mungu mtu wake kisheria kuendesha mambo anavyjiskia yeye.Hiyo ni hatari kwenye nchi inayoendeshwa kwa kufuata utawala wa sheria.

Pasipo kutaka kuingilia utendaji kazi wa DPP,nadhani kuna umuhimu wa kuwepo mamlaka ambayo inaweza kumbana DPP katika maamuzi yake hasa hayo ya kuwaachia watuhumiwa bila kutoa sababu.Kwa nchi ambayo “wenye nazo” wanaweza kupindisha sheria,yayumkinika kuamini kuwa baadhi ya kesi ambazo DPP anazitupilia mbali zinapata “bahati” hiyo baada ya “kuwepo namna flani.”Kuwa na nguvu kubwa kisheria ni suala zuri lakini iwapo nguvu hizo zikitumika vibaya basi hapo inakuwa balaa.Nadhani ni vema kukawekwa utaratibu utakaouhakikishia umma kuwa pindi DPP akiamua kufuta kesi kwa madai kuwa “mtuhumiwa hana kesi ya kujibu” basi ALAZIMIKE kuujulisha umma sababu zilizomfanya afikie uamuzi huo.

Jingine ambalo nilishalizungumzia huko nyuma ni ubabaishaji wa viongozi wa klabu ya Simba.Na kama nilivyotabiri,hatimaye Mbrazili waliyemleta kwa mbwembwe kibao ameamua kuwaacha kwenye mataa.Nakubaliana na kauli ya Katibu Mkuu wa TFF kuwa viongozi wa timu hiyo wanapaswa kuwa makini wanapokimbilia kuchukua makocha kutoka nje ya nchi bila kuzingatia suala la mikataba.Laiti viongozi hao wangekuwa wamewekeana mkataba wa kueleweka na kocha huyo ni dhahiri kuwa asingeamua kuondoka bila kuwaaga kwa vile anafahamu kuwa sheria ingekuwa dhidi yake.Niliposikia viongozi hao wakijigamba kuwa licha ya kelele walizokuwa wakipigiwa wameweza kumleta kocha kutoka Brazil,nilipata hisia kuwa wamekurupuka kufanya hivyo ili kuua tuhuma kadhaa zilizokuwa zikiwakabili.Na kweli “triki” hiyo ilifanya kazi kwani mizuka ya wapenzi wa klabu hiyo ilitulia na wakaungana na viongozi hao wababaishaji kumpatia kocha huyo mapokezi makubwa na ya kihistoria.

Muda mfupi kabla sijamaliza kuandaa makala hii nimesoma kwenye gazeti moja mtandaoni kuwa viongozi hao wa Simba wanataka kuleta kocha kutoka Ureno.Hivi kwanini wana-Simba wanafanywa wajinga kiasi hicho?Kabla uongozi haujaweka bayana kilichomkimbiza kocha Mbrazil,wanakimbilia kuleta habari za kocha mwingine kutoka ng’ambo!Huo ni ubabaishaji wa daraja la kwanza.Nilishasema kuwa ni vigumu sana kwa vilabu vyetu kudumu na makocha wenye upeo hasa wa kutoka nje ya nchi kwani mfumo wa soka katika ngazi ya vilabu umetawaliwa sana na ubabaishaji.Viongozi wa Simba wanaweza kuwabeza “Friends of Simba” lakini wanasahau kuwa “wamekalia makuti makavu” kwa vile hawana mbinu za kuiingizia mapato klabu hiyo kongwe bila kutegemea hisani za wafadhili.Vyanzo vya mapato vipo waziwazi lakini kwa vile viongozi hao wametawaliwa na fikra finyu ambazo kwa kiasi kikubwa zinaelemea kwenye maslahi yao binafsi badala ya maendeleo ya klabu,wanajikuta wakiitisha “press conferences” moja baada ya nyingine kutoa “mipango hewa” ya maendeleo kama zile ndoto za alinacha za kujenga uwanja wa kisasa.Wito wangu kwa wana-Msimbazi ni kuachana na wababaishaji hao mapema kadri iwezekanavyo,la sivyo mambo yatakuwa mabaya zaidi ya yalivyo sasa.

Mwisho ni uchungu wangu mkubwa baada ya kuona wenzetu Wakenya wakitesa kwenye London Marathon huku sie wabongo tukiwa hatuna mwakilishi.Hivi kizazi za akina Ikangaa,Bayi,Shahanga,Nyambui na wengineo kimepotelea wapi.Hivi kweli tunahitaji wawekezaji hata kwenye “kufukuza upepo”?Jiografia ya mkoa kama Kilimanjaro inatoa upendeleo mkubwa kwa Watanzania kuzalisha wanariadha wa kiwango cha kimataifa.Riadha iliwahi kutupa jina kubwa huko nyuma lakini sijui tatizo liko wapi.Wakongwe wa riadha walioingia kwenye uongozi wa vyama vya riadha na kamati ya Olimpiki wanaelekea wameridhika na mafanikio waliyoyapata wao miaka ya nyuma na hawajali kama kutawekwa historia nyingine.Ni wivu wa kutaka rekodi zao zisifikiwe na wanariadha wa sasa,uzembe na kutojua kazi yao, au ndio yaleyale ya kuthamini zaidi matumbo yao kuliko maslahi ya Taifa?

Alamsiki

KULIKONI UGHAIBUNI-58

Asalam aleykum,

Kuna habari moja niliyoiona kwenye runinga hivi karibuni kuhusu falsafa ya ushindani huko nchini China imenivutia sana kiasi najiskia “kushea” nawe msomaji mpendwa.Stori hiyo ilikuwa inazungumzia kuhusu binti mmoja wa miaka minane ambaye huamshwa na baba yake kila siku saa 9 alfajiri kwa ajili ya mazoezi ya mbio za marathon.Mazoezi hayo hudumu kwa zaidi ya masaa mawili na sio suala la hiari bali ni sehemu ya maisha ya binti huyo na familia yake.Anapoulizwa kuwa haoni kwamba “kwa kumpelekesha puta” binti yake namna hiyo ni kama anamwadhibu,baba yake anamnukuu Adolf Hitler kwenye usemi wake kwamba “askari asiyepania kuwa jenerali hastaili kuwa jeshini” akimaanisha kwamba ni muhimu kwa mwanadamu kupania mafanikio ya juu kabisa kama anataka kufanikiwa katika maisha.Mzazi huyo anaamini kuwa baadaye bintiye atavuna anachopanda hivi sasa hasa kwa vile “kufukuza upepo” (riadha) ni mchezo wenye maslahi makubwa sana.Na inahitaji maandalizi ya mapema kweli ili uweze kuibuka kijogoo kwenye fani yoyote ile katika nchi kama China ambayo ina watu zaidi ya bilioni moja.

