Thursday, 26 June 2014

 
 
Ziara ya Makamu wa Rais wa China, Li Yuanchao, nchini Tanzania imeambatana na tatizo la lugha, ambapo kiongozi huyo amekuwa akihutubia hadhara mbalimbali kwa Kichina pasipo mtafsiri wa Kiswahili.


Wednesday, 25 June 2014

Serikali imetangaza  kodi ya ongezeko la thamani (VAT) kwa MAJENEZA
KWA kila anayefuatilia makala zangu kwa karibu hatashindwa kubaini kuwa moja ya vyanzo vya mada za makala hizo ni kwenye mijadala mbalimbali ya mitandao ya kijamii, hususan twitter. Mara kadhaa nimekuwa nikipata cha kuandika katika makala hizi kutokana na mijadala hiyo inayohusu masuala mbalimbali.
Na kwa hakika, mitandao ya kijamii imekuwa na umuhimu wa kipekee kwangu hasa katika jitihada zangu za kukuza uelewa nje ya mazingira ya kitaaluma. Lakini pengine faida kubwa zaidi imekuwa katika kutengeneza marafiki muhimu kutoka nyanja mbalimbali za maisha. Nimefahamiana na wanasiasa, wasanii, wasomi, wanahabari na wengineo. Wakati kwa bahati mbaya au makusudi, baadhi ya watumiaji wa mitandao ya kijamii huko nyumbani (Tanzania) wameigeuza kuwa sehemu za kutafutia umaarufu kama sio kuwabughudhi wenzao, kwangu mitandao hiyo imekuwa fursa ya kutengeneza ‘mduara wa watu muhimu’ sambamba na ‘kisima cha kuchota elimu ya bure.’
Lengo la makala hii sio kuzungumzia umuhimu wa mitandao ya kijamii japo ningependa kuwahamasisha ‘wanaoikwepa’ watumie hamasa hii kuijaribu, na nina uhakika wataafikiana nami juu ya umuhimu wake. Makala hii inalenga kuzungumzia kinachoendelea huko Mashariki ya Kati, hususan nchini Iraq.
Nimeanza makala hii na umuhimu wa mitandao ya kijamii kwa sababu majuzi nilifanya maongezi na dada mmoja ambaye kwa asili ni Mkenya lakini ameishi sehemu mbalimbali duniani kutokana na wazazi wake kuwa wanadiplomasia. Nilifahamiana naye huko twitter hasa baada ya kuvutiwa na ‘tweets’ zake kuhusu masuala mbalimbali ya kimataifa. Kumbe pasi kufahamu, naye pia alikuwa akiguswa na ‘kelele’ zangu kuhusu maovu mbalimbali yanayoikabili Tanzania yetu.
Binti huyo ana uelewa mkubwa kuhusu siasa za Mashariki ya Kati, na kwa hakika ‘darasa’ alilonipatia kuhusu mapigano  yanayoendelea nchini Iraq kati ya waumini wa madhehebu ya Sunni na Shia lilinifungua upeo wangu zaidi ya nilivyokuwa nikielewa kupitia vyanzo vingine mbalimbali. Kikubwa zaidi, aliweza kwa ufanisi mkubwa kunifahamisha madhara ya kinachoendelea katika eneo hilo la Mashariki ya Kati na athari zake kwa nchi za Afrika Mashariki, hasa kwa sababu, kwa mujibu wa uelewa wake, uhusiano wa kidiplomasia kati ya baadhi ya mataifa ya eneo hilo na nchi za Afrika Mashariki umekuwa wa kimkakati (strategic) zaidi kuliko tunavyodhani (nitaongelea suala hili katika makala zijazo).
Lakini kubwa zaidi ni mjadala wetu kuhusu chanzo cha ukosefu wa amani nchi Iraq na jinsi kinachotokea huko kinavyoweza kulinganishwa na hali ilivyo katika nchi zetu, Kenya kwake na Tanzania kwangu.
Kwa mujibu wa taarifa za kiintelijensia za Marekani, Waziri Mkuu wa Iraq, Nouri al-Maliki, alikwishaonywa miaka miwili iliyopita kuhusu hisia miongoni mwa waumini wa madhehebu ya Sunni nchini humo kuwa wanatengwa. Hata hivyo, si Maliki wala serikali yake waliochukua hatua stahili kushughulikia tatizo hilo. Kimsingi, kuna lawama kadhaa zinazoelekezwa kwa Serikali ya Maliki kwa kushindwa kwake kujifunza kuhusu siasa za upatanishi (reconciliatory politics) kati ya Watutsi na Wahutu nchini Rwanda na Weusi na Makaburu nchi Afrika Kusini.
Miaka michache iliyopita nilipokuja huko nyumbani kwa ajili ya utafiti wa vitendo (fieldwork) kuchunguza kuibuka kwa ‘Uislamu wa msimamo mkali’ nchini Tanzania, moja ya hoja iliyojitokeza mara kwa mara ni hisia miongoni mwa Waislamu wengi kwamba wanatengwa. Nilizungumzia suala hili katika makala zilizopita lakini kwa sasa nadhani kuna umuhimu wa kuliangalia kwa kurejea kinachojiri nchini Iraq.