Wazazi mnaosoma makala hii,mnaonaje na nyie mkaanzisha utaratibu wa kuwachukua vijana wenu kwenda sehemu ambazo zitawaandalia “future” bora maishani mwao.Kwa wewe mzazi Mwislam unayeamka alfajiri kwa ajili ya swalat alfajir,unaonaje kama utaambatana na mwanao ili kumjengea msingi bora wa kiroho?Nimetolea mfano wa swala ya alfajiri ili kuendana na stori hiyo hapo juu lakini si lazima iwe muda huo tu,bali hata alasir,adhuhur,magharib au isha.Haihitaji kuwa na PhD ya dini ili kufahamu kuwa mara nyingi familia inayothamini ibada huwa familia bora,imara ,yenye mwelekeo na isiyoyumbishwa na vitu visvyo na msingi hasa vile vya kishetani.Unadhani familia yenye kuendekeza ibada inaweza kuzaa mla rushwa?No way.Wala rushwa ni watu waliopotoka kimaadili,ni wezi wanaovunja amri za Mungu,na ibada siku zote inasisitiza kumheshimu Mungu na kutekeleza yale anayotaka,ambayo siku zote ni mambo mema.

Wazazi Wakristo ndio hawapaswi kuwa na kisingizio hata kidogo kwa vile idadi ya sala kwa siku huko kanisani (ukitoa Jumapili) ni chache kulinganisha na wenzao Waislam.Kwa Wakatoliki,sala ya asubuhi katika siku za juma ni moja tu,na laiti mzazi mwenye dhamira ukiamua,basi inawezekana kabisa kwamba kila asubuhi wakati unaelekea kibaruani na mwanao anaelekea mkaambatana kwenda “kupata neno” kanisani kabla hamjaendelea na ratiba zenu.Amin nakuambia,siku inayoanza kwa sala inakuwa siku ya amani,na mwanao atakwenda shule akiwa na wazo moja tu la “kitabu” na sio sketi za wanafunzi wa kike,na wewe mzazi utawajibika kibaruani kwa namna ya kumpendeza Mungu wako,na utapomaliza job jioni njia ya kwenda nyumbani itakuwa pana zaidi ya ile nyembamba inayoelekea baa au nyumba ndogo.


Baada ya hayo,sasa naelekeza macho yangu kwenye muziki.Lakini kabla sijaingia kwa undani kwenye mjadala wangu,ngoja nikudokezee utata huu unaendelea huko Marekani na baadhi ya nchi nyingine za magharibi.Ni hivi,ni kosa linaloweza kumpeleka jela mtu mweupe pindi akimwita mtu Mweusi “nigger.” Ni neno ambalo ni zaidi ya mwiko na pindi likitumiwa kwenye vyomba vya habari basi hutajwa kama “neno lenye N” (the N-word).Kichekesho ni kwamba neno hilo ni la kawaida sana miongoni mwa watu weusi.Kulirembesha na kuwa “nigga” badala ya “nigger” hakubadilishi lolote zaidi ya kuongeza utata.

Sio siri kuwa muziki wa kufokafoka (rap) umekuwa na mwonekano (image) mbaya sana zaidi miongoni mwa jamii ya watu weupe na hata kwa watu weusi.Marapa weusi wamekuwa wakishutumiwa sana kwa kile kinachoonekana kama kuchochea matumizi ya silaha,utumiaji wa mihadarati na kibaya zaidi ni dharau yao kwa jinsia ya kike,ambapo kwa wengi wao kila mwanamke kwao ni “biach”, “hoo”,n.k (malaya) utadhani wao walizaliwa kwenye testi tyubu.Wanaelimishaji miongoni mwa jamii ya watu weusi wamekuwa wakitoa kilio chao dhidi ya udhalilishaji wa namna hiyo,na kukemea matumizi ya neno “nigga” lakini marapa hao hawana muda wa kusikia.Baadhi ya watu weupe wanalalamika kwamba iweje wako wakimwita mtu Mweusi “nigger” inakuwa kosa la ubaguzi wa rangi lakini wenyewe kwa wenyewe wanaitana hivyo.Hoja yao ni kwamba kama neno hilo ni sawa na tusi basi iwe hivyo kwa watu wote pasipo kuangalia rangi ya mtu.

Kwa muziki wetu wa nyumbani,mie bado nataabika na mwonekano “image” wa baadhi ya wasanii wetu.Najua hapa nitatofautiana kimawazo na baadhi ya watu,lakini tutafika.Hivi unapata picha gani unapokuta kundi zima la kikundi cha bongofleva likiwa na watu waliosokota minywele yao katika kile wenyewe wanakiita rasta huku wamevaa miflana yenye picha za majani ya bangi!Na hapa ntakuwa muwazi zaidi.Mvumo wa bongofleva ulijiri wakati mie nimeshaondoka huko nyumbani.Nilipoona mtandaoni kuwa muziki wa kizazi kipya umefunika mipasho na “bakulutu” nilidhani ni stori tu.Lakini nilipokuja huko home mwaka jana nikajionea mwenyewe namna gani bongofleva ilivyofanikiwa kuteka hisia za wapenda muziki.Kundi moja ambalo nililikubali mara moja ni TMK Wanaume (kabla halijameguka).Lakini tatizo la msingi nililokuwa nalo dhidi yao ni hiyo taswira waliyokuwa wanajitahidi kuitengeneza na kuindekeza:taswira ya “jah people”,taswira ya “marastafari”,kwa lugha ya wazi taswira ya wavuta bangi.

Jana nimeona kwenye blogu ya Michuzi picha ya basi la ziara ya Juma Nature na kundi lake huko Mwanza,na ndani ya basi hilo kuna kijipicha chenye jani la bangi.Hivi hawa watu wanataka kutuambia nini kuhusu taswira hiyo ya “widi” wanayoonekana kuitukuza sana?Hivi huwezi kuwa supastaa mpaka uwe na mwonekano wa ajabuajabu?Mbona Mista Two amedumu miaka nenda miaka rudi huku “pesonaliti yake ni ya kishua” (yaani anaonekana zaidi kama meneja flani kuliko rapa).Solo Thang,Prof Jay,Banana,Mike Tee,Mr Paul na wengineo,ni mwiongoni watu ambao wamekuwepo “kwenye gemu” kwa kitambo sasa lakini hawajajichafulia mwonekano wao katika namna ya kuabudia “majani.”

Mie sio mpinzani wa mtindo wa rasta,wala sina chuki na imani ya urastafari.Lakini mtu yeyote mwenye busara atafikiria mara mbilimbili kabla ya kujitundika mtindo ambao kwa namna moja au nyingine unaweza kumfanya aonekane “mvuta bangi flani.”Nafahamu kuwa cha muhimu zaidi sio mtindo wa nywele bali “fleva na meseji” lakini nani asiyejua kuwa meseji inayotolewa na mlevi inaweza kupoteza fleva yake kwa vile tu mtoaji ni mlevi!Hiyo mibangi mnayoendekeza na kuiwekea lebo kila mahali itawapeleka pabaya.