Kimsingi hisia hizo za kutengwa ni zaidi ya miongoni mwa baadhi ya Waislamu pekee. Hebu msomaji mpendwa angalia tofauti kati ya mbunge anayelipwa zaidi ya shilingi milioni 10 kwa mwezi na mlalahoi ambaye hana uhakika wa mlo wake wa siku inayofuatia. Unaweza pia kuangalia sekta ya afya ambapo watawala wetu wakipatwa na mafua tu wanakwenda ng’ambo kuangalia afya zao ilhali inafahamika kuwa hali ni mbaya sana katika takriban kila hospitali zetu.
Kilichonisukuma zaidi kuzungumzia suala hili ni taarifa kwamba katika jitihada zake za kuongeza mapato kwa ajili ya bajeti ya mwaka ujao wa fedha, Serikali imeanzisha kodi ya nyongeza ya thamani (VAT) kwenye majeneza. Hivi kweli Serikali yetu imeishiwa kabisa mbinu za kukusanya mapato hadi ifikie hatua ya kukifanya kifo kiwe ghali kiasi hicho?
Ndio, tatizo la waumini wa madhehebu ya Shia na Sunni nchini Iraq ni la kidini zaidi, lakini ukweli unabaki kuwa uwepo wa hisia za kubaguliwa, kutengwa, kunyanyaswa au kupuuzwa na watawala kunaweza kuzua balaa kubwa katika nchi husika.
Ikumbukwe kuwa pamoja na kuandamwa na tuhuma kuhusu ufisadi wa kampuni ‘feki’ ya Richmond kulikosababisha kujiuzulu, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, amekuwa akikumbushia mara kwa mara kuhusu kile Anachokiita ‘bomu la wakati,’ yaani tatizo la ukosefu wa ajira kwa vijana. La muhimu hapa sio kama ‘kelele’ zake ni za uchungu wa dhati au anasaka tu ‘kura za vijana,’ bali ukweli kwamba ukosefu wa ajira ni tatizo ambalo lisipopatiwa ufumbuzi wa haraka linaweza kuzua matatizo makubwa huko nyumbani.
Ninachojaribu kubainisha hapa ni jinsi mazingira ya baadhi ya wananchi kuhisi wanatengwa yanavyojengeka kama ilivyokuwa nchini Iraq. Sina maana wala kutabiri kuwa kinachojiri nchini humo kitatokea Tanzania, na Mola aepushe hilo, lakini ni vema kwa watawala wetu kutambua kuwa mazingira hayo ni kile Waingereza wanakiita ‘recipe for disaster.’
Tuna makundi mbalimbali katika nchi yetu yanayohisi kutengwa na watawala wetu. Haiingii akilini kwa Serikali kuamua kutoza VAT kwa majeneza badala ya kwa mfano, kupunguza safari mfululizo za Rais Jakaya Kikwete nje ya nchi ambazo zinatafuna mamilioni ya fedha za walipakodi. Ndio, Rais lazima asafiri lakini sio mara kwa mara, zaidi hata ya viongozi wa nchi tajiri kama Marekani ambazo zinamudu gharama za Rais kuwa ziarani hata kila siku ya mwaka.
VAT kwenye majeneza ni mkakati fyongo wa kuongeza mapato sio tu kwa vile karakana zinazotengeneza majeneza zinalipa kodi za uendeshaji biashara bali pia sio ubinadamu kuwa na ‘kodi ya kifo’ ilhali tungeweza kuokoa fedha nyingi tu kwa Serikali yetu kuwa na matumizi yanayoendana na umasikini wetu.
Nimalizie makala hii kwa kuwasihi watawala wetu wafumbue masikio na macho yao na kujifunza yanayojiri katika sehemu nyingine duniani kama huko Iraq kuhusiana na athari za mazingira ambapo makundi fulani katika kujiona yanatengwa, yanabaguliwa, yanadharauliwa au yanakandamizwa. Watanzania walio wengi hawatendewi haki na watawala wetu ambao ni wepesi wa kutoa ahadi zisizotekelezeka wakati wanaomba kura lakini wepesi wa kuchukua uamuzi unaowafanya watawaliwa kuhisi watawala hao wanaishi sayari tofauti kabisa (kwa mfano uamuzi wa VAT kwa majeneza).
Wito wangu kwa Rais Kikwete ni kuwaagiza watendaji wake waachane na ‘kodi hiyo ya laana’ ya VAT kwa majeneza. Ninarejea kumkumbusha kuwa amebakiwa na takriban miezi 18 tu madarakani kutengeneza legacy nzuri ya kukumbukwa na kuenziwa na Watanzania atakapostaafu hapo mwakani. Kadhalika, ninamsihi atumie muda huu uliobaki kufanya jitihada zaidi kuleta usawa kati ya makundi mbalimbali katika Tanzania yetu, hususan pengo linalozidi kukua kati ya wenye nacho na wasio nacho.
- See more at: http://www.raiamwema.co.tz/ipo-siku-watawaliwa-hawa-wataamua-%E2%80%98liwalo-na-liwe%E2%80%99#sthash.eJ7DR5WJ.dpuf