Mibangi hiyo ndio inayofanya matamasha yenu yawe ya kuvutia kwa vile changamoto hapo huwa ni “stimu za widi” lakini likija suala la kutengeneza video za kueleweka,unamkuta msanii anaionea aibu kamera,kisa hajashtua hisia zake.Sio siri kuwa kwa namna flani hatma ya baadhi ya mastaa wa bongofleva iko mikononi mwa hayo majani wanayoyaendekeza.Nasema hivyo kwa sababu bangi sio kitu chema,na ukichanganya na mikanganyiko ya kawaida katika maisha ya kila siku,basi si ajabu baadhi ya mastaa hao wakajikuta “wanatema vesi” wakiwa Mirembe.

Friday, 6 April 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-57

Asalam aleykum,

Wakati naelekea mtamboni kuandaa makala hii,hatimaye Rais wa Iran ametangaza kuwaachia huru wanajeshi 15 wa Uingereza ambao walikuwa wakishikiliwa mateka na jeshi la Iran.Mgogoro huu ulikuwa umetawala mno kwenye vyombo vya habari vya hapa Uingereza na nchi nyingine za Magharibi.Kwa namna mambo yalivyokuwa yakienda ilikuwa ni vigumu kutabiri nini kingefuatia iwapo Iran ingeendelea na msimamo wake wa kuwashikilia wanajeshi hao.Tayari baadhi za sauti zenye msimamo mkali hapa UK zilishaanza kumtaka Waziri Mkuu Tony Blair “kufanya kitu flani” kuhakikisha kuwa mateka hao wanaachiwa.Nadhani akilini mwao,watu hao walikuwa wakijaribu kuchochea matumizi ya nguvu za kijeshi ili kutatua tatizo hilo.Hata hivyo,kiongozi yoyote mwenye busara angelazimika kufikiria mara mbilimbili kabla ya kuchukua uamuzi mzito kama huo hasa ikizingatiwa kuwa Iran “imekamilika” kijeshi bila kusahau karata yake turufu ya mafuta.Hadi muda huu haijafahamika ni lini hasa mateka hao watarejea hapa lakini lililo wazi ni kuwa wameachiwa kwa kile Rais wa Iran alichokiita “zawadi kwa watu wa Uingereza.”Pengine alikuwa anamaanisha zawadi ya Pasaka.

Tukiachana na hilo,ningependa kuungana mkono na wito uliotolewa na mwanasiasa mkongwe,mbunge wa Mtera na Makamu Mwenyekiti wa CCM,John Malecela,ambaye amenukuliwa hivi karibuni akiomba ifanyike semina kwa wabunge kuhusu ugonjwa wa homa ya bonde la ufa (Rift Valley Fever-RVF).Naamini madhumuni ya mkongwe huyo wa siasa ni katika jitihada ya kulipa kipaumbele janga hilo katika namna ambayo Taifa zima kwa kupitia wawakilishi wao Bungeni litawekwa katika tahadhari ya kupambana na ugonjwa huo.Nadhani licha ya semina kwa wabunge,jitihada za haraka zinahitajika kuuelewesha zaidi umma wa Watanzania kuhusu namna ya kuukabili ugonjwa huo.Japo si ugonjwa mpya lakini hii ni mara ya kwanza ambapo unaelekea kuchukua taswira ya kitaifa.Inatupasa kukumbuka kuwa hadi muda huu bado gonjwa jingine tishio la kipindupindu linaendelea kutesa katika baadhi ya maeneo ya nchi yetu.Haimaanishi kuwa serikali haifanyi jitihada zinazopaswa bali sote tunafahamu kuwa ni rahisi kukumbwa na ugonjwa kuliko kuutokomeza.Kwa mantiki hiyo,kinga dhidi ya RVF itakuwa ni jambo la muhimu zaidi kuliko kuanza kuhangaika na tiba pindi utakapotapakaa.

Labda la kukumbushana hapa ni ile tabia ya semina juu ya semina kujadili kitu flani.Yayumkinika kusema kwamba laiti semina lukuki dhidi ya majanga kama ukimwi zingeishia kutafsiriwa kwa vitendo basi tungeweza kuwa tumepiga hatua kubwa zaidi ya hapa tulipo sasa.Hivyohivyo,kwenye maeneo kama vita dhidi ya umasikini na tatizo sugu la rushwa.Semina ni kitu kizuri kwa vile lengo ni kuelimishana kuhusu suala husika.Lakini semina ambazo zinaishia kwenye posho tu ilhali fedha hizohizo za posho zingeweza kuelekezwa kwenye utatuzi wa matatizo yanayojadiliwa katika semina hizo ni jambo ambalo linapaswa kuepukwa.


Jambo jingine nalopenda kuligusia ni kipigo cha Taifa Stars huko Senegal.Aliyekuwa akijidanganya kuwa tungeweza kuibika na ushindi kirahisi katika mechi hiyo atakuwa haijui vizuri dunia ya soka.Yayumkinika kusema kipigo cha mabao manne kilikuwa ni halali yetu japo hakuna mpenda soka ambaye yuko tayari kuridhika na kipigo.Tulitegemea nini tulipopambana na timu ambayo wachezaji wake wote 11 wanacheza soka la kulipwa nchi za nje.Na hapo tunawazungumzia watu kama Elhadj Diouf ambao wana majina makubwa hadi kwenye ligi ya hapa Uingereza.Senegal ni moja ya timu zenye hadhi kubwa ya soka duniani na ndio maana timu za taifa za nchi zinazotamba kwenye dunia ya soka hupendelea kuomba mechi za majaribio na Simba hao wa Teranga.Wenzetu hawahitaji ziara ya sehemu kama Brazil kujiandaa kwa mechi zao kwa vile mechi ngumu katika klabu wanazochezea wanasoka wao ni majaribio tosha ya kukabili timu kama Taifa Stars.

La msingi hapa ni kujiandaa kwa mechi ijayo.Ni mechi ngumu kweli,na sote tunapaswa kutambua ukweli huo.Ni rahisi kuishi kwa matumaini kuliko kuikabili hali halisi.Kwa namna hiyo hiyo,ni rahisi kuamini kuwa tunaweza kuwatoa Wasenegali hao watapokuja kwenye mechi ya marudiano Dar,lakini kuwa na imani pekee hakutoshi.Kunahitajika maandalizi ya hali ya juu.Nadhani kwa mtizamo wangu,zile fedha zinazotafutwa kwa ujio wa ziara ya timu ya Real Madrid zinaweza kuelekezwa kwenye maandalizi ya mechi dhidhi ya Senegal.Na pengine kwa kufanya hivyo tutakuwa tunaua ndege wawili kwa jiwe moja.Yayumikika kusema kuwa timu ya taifa ya Senegal ina umaarufu unaokaribiana na Real Madrid.Na kama suala ni kulifanya tukio la uzinduzi wa uwanja mpya wa taifa kuwa la kihistoria basi hakutakuwa na historia au zawadi kubwa kama kuufungua kwa mechi ya marudiano na Senegal na kuwafungasha virago siku hiyohiyo.Naamini kabisa kuwa pesa ambazo zinatafutwa kuwagharamia mastaa wa Real Madrid zinaweza kuwa changamoto tosha kwa wachezaji wetu iwapo kwa mfano wataahidiwa hata nusu ya posho ya siku ambayo taifa letu litawajibika kuwalipa “wageni wetu kutoka Madrid.”Unadhani kama wanasoka wetu wataahidi shilingi milioni 1 kila mmoja iwapo wataibuka na ushindi kwenye mechi hiyo,hawatajituma katika namna ya “kuua mtu”?

Kingine ni pongezi zangu kwa kituo cha redio cha Clouds FM kwa kuanzisha huduma ya matangazo yake kwenye mtandao.Nilijiskia raha isiyoelezeka wakati nafuatilia “laivu” kwenye mtandao uzinduzi wa albamu ya “ndege tunduni” ya Juma Nature na wenzake hapo Diamond Jubilee.Sijui kama wenyewe walikuwa wanafahamu kuwa uzinduzi huo ulikuwa ukisikika sehemu mbalimbali duniani kwa kutumia teknolojia ya internet.Kwa hilo,nawapongeza sana Joseph Kusaga na timu yake nzima ya Clouds FM.Kwa hakika wamefungua njia mpya katika sekta ya habari.

Hata hivyo,kwa vile sasa matangazo ya stesheni hiyo yanasikika ulimwenguni kote ni muhimu kwao kuhakikisha kuwa utendaji wao unakuwa na hadhi ya kimataifa.Wikiendi iliyopita nilikuwa nasikia kipindi flani (sikijui jina lake) ambacho kilirushwa hewani alfajiri kwa saa za hapa na kilipitia habari za kimataifa.Naomba niseme kwamba mtangazaji (wa kiume) aliyekuwa akiendesha kipindi hicho alikuwa “anajiumauma” sana kana kwamba habari hizo zinatoka kichwani mwake badala ya kuzisoma mahala flani.Lengo langu sio kumuumbua bali nachofanya ni sawa na changamoto kwake na kwa watangazaji wengine hususan katika kipindi hiki ambacho wasikilizaji wao wako zaidi ya mipaka ya Tanzania.Na hilo halimaanishi kuwa “kulipua” matangazo yaliyo ndani ya mipaka ya nchi yetu ni suala linalokubalika.Raha ya kusikiliza habari ni pamoja na umakini wa mtangazaji.

Mwisho nitoe pongezi kwa “mdau” mmoja mwenye blogu ya haki-hakingowi.bogspot.com.Blogu yake ina mkusanyiko wapicha kutoka sehemu mbalimbali hasa za huko nyumbani.Na ukiwa huku ughaibuni,kila picha ya nyumbani inaleta kumbukumbu flani za kuvutia.Kazi anayofanya ni ya kuvutia hasa ikizingatiwa kuwa inahitaji jitihada flani kutumia muda binafsi kwa ajili tu ya kuwafurahisha watu wengine.Napenda pia kutumia fursa hii kutoa changamoto kwa watu wa fani mbalimbali kuanzisha blogu zao.Ni eneo ambalo linapanuka kwa kasi sana hasa kwa vile linafanikiwa kuwaunganisha watu walio sehemu mbalimbali duniani pasipo vikwazo vilivyozoeleka katika vyombo vya kawaida vya habari.

Pasaka njema.

Wednesday, 28 March 2007

Asalam aleykum,

Wiki hii kumefanyika maadhimisho ya miaka 200 ya kutokomezwa kwa biashara ya utumwa.Hafla maalumu zilifanyika sehemu mbalimbami hapa Uingereza pamoja na huko Jamaika na nchini Ghana.Kwa hakika,maadhimisho hayo yalikuwa yamegusa hisia za watu wengi hususan wale ambao wanajihesabu kuwa ni vizazi vya watumwa.Pia maadhimisho hayo yamezua mjadala ambao umedumu kwa muda mrefu kuhusu nini kifanywe na waliohusika katika biashara hiyo kwa namna moja au nyingine.Baadhi ya watu wamekuwa wakisisitiza kuwa licha ya nchi husika kuomba radhi kutokana na kuhusiaka kwao kwenye biashara hiyo isiyo ya kibinadamu,kunahitajika malipo kwa wahanga wa utumwa.Lakini swali ambalo limekuwa likiulizwa kila siku ni kuwa je malipo hayo yafanywe kwa nani na kama yakifanyika je kiasi gani kitakuwa sahihi kufidia uharamia huo.

Wapo wanaopinga suala la malipo kwa kigezo kwamba fedha haziwezi kutosha kufuta athari za biashara ya utumwa ambazo hadi leo bado zinaendelea hasa katika nchi za Magharibi.Miongoni mwa athari hizo ni suala la ubaguzi wa rangi ambao kwa hakika ni tatizo sugu sana katika nchi ambazo zilikuwa vinara wa biashara ya utumwa.Kwa mfano,kwa kiasi kikubwa jamii ya watu weusi hapa Uingereza na huko Marekani ni vizazi vya watumwa walioletwa kutoka Afrika kuja kujenga uchumi wa nchi hizo.Jamii hizi za weusi zimeendelea kuwa majeruhi wakubwa wa masuala ya ubaguzi wa rangi.

Pia suala lililoonekana kuzua mjadala wakati wa maadhimisho hayo ni namna umuhimu ulivyoelekezwa kwa wanasiasa wazungu waliohamasisha kukomeshwa kwa biashara hiyo huku jitihada za wasio wazungu (ambazo pengine ndio zilikuwa muhimu zaidi) zikisahaulika kwa makusudi.Kuna bwana mmoja Muingereza aliyekuwa akiitwa William Wilberforce.Huyo alijitahidi kulichachafya bunge la nchi yake kuhakikisha linapitisha sheria za kukomesha biashara ya utumwa.Katika maadhimisho hayo,Wilberforce ndiye aliyekuwa shujaa na kinara wa mapambano dhidi ya utumwa,suala ambalo limeonekana kama la kibaguzi miongoni mwa jamii za watu weusi hasa kwa vile mchango wa mashujaa kadhaa weusi (waliosimama kidete aidha wao pekee au kwa kushirkiana na wazungu wasiopenda utumwa kuhakikisha kuwa biashara hiyo inamalizwa ) unaonekana kupuuzwa kabisa.
Na kama vile kutia chumvi kwenye kidonda kibichi,baadhi ya wazungu wamekuwa wanadai kuwa si sahihi kuendelea kuwalaumu wao kwa makosa yaliyofanywa na mababu zao,na kwa mantiki hiyo hawaoni haja ya kuomba msamaha .Sambamba na “kiburi” hicho ni hoja kwamba biashara hiyo ya utumwa ilifanyika kwa ushirikiano kati ya wazungu na watawala wa Kiafrika.Hapa inakuwa kama hadithi ya nani kaanza kati ya kuku na yai.Je biashara hiyo ingekuwa kubwa namna hiyo kama wazungu wasingekuja kufuata watumwa Afrika?Au,je biashara hiyo ingekuwepo iwapo baadhi ya watawala wa Kiafrika kwa kushirkiana na wafanyabiashara wa Kiarabu wasingejihusiha na kuuza watumwa kwa wazungu?Yaani kimsingi ni kama biashara ya uchangudoa ilivyo:kama akina dadapoa hawatakuwepo maeneo kama Ohio na “vijiwe” vinginevyo wazinzi wataenda kufanya nini huko,na iwapo wazinzi hawatakwenda huko akina dadapoa watakwendaje kuumwa na mbu ilhali hakuna wateja.