Friday, 13 June 2014

Tunaomba radhi kwa picha hizi ambazo ni graphic. Tumejitahidi kuficha sura ya marehemu
Mwili wa mtu aliyeuawa kutokana na shambulio hilo la bomu

Mtu mmoja ameuawa na wengine kadhaa kujeruhiwa katika shambulio la bomu karibu na msikiti huko Zanzibar. Kwa mujibu wa polisi, shambulio hilo lilitokea katika eneo la Stone Town kwenye sehemu ya biashara ya Darajani.

Mashuhuda wa tukio hilo walieleza kwamba miongoni mwa majeruhi ni waumini waliokuwa wanatoka kuswali katika msikiti ulio jirani na eneo hilo.

"Tunafanya uchunguzi kutambua aina ya bomu, waliohusika na shambulio hilo na lengo lao. Tunaomba wananchi kutupatia taarifa," alisema afisa mwandamizi wa jeshi la Polisi, Mkadam Khamisi.

Taarifa zaidi kuhusu tukio hili la kusikitisha zitawajia kadri zinavyopatikana

Wednesday, 11 June 2014

Wakati taarifa zinatanabaisha kuwa nchi yetu ipo hoi kifedha,

Embedded image permalink

 huku deni la taifa likizidi kupaa, na serikali ikikuna kichwa kutengeneza bajeti ya kueleweka kwa mwaka ujao wa fedha, 

Embedded image permalink
haya ndio matumizi ya viongozi wajuu wa chama Tawala CCM



CHANZO: Jamii Forums

Nakuachia wewe msomaji na kila anayeipenda Tanzania kwa dhati kutoa hukumu hapo mwakani katika uchaguzi mkuu.

Saturday, 31 May 2014

Licha ya kuwa sehemu muhimu za kubailishana mawazo, na pengine kufahamiana na watu mbalimbali, mitandao ya kijamii (social networks) ina upande wa pili ambao kwa hakika unaweza kuyafanya maisha yako yawe magumu mtandaoni. Pengine umeshawahi kusikia kuhusu watu wanaoitwa TROLLS. Pengine ushawahi kukutana nao, iwe Twitter au Facebook au hata Instagram. TROLL ni mtu anayeamua kukuandama kwenye mtandao wa kijamii pasipo sababu ya msingi.

Mara nyingi TROLLS humwandama mtu mwenye umaarufu bila kujali umaarufu huo unatokana na nini. Mtandao wa kijamii unaopendelewa zaidi na TROLLS ni Twitter. Na mara nyingi TROLLS humwandama mtu mwenye followers wengi, pengine lengo likiwa ni kusababisha madhara makubwa kwa mtu huyo. Hapa ninamaanisha kuwa kwa mfano TROLL anapo-tweet kitu kibaya dhidi yako, anatamani watu wengi wakione. Sasa ukiwa na followers wengi, lengo la TROLLS kukudhalilisha linafanikiwa kwa kiasi kikubwa kwani kila follower wako ataona kitu hicho.

Kuna wanaotetea tabia hiyo chafu wakidai kuwa ni sehemu tu ya utani huku wengine wakidai ni uhuru wa kuongea (freedom of speech). Lakini ukweli ni kwamba TROLLS husukumwa na kauli za chuki (hate speech). Katika mazingira ya kawaida tu, mtu anayekudhalilisha hadharani anakuwa na lengo moja tu: kukudhalilisha. Ndio, uhuru wa kujieleza (freedom of expression/speech) ni kitu kizuri lakini sote twafahamu kuwa hakuna uhuru bila wajibu. Huwezi kumwandama au kumdalilisha mtu hadharani kisha ukajitetea kuwa unatumia uhuru wako wa kujieleza. Uhuru wa kujieleza shurti uambatane na wajibu wa kutowabughudhi watu wengine.

Jana nimekumbana na TROLL mmoja huko Twitter. Huyu jamaa tulikuwa tunaelewana kitambo. Sio marafiki as such lakini mara nyingi tulikuwa tukijadialana kuhusu masuala mbalimbali. Yeye ni mwana-CCM, kwa maana ya kuisapoti CCM,ilhali mie sio kama ni mpinzani wa chama hicho tawala bali ninapinga matendo mengi yasiyopendeza, hususan ufisadi. Kwahiyo mara kadhaa mie na huyu ndugu tulikuwa tukijikuta katika malumbano ya hoja, japo mara zote yalikuwa ya kistaarabu.

Siku moja nikabaini kuwa ameni-unfollow. Nikiri kwamba nilishtushwa na uamuzi wake huo kwa sababu sikuwa na uhasama nae, na hata siku moja sikuwahi kutamka neno baya dhidi yake. Hata hivyo, niliheshimu uamuzi wake huo hasa ikizingatiwa kuwa awali ni yeye ndiye aliyeanza kuni-follow na mie nikam-follow back. Kwa maana hiyo, kama nafsi yake ilivyomtuma kuni-follow mwanzoni, niliamini kuwa nafsi yake hiyohiyo ndiyo iliyomtuma kuni-unfollow.Ila kwa hakika uamuzi wake huo wa kuni-unfollow pasi sababu ulinishangaza.

Nirejee tukio la jana. Hapa chini ndio tweet niliyoifahamu uwepo wake kupitia kwa dadangu yangu mmoja aliyenijulisha kwa Whatsapp, 


Huhitaji kuwa muelewa wa kauli za kashfa kutambua kuwa lengo la mtu huyu halikuwa jema. Ila kukuweka mahala pazuri kuelewa anachoongelea, ni vema nikiambatanisha maelezo na picha ya 'event' (tukio) anayoongelea. Jumatano ya tarehe 28 mwezi huu, nilialikwa jijini London kutoa mada katika semina kuhusu Rushwa na Haki za Binadamu nchini Tanzania. Semina hiyo iliandaliwa kwa ushirikiano kati ya Kundi la Wanasheria wa Kimataifa wa Haki za Binadamu (Solicitors International Human Rights Group) na Taasisi za Stadi za Juu za Sheria (Society for Advanced Legal Studies). Semina hiyo ilifanyika Institute of Legal Studies ya Chuo Kikuu cha London (University of London)

Pengine kutokana na kutokuwa na uelewa wa events zinazoendeshwa kitaasisi, mtu huyo alitamani kuona picha zangu nyingi nikiwa katika tukio hilo ili kuthibitisha kuwa kweli nilihudhuria na kutoa mada. Lakini licha ya ukweli kwamba sikwenda kwenye tukio hilo kwa ajili ya kupiga picha, pia mie kama mtoa mada ningeonekana kituko kuwa busy na kujipiga picha badala ya kutekeleza jukumu lililonipeleka hapo. Vilevile, yeyote anayeyafahamu vema maisha yangu mtandaoni atatambua kuwa sina tabia ya kujipiga picha, na kwa hakika picha zangu binafsi ni chache mno mtandaoni. Nina sababu zangu za msingi kutotaka kuweka picha zangu mtandaoni, na hilo ni suala binafsi.