Lakini maadhimisho hayo yamesaidia kwa namna flani kukumbusha kuwa licha ya ukweli kuwa biashara hiyo kukomeshwa bado utumwa unaendelea katika sehemu mbalimbali duniani japo pengine sio kwa kiwango kikubwa kama ilivyokuwa katika zama za “biashara ya pembe tatu” (Triangular Trade).Kumekuwa na taarifa mbalimbali zinazoonyesha kuwa aina flani ya utumwa inaendelea nchini Sudan japokuwa serikali ya nchi hiyo imekuwa ikikanusha kama inavyokanusha kuwepo kwa mauaji ya halaiki huko Darfur.

Pia kuna utumwa unaoendelea katika nchi mbalimbali za Magharibi ambapo akinadada wenye ndoto za maisha bora hujikuta wakirubuniwa kuondoka kwenye nchi zao kukimbia umasikini na hatimaye kujikuta wakiishia mikononi wa magenge yanayomiliki biashara ya ukahaba wa kimataifa.Wahanga wakubwa wa biashara hii ni akinadada kutoka nchi za Ulaya ya Mashariki ambao mara nyingi huahidiwa kupatiwa kazi bora pindi watapoletwa Ulaya Magharibi lakini wafikapo wanapokwenda hunyang’anywa pasi zao za kusafiria na kulazimishwa kulala na wanaume kadhaa kwa siku na wakati huohuo kutakiwa kulipia huduma za malazi,chakula na nyinginezo wanazopatiwa na hao wanaowatumikisha.Wanapoonyesha nia ya kukataa, “wamiliki” wao hitishia kuwaripoti kwenye mamlaka za uhamiaji kwa vile kwa wakati huo akinadada hao huwa wanaishi kama wahamiaji haramu kwa kuwa hati zao za kusafiria ziko mikononi mwa wamiliki hao.

Pengine baadhi yenu wasomaji wapendwa ambao hamkereki mnaposikia muziki wa kufokafoka (rap) mtakuwa mmeshasikia kibao cha mwanamuziki wa Kimarekani,50 Cent kinachoitwa P.I.M.P (ambacho amemshirkisha “mfokaji” mwingine Snoop Dogg). “Pimp” ni mtu anayekuwadia wanawake kupata mabwana,na japo kwa namna flani mahusianao kati ya “Pimp” na wanawake husika huwa kama ya ridhaa,bado yana dalili za utumwa wa namna flani.Ma-Pimp ni maarufu zaidi huko Marekani hususan miongoni mwa jamii ya watu weusi na inasemekana akinadada wanaojihusisha na ma-Pimp huwa kama wametekwa akili kwa namna wanavyowategemea “makuwadi” hao kwa kila kitu,hali ambayo inawafanya waendelee kutumikishwa huku ma-Pimp wakipendelea kutengeneza faida.

Ripota wa televisheni ya Sky News Emma Herd alipokuwa akiripoti kutoka mjini Accra,Ghana kuhusu maadhimisho ya kutokomezwa biashara ya utumwa alionyesha kushangazwa na namna ambavyo maadhimisho hayo yaliwavutia zaidi watalii kutoka nchi za Magharibi (hasa Wamarekani Weusi) ilhali Waghana wenyewe “wakiwa hawana mpango” na shughuli hiyo.Lakini baadaye alikiri kuwa wenyeweji hapo wana mambo lukuki ya “kudili” nayo kila kukicha badala ya kupoteza muda wao kuadhimisha siku moja ambayo kwao haileti tofauti yoyote katika maisha yao.Na hilo lina ukweli kwa sababu wengi wetu tunafahamu kuwa katika jamii zetu za Kiafrika bado tunakabiliwa na aina flani za utumwa ambazo kwa kiwango kikubwa tunaziona kama sehemu ya maisha yetu ya kila siku.Mfano mwepesi ni namna baadhi ya watumishi wa ndani (housegirls) wanavyotumikishwa kama watumwa kwenye makazi mbalimbali huko mitaani.Licha ya ahadi luluki wanazopewa wakati wanatolewa vijijini, baadhi ya mahauzigeli hao huishia kuwa “watumwa wa kisasa” ambao hupatiwa malazi duni,ujira mdogo,hunyimwa mawasiliano na ndugu zao na wengine hawaruhusiwi hata kwenda nje bila ruhusa ya “wamiliki wao.”

Kundi jingine linalofanyishwa kazi karibu kabisa na namna ya utumwa ulivyokuwa ni “mabaamedi.”Pasipo kuwadhalilisha,yayumkinika kusema wengi wa dada zetu hawa wanatumikishwa kwa namna mmiliki wa baa anavyotaka ilhali mshahara wanaopewa ni mdogo sana kiasi kwamba “wasopochangamkia wateja” wanaweza kujikuta wanapoteza muda wao kufanya kazi hapo baa.Hili ni kundi ambalo limesahaulika kabisa kwenye sheria za kazi.Tafiti zangu zisizo rasmi wakati nikiwa huko nyumbani zilionyesha kuwa tofauti na hisia kwamba akinadada hao hupenda “kuondoka na wateja wao” kwa hiari baada ya kumaliza kazi,ukweli ni kwamba wengi wao hulazimika kufanya hivyo ili angalau kupata nauli ya kurudi nyumbani na kujia kazini siku inyofuata au kujiongezea kipato kwenye mishahara kiduchu wanayolipwa na wenye baa,mishahara ambayo haitoshi kulipia kodi za nyumba wanazoishi,haitoshi kwenye nauli ya kwenda na kurudi kazini,na haitoshi kwa vile mara nyingi huwa inakatwa kutokana na “demeji” ya chupa au glasi.

Wakati Waingereza na wapenda ubinadamu wengine wanaadhimisha miaka 200 ya kutokomezwa biashara ya utumwa,ni jukumu la jamii yetu yote inayothamini ubinadamu kufanya kila siku iwe ya mapambano dhidi ya uonevu,unyanyasaji,utumikishwaji na utumwa.Hebu tuungane kuwafanya mahauzigeli,mabaamedi,“mateka wa ma-Pimp” na wale walio katika “ndoa za kijeshi” wawe huru kama ambavyo mie na wewe tunavyopenda kuwa huru.

Alamsiki

Wednesday, 21 March 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-55

Asalam aleykum,

Kwanza nianze na pongezi zangu kwa Chama Tawala (CCM) kwa kuibuka kidedea huko Tunduru.Kama ilvyotarajiwa,vyama vya upinzani vilivyoshiriki katika uchaguzi huo mdogo vimekimbilia kulalamikia “mchezo mchafu.”Pengine wanachopaswa kukumbuka ni kukubaliana na wajuzi wa siasa ambao wanaitafsiri siasa kuwa “mchezo mchafu.”Lakini pia wanapaswa kuelewa kuwa wanapouelezea ushindi wa CCM kuwa umetokana na mchezo mchafu wanatakiwa wakumbuke kuwa kimsingi ushindi katika uchaguzi wowote ule hautokani na matakwa ya chama pekee bali maandalizi ya kutosha,ya kisayansi na mbinu ambazo zinakiwezesha chama kutabiri matokeo hata kabla hayajatangazwa.Wote tunafahamu kuwa CCM huwa makini sana linapokuja suala la uchaguzi.Chama hicho hukusanya nguvu zake zote kuhakikisha kuwa ushindi unapatikana.Bila kukusudia kuvivunja nguvu vyama vya upinzani,yayumkinika kusema kwamba CCM itaendelea kushika hatamu kwa miaka mingi sana ijayo.Na kikubwa kitachochangia hilo ni maandalizi mazuri,umoja na mshikamano bila kusahau kuitumia vizuri nafasi ya upinzani dhaifu nchini.Sina budi kusema “CCM Oyee!!!” kama pongezi zangu japo mie sio mwanachama wa chama hicho.

Tukuiachana na habari hizo za uchaguzi,leo nataka kuangalia hali ilivyo nchini Zimbabwe.Mpaka kesho wengi wetu tunakubuka jinsi uhuru wa nchi hiyo ulivyolisismua bara za Afrika na pengine dunia kwa ujumla.Wapenzi wa muziki watakumbuka kuwa sherehe za uhuru wa nchi hiyo zililiwezesha bara letu kupata ugeni mahsusi wa mfalme wa muziki wa reggae hayati Bob Marley.Na licha ya ziara hiyo,Bob na kundi lake la The Wailers waliamua kutunga kibao mahsusi cha “Zimbabwe” ambacho hadi keshokutwa bado kinapendeza ukikisikiliza.Kwa hakika,uhuru wa nchi hiyo ulifungua sura mpya sio tu kwa Wazimbabwe bali kwa wapenda uhuru na amani sehemu nyingi duniani.

Leo hii mambo yako tofauti kabisa katika nchi hiyo.Kwa mtizamo wangu na ujuzi wangu mdogo kama mchambuzi wa siasa (political analyst) nashawishika kumtupia lawama nyingi kiongozi wa nchi hiyo Robert Mugabe.Tatizo kubwa la Mugabe ni uchu wake wa madaraka.Yaani anaiendesha nchi hiyo kama kampuni yake binafsi,anapindisha sheria anavyotaka kuhakikisha kuwa anaendelea kukalia madaraka na anaendelea kuwapa mateso wananchi wake kwa kung’ang’ania sera mufilisi ambazo zimeiacha nchi hiyo masikini wa kutupwa huku maelfu kwa maelfu ya Wazimbabwe wakikimbilia nchi za nje kutafuta hifadhi.

Mwanzoni nilikuwa naafikiana na sera zake za kupora ardhi wazungu na kuwagawia wazawa.Sera ilikuwa nzuri,ila inaelekea ilikuwa ni ya kukurupuka zaidi pasipo kufikiria matokeao yake.Inapaswa kufahamu kuwa nchi nyingi zilizopitia ukoloni haziwezi kufuta moja kwa moja baadhi ya matokeo ya ukoloni.Nachomaanisha hapo ni kwamba hatuwezi kubomoa mashule,barabara,nk kwa vile tu vilitengenzwa na mkoloni.Bahati mbaya baadhi ya wenzetu walijikuta wanapata uhuru huku kukiwa na idadi kubwa kidogo ya wakoloni walioamua kubaki kwenye makoloni hayo huru.Wengi tunafahamu kuwa Kenya iliendelea kubakiwa na idadi kubwa ya wakulima wa kizungu baada ya kupata uhuru kama ambavyo wengi wa makaburu walivyoamua kubakia Afrika Kusini baada ya kung’olewa kwa siasa za kibaguzi.Pamoja na ukweli kwamba bado kuna matatizo ya hapa na pale lakini nchi hizo nilizozitaja na nyinginezo zimefanikiwa kwa kiasi kikubwa kuwajumuisha wakoloni hao katika mifumo yao ya kiuchumi na kisiasa.

Hivi hadi leo Wazimbabwe wamenufaika vipi na mbinde ya Mugabe ya kuwanyang’anya ardhi wazungu?Wapo ambao maisha yao yalikuwa yanategemea mashamba hayo ya wazungu,na kuwatimua hapo pasipo kuwatafutia ajira mbadala ni sawa na ulevi.Yayumkinika kusema kuwa wazungu hao walikuwa na mchango flani katika uchumi wa Zimbabwe.Sasa kilichopaswa kufanyika kabla ya kuwapora ardhi ni kuangalia namna ya kuziba pengo ambalo kwa vyovyote lingejitokeza baada ya kunyofoa kigezo kimoja kinachochangia uchumi wa nchi.

Lakini kinachokera zaidi ni namna Mugabe anavyowapelekesha wapinzani wake.Awali nilikuwa naamini kuwa wapinzani kama Tsavingirai ni vibaraka wa nchi za Magharibi,lakini mtizamo huo ulibadilika baada ya kusikia mawazo ya baadhi ya Wazimbabwe kadhaa niliobahatika kukutana nao hapa.Mugabe anatumia kila nafasi aliyonayo kuhakikisha kuwa anabaki madarakani utadhani yeye ni rais wa maisha.Hilo la kubaki madarakani linaweza kuwa poa iwapo hataendeleza kampeni yake ya mkono wa chuma kuwapondaponda wale wote wanaonekana kuwa na mawazo tofauti na dikteta huyo.

Linalosikitisha zaidi ni namna gani Umoja wa nchi za Afrika (AU) ulivyoshindwa kabisa kuisaidia nchi hiyo isielekee pabaya zaidi.Jitihada zilizofanywa na Rais Kikwete hivi majuzi ni za binafsi na licha ya kupaswa kupongezwa zinapaswa pia kuifanya AU ijisikie aibu kwa namna ambavyo imekuwa kama dude flani ambalo halina uwezo wowote wa kutatua migogoro katika bara letu la Afrika.Wakati naandakaa makala haya nimesmsikia Tony Blair akiongea bungeni kwamba nchi za Afrika zinapaswa kufahamu kwamba matatizo ya mmoja wao yanawaathiri wote kwa namna moja au nyingine.Na hilo ni kweli kwa vile hadi leo sie tunabeba mzigo mkubwa wa wakimbizi kisa ni mamtatizo ndani ya nchi wanazotoka.Kwa AU kuendelea kutoa matamko yasiyo na nguvu huku Somalia inaendelea kuteketea,Darfur inazidi kuwa uwanja wa mauaji,ubakaji na ukiukwaji wa haki za binadamu,na Mugabe anaendelea kuwatumia mkono wa chuma kuipeleka nchi yake kusikoeleweka,ni sawa kabisa na kumpigia mbuzi gitaa:hatacheza.Ndio maana huwa napatwa na usingizi naposikia baadhi ya wanafalsafa wa Kiafrika wanapodai kuwe na taifa moja litakalounganisha nchi zote za Afrika (the united states of Africa).