Lakini hata tukiweka kando sababu nilizotoa hapo juu, mtu huyu ambaye awali alini-unfollow alikuwa anahitaji nini katika picha zangu? Je akishaziona zitamsaidia nini yeye? Na ukiangalia hiyo tweet yake utabaini ameweka inverted comas kwenye 'usalama wa taifa' kana kwamba mtajwa (mie) ninatumia ndivyo sivyo uhusiano wangu na taasisi hiyo. Sijawahi kuficha kuwa niliwahi kuwa mtumishi wa taasisi hiyo, lakini hilo ni suala langu binafsi ambalo sidhani kama linahitaji kumnyima raha mtu mwingine. Kuwa shushushu sio dhambi, na kwa hakika ninajivunia utumishi wangu katika taasisi hiyo kwa miaka kadhaa, sio kwa sababu ya 'ujiko' bali ukweli kwamba taaluma ya intelijensia inahusiana na kiwango cha juu kabisa cha akili (intelligence) na uzalendo. 

Kilichonisikitisha zaidi katika tukio hilo ni mtu mwingine aliyekuwa anani-follow na mie ninam-follow kuamua ku-RT (retweet) tweet hiyo ya kebehi. Huyu jamaa aliye-RT tuna historia ndefu kidogo. Awali tulikuwa 'marafiki' katika Twitter, ikatokea tukatibuana, nikam-block, lakini katika kuukaribisha mwaka mpya mmoja (nadhani mwaka juzi) alinisihi tusahau tofauti zetu na tuishi mtandaoni kwa amani. Nikam-unblock, na tukaendeleza 'urafiki' wetu huko Twitter. Nilitarajia kuwa kama 'rafiki' angetambua wazi dhamira ya mtu aliye-tweet kuhusu ushiriki wangu katika event hiyo ya London. Na kwa vile ninaamini ni mwelewa, angebaini pia kuwa kui-RT tweet hiyo sio tu kuna lengo la kunifikishia ujumbe bali pia ni kama ana lengo la kuisambaza tweet hiyo ninayoitafsiri kuwa ya kashfa (offensive/malicious)..

Ilinisikitisha kwa sababu kama nilivyoeleza awali, huyu ndugu tulikuwa marafiki, tukatibuana, nikam-block kwa sababu kama hii aliyotenda jana, akataka suluhu,nikaafikiana nae, lakini cha ajabu karejea hukohuko alikotoka. Huu si uungwana hata kidogo na ndio maana nimem-block tena, safari hile milele daima.

Huu ni mfano hai wa TROLLS, watu wanaoamua kukuandama pasi sababu ya msingi. Lakini tafiti mbalimbali zinabainisha kuwa wengi wa TROLLS ni watu wenye matatizo ya kiakili. Hawa ni watu wanaokerwa kuona mtu flani anakubalika kwa jamii (angalau katika mawazo yao), au anapiga hatua flani (na pengine si hatua bali mtizamo wao fyongo tu), au anapata sifa (na pengine sio sifa bali ni sehemu ya kawaida tu ya maisha ya mtu). Ni viumbe wanaosukumwa na chuki, watu wasiopenda kuona flani ana amani. Ni magaidi wa mtandaoni wanaosukuwa na chuki. Ni watu waliokosa kitu flani lakini wanataka kufidia pengo la walichokosa kwa kumwandama mtu aliyenacho. Kwa mfano, chuki ya TROLL yaweza kusababishwa na uhaba wa elimu na hivyo kuwaandama watu walioelimika dhidi yake.

Nieleze bayana kuwa sihitaji kuweka ushahidi wa nifanyacho maishani mwangu, iwe ni kuhudhuria semina, kutoa mada katika semina au jinsi ninavyoishi. Ninaamini kuwa masuala binafsi yanapaswa kubaki binafsi (private things should remain private). Sababu kubwa ya kutopendelea kubandika picha zangu mtandaoni ni hiyo. Sipendi kuyaweka maisha yangu binafsi hadharani. 

Lakini hata kama kulikuwa na umuhimu wa picha za tukio hilo kuwa hadharani (na taasisi husika itaziweka kwenye tovuti yake), kulikuwa na haja gani ya mtu au watu kutaka ushahidi wa picha hizo? Halafu kuna namna ya kistaarabu ya kutaka ushahidi badala ya kukimbilia kuhisi kuwa  "event ilibuma (haikufanikiwa, ni kitchen party..." na kushauri kui-Adobe (akimaanisha kutengenza picha feki za tukio hilo.