Ni jukumu la AU kuhakikisha kuwa mambo yanarekebika nchini Zimbabwe.Damu ya wasio Wazimbabwe iliyotumika sambamba na ile ya Wazimbabwe katika harakati za uhuru wa nchi hiyo zisiachwe kupotea bure kwa vile tu mtu mmoja anataka kuwa madarakani milele.Kwa Mugabe,ujumbe kubwa ni kwamba tamaa zake za madaraka zinaendelea kuwatesa wananchi wake.Pia anapaswa kufahamu kuwa ipo siku atatoka madarakani,iwe kwa njia za kidemokrasia au kwa ubabe.Pengine ni vema akafikiria maisha yake ya baadaye yatakuwaje kwa vile hao wanaoteseka kwa ajili yake wanaweza kummeza pindi “ataporejea mtaani.”

Jingine dogo ambalo linanigusa zaidi mie binafsi ni habari kuwa hatimaye mto Kilombero umepata kivuko kipya.Hizo ni habari njema sana kwa wakazi wa Wilaya za Ulanga na Kilombero kwa vile kivuko hicho ni muhimu sana kwa maisha yao ya kila siku.Nitamke bayana kuwa pamoja na kukaa kwangu Ifakara miaka kadhaa sikuwahi kwenda ng’ambo ya pili ya mto Kilombero (upande wa Wilaya ya Ulanga) kwa vile kivuko chenyewe kilitaka ujasiri wa namna flani kabla hujajitosa ndani yake.

Mwisho,ni pongezi zangu kwa watani wetu wa jadi wa mtaa wa Jangwani.Ushindi wao hapo Dar na baadaye huko Angola ni habari za kufurahisha kwa kila Mtanzania asiyependa kuiona nchi yetu ikiwa kichwa cha mwendawazimu.Mechi iliyo mbele yao ni ngumu kwa ni hao Watunisia ni watu waliozowea kushinda kwa gharama yoyote ile.Hata hivyo,hakuna lisilowezekana katika soka.Kwa vile watakapopambana watakuwa 11 kila upande basi ni suala la mbinu na maandalizi tu.Baadhi ya wachezaji wa Yanga waliwastaajabisha hata Wabrazil wakati timu ya Taifa ilipokuwa huko kwa mechi za majaribio.Naamini hao na wengineo ambao hawako timu ya Taifa,pamoja na “uchawi wa Micho” wanaweza kawaondoa Esperance na hata kufika fainali na mwishowe kutuletea kombe.Najiskia kusema “Yanga Oyeee!!!!”

Alamsiki



Wednesday, 14 March 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-54

Asalam aleykum,

Katika makala zangu nyingi nimekuwa nikijitahidi kuwakumbusha Watanzania wenzangu juu ya umuhimu wa kufanya kila liwezekano kuitunza hali ya utulivu na amani tuliyobarikiwa kuwa nayo kwa miongo kadhaa sasa.Na kwa hakika ni jukumu la kila mmoja wetu kuhakikisha kuwa hatutoi fursa kwa mtu yeyote kuichezea lulu hii adimu hasa tukizingatia kuwa takriban majirani wetu wote wanaotuzunguka wako kwenye songombingo moja au nyingine.Hakika,jiografia ya hali ya usalama barani Afrika,hususan eneo la Maziwa Makuu inasapoti kabisa “nickname” yetu ya KISIWA CHA AMANI.Lakini inaelekea kuna wenzetu ambao kwa namna moja au nyingine inaelekea wameshachoshwa na hii amani ya kila siku.Wanataka kufanya majaribio kuona nchi inakuwaje pindi amani ikitoweka.Ni vizuri tukakumbushana kwamba wakati inaweza kuchukua karne kadhaa kujenga amani,amana hiyo adimu inaweza kupotezwa na wazembe wachache kwa siku kadhaa tu.Na kamwe tusiruhusu hilo litokee kwa gharama yoyote ile.

Majuzi,aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Tabora Braza Ditto alipewa dhamana na mahakama katika kesi inayomkabili ya kuua bila kukusudia.Kwamba dhamana ni haki ya kila mshtakiwa,hilo halina mjadala.Kama alivyosema Waziri wa Usalama wa Raia Bakari Mwapachu kwamba ukiwa na mawakili wazuri basi kuna uwezekano wa mshtakiwa kupatiwa dhamana mapema kama ilivyotokea katika kesi ya Braza Ditto.Labda la kujiuliza ni kwamba ni wangapi kati yetu wenye uwezo wa kuajiri mawakili waliobobea ambao kimsingi gharama za huduma zao ziko juu sana.Na kama suala ni la mawakili wazuri au waliobobea,je itakuwaje kwenye kesi za mahakama za mwanzo?Nadhani suala la msingi hapa sio mawakili bali ni kwa mahakama kutoa haki ya dhamana au kusikiliza kesi mapema bila kujali uwezo wa mshtakiwa.

Kesi ya Braza Ditto imekuwa na mvuto wa kipekee.Binafsi,nilishtuka sana niliposikia yaliyomsibu Mkuu huyo wa zamani wa Mkoa wa Tabora.Yayumkinika kusema kuwa wengi tulimuonea huruma mwanasiasa huyo hasa kwa vile ni mtu mcheshi, “mtoto wa mjini” na hutochoka kusikia stori zake.Nadhani wale wanaolalamika kwa hisia kuwa kesi yake imeharakishwa sana hawafanyi hivyo kwa vile hawampendi Ditto bali wangependa kuona kesi zote zinaharakishwa.Binafsi namfananisha Ditto na Makamba.Yaani ni mwanasiasa ambaye ana mvuto wa aina flani.Ditto ni miongoni mwa wanasiasa ambao ungependa kuwasikia muda wote na anajua kuichangamsha hadhira yake.Nitamke bayana kuwa niliposikia yaliyomkuta,hisia yangu ya kwanza ilikuwa kuamini kwamba kila binadamu ana “siku yake mbaya.”Bila kutaka kuingilia uhuru wa mahakama kuhusu kesi yake,nashawishika kuamini kuwa mauaji hayo hayakuwa ya kukusudia kama yalivyobadilishwa na wanasheria wa serikali.Na ukiangalia kwa makini sana matendo ya Ditto tangu akutwe na janga hilo unaweza kukubaliana nami kuwa hajafanya jitihada yoyote ya kutaka kutumia umaarufu wake kisiasa kupindisha mkondo wa sheria.Huwezi kumlaumu yeye kwa kubadilishiwa mashtaka wala kuharakishwa kwa dhamana yake.Ukweli kwamba yeye mwenyewe ndiye aliyewapigia simu polisi kuwajulisha kuhusu mauaji unaeleza jinsi gani alivyokuwa na busara katika kulishughulikia sakata hilo.

Ilianza na kubadilishwa mashtaka yanayomkabili ambapo japo sikuwahi kusikia malalamiko yoyote,mtu mmoja alikurupuka kudai kuwa mashtaka hayo hayakubadilishwa kwa vile Ditto ni mtu maarufu.Ukiona mtu anakimbilia kujitetea kabla hajalaumiwa basi ujue aidha anaogopa balaa flani au kitu flani hakiko sawia kama kinavyoonekana.

Mimi sio mtaalamu wa sheria za mahakama au jela kwa hiyo sijui kama ilikuwa sawa au la wakati tulipokuwa tunasoma kwenye magazeti kuwa mtuhumiwa huyo analetwa mahakamani kwenye gari tofauti na watuhumiwa wengine.Pengine ni suala la mtuhumiwa kuwa na uwezo wa kupata usafiri wake binafsi kumleta mahakamani.Lakini hilo si la msingi sana kwa vile cha muhimu sio usafiri anaojia mtuhumiwa mahakamani bali ukweli kwamba amehudhuria mahakamani hapo.Katika nchi za wenzetu,sio lazima kwa kila mtuhumiwa kuwa rumande wakati anasubiri kuanza kwa kesi yake au hukumu.Wapo watuhumiwa wanaotokea nyumbani kwenda mahakamani japo wana kesi kubwa zinazowakabili.Ila inapaswa kukumbukwa kuwa hawa wenzetu wana teknolojia na utaalam wa kutosha wa kuhakikisha kuwa mtuhumiwa hapotei kiajabuajabu.

Kwa polisi kumpitisha mtuhumiwa kwenye lango linalotumiwa na majaji inaonyesha ni jinsi gani watu tunaowategemea kulinda sheria wanavyoweza kuwa mufilisi wa mawazo pengine sio kwa vile wameelekezwa kufanya bali uoga wao tu.Hakuna uthibitisho wowote kuwa polisi waliofanya madudu hayo walipewa maelekezo ya kufanya hivyo.Kwa mantiki hiyo,ni aidha walikuwa wanajipendekeza au ipo namna flani ambayo mie na wewe hatuwezi kuielewa hivi hivi.Lakini kwa polisi kuwaruhusu wahuni flani kuwafanyia vurugu wanahabari ilhali wao (polisi) wakizubaa tu ni suala ambalo linapaswa kuangaliwa kwa mapana zaidi kwani ni sawa na kupandikiza virusi vyenye sumu kwenye suala zima la usalama na amani kwa raia.Nasema “kuruhusu” kwa vile polisi hawakuchukua hatua yoyote kuzuia uhuni huo.Lakini ukisikia bosi wao anajitetea kuwa eti ilikuwa vigumu kwa polisi kutofautisha ndugu wa Ditto na waandishi wa habari unabaki mdomo wazi.Ina maana hata hao waliokuwa na kamera ya kurekodia picha za televisheni nao walioonekana kuwa ni ndugu za Ditto?Huo ni utetezi dhaifu ambao haukupaswa kutolewa na kwa namna flani umeharibu hata ile samahani iliyotolewa kwa wanahabari waliokumbwa na zahma hiyo.

Lakini pengine watu ambao wanapaswa sio tu kulaumiwa bali pia kuchukuliwa hatua kali ni hao ndugu wa Ditto waliofanya vurugu mahakamani.Wanapaswa kufahamu kuwa baadhi ya maneno waliyokuwa wanasema sio tu yanaweza kuathiri mwenendo mzima wa kesi hiyo bali pia yanachafua majina ya baadhi ya watu ambao hata kama ni marafiki wa Braza Ditto hawakuhusika na uamuzi wa dhamana kwa mshtakiwa huyo.Kujigamba kuwa “wao ndio wenye nchi…” sio kauli nzuri na natumaini hivi karibuni mwenye busara mmoja miongoni mwao atajitahidi kuomba radhi na kurekebisha kauli za kihuni kama hizo.Wakumbuke kuwa moja wa wahusika wakuu wa kesi hiyo ni marehemu,na kifo chake (licha ya kuwa bila ya kukusudia kama tunavyoelezwa) kilisababishwa na mhusika mwingine ambaye yuko hai na huru.Hivi wanadhani wafiwa wanalijisikiaje wakati wao (ndugu za Ditto hapo mahakamani) walipokuwa wanatoa kejeli zao?

Naamini kabisa kuwa Braza Ditto mwenyewe anataka haki itendeke lakini matakwa hayo yanaweza kuathiriwa na jinsi hao wahuni wanaojiita ndugu zake wanavyoendesha mambo yao bila kutumia akili.Ifahamike kuwa kupatikana kwa haki hakumaanishi lazima mtuhumiwa apatikane na makosa,au akipatikana na makosa lazima aende jela.Kanuni muhimu ya kisheria ni sio tu kutendeka kwa haki bali haki ionekane imetendeka.Na ili hilo liwezekane pasipo kinyongo au malalamiko ni lazima pande zote zinazohusika na kesi hiyo ziheshimu utawala wa sheria.Wahuni waliosababisha vurugu mahakamani hapo ndio chanzo halisi cha hii migomo baridi iliyoanzishwa wa mahabusu wanaopinga kesi zao kuendeshwa kwa mwendo wa kinyonga huku ile ya mwenzio imepelekwa kwa kasi ya radi.Wahuni hao wamesababisha kuleta hisia kwamba kwa “wenye nchi” kila kitu kinakwenda “fasta” japo kimsingi uamuzi wa dhamana kwa Ditto umefuata misingi ya sheria kwa vile ni haki yake kwa mujibu wa kesi inayomkabili.Hilo la “kasi ya radi” linaweza kuwa ni matokeo ya kuwa na wanasheria wanaojua wanachokifanya mahakamani.Naungana na kauli ya Jaji Mkuu aliyoitoa huko Tabora kuhusu umuhimu wa kuheshimu sheria (na taasisi za kisheria) na kutowafumbia macho wale wanaotaka kuichezea.Ikumbukwe kuwa pasipo sheria ni vurugu na penye vurugu hao wanaodhani ni “wenye nchi” wanaweza kujikuta hawana pa kufanyia nyodo zao kama walivyofanya pale mahakamani.

Alamsiki


Categories

Unordered List

Sample Text

Blog Archive

Labels

Follow Us on FaceBook

Popular Posts

Recent Posts

Recent Comments

Recent Premium Themes

Your Links

Flickr

Powered by Blogger.

Blog Archive

Followers

Download

Your Links

Blogger Tricks

Popular Posts

Recent Posts

Text Widget