Binafsi sikumbuki idadi ya seminars, conferences,workshops na mikusanyiko mingine ambayo nimeshawahi kuhudhuria maishani. Ni mingi mno lakini cha muhimu sio idadi ya misanyiko ya aina hiyo bali umuhimu wake kwangu bainfsi na kwa jamii. Semina hiyo ya London ilikuwa na umuhimu mkubwa kwangu binafsi na kwa Watanzania kwa ujumla, kwa sababu mie binafsi nimekuwa nikijihusisha na vita dhidi ya rushwa na pia rushwa na ukiukwaji wa haki za binadamu ni matatizo sugu huko nyumbani.

Hivi kweli serioulsy mtu anaweza kushauri kutengeneza picha feki kwa Adobe ili kuidanganya jamii kuhusu ushiriki wake kwenye tukio flani? Ili iweje na imsaidie nani? Ama kwa hakika shule ni kitu muhimu sana. Kuna wenzetu wanaishi kwa SIFA na wanahangaika kusaka SIFA kwa gharama yoyote ile. Na kwa hakika, wakipata fursa kama hiyo niloipata juzi basi wangemwaga mapicha lukuki ya kila dakika ya uwepo wao hapo. 

Kama nilivyosema awali, kilichonipeleka katika semina hiyo ni umuhimu wake kwangu na kwa nchi yangu kwa ujumla. Kamwe sijawahi kufanya jambo kwa minajili ya kusaka sifa au maonyesho. Nilizaliwa na kukulia katika kile Waingereza wanakiita humble background. Na ukubwani, nikapata ajira inayohitaji 'maisha ya kificho' kwa aina flani. Simlazimishi mtu kunitafsiri tofauti, kwa sababu siishi kwa kumridhisha mtu flani bali Mola wangu pekee.

Mwisho, ni vema kwa mtu huyo kutambua madhara ya TROLLING. Pengine kwa huko nyumbani ni jambo la kawaida kumsambulia mtu mtandaoni pasi sababu lakini kwa wenye uelewa wa sheria za mtandaoni wanafahamu athari za kudhani ukiwa kwenye keyboard ya kompyuta yako una uhuru wa kuandika chochote kile hata kama kina madhara ya kisheria. Ukweli kwamba hakuna Mtanzania hata mmoja aliyewahi kuchukuliwa hatua za kisheria kwa 'kashfa mtandaoni' sio sababu ya kumwaminisha mtu kuwa kashfa mtandaoni sio kosa kisheria. Japo sitamani kuwa Mtanzania wa kwanza kumchukulia hatua za kisheria mtu anayenikashifu mtandaoni, lakini pindi ikibidi nitafanya hivyo ili iwe fundisho kwa kila anayedhani TROLLING ni ruksa kwa Watanzania.

Mwisho kabisa ni wito wangu kwa Watanzania wenzangu hasa mtandaoni. Tusikatishane tamaa kwa sababu ya chuki binafsi. Kama mtu anajituma kufanya jambo flani iwe lake binafsi au kwa maslahi ya taifa lake basi kama haiwezekani kumsapoti basi ni vema kukaa kimya tu. Kwanini ukerwe na jambo lisilokuhusu? Ni matumaini yangu kuwa waraka huu utasaidia sio tu kupunguza chuki zisizo na msingi mtandaoni bali utasaidia kuhamasisha mapambano dhidi ya TROLLS. Kamwe usiumie kimyakimya mtu anapokubughudhi mtandaoni, maana hicho ndicho kinachowapa nguvu TROLLS-kukuona unateseka kimyakimya. Ni muhimu kukabiliana nao hata kama silaha yao kuu ni kashfa na matusi. Kuna sheria kali tu dhidi ya watu wa aina hiyo, na ikibidi ni muhimu kujikinga au kutafuta haki kwa kutumia sheria hizo.

Pia napenda kuwashukuru TROLLS hao wawili, aliyepost tweet ya kejeli na huyo aliye-RT. Japo kitendo chao kimenisikitisha lakini kwa upande mwingine kimenihamasisha. You see, kama kuna mtu anakerwa na jambo zuri unalofanya kwa ajili yako au kwa ajili ya jamii, njia bora ya kumdhibiti sio kuacha jambo hilo bali kuliendeleza zaidi. Labda siku moja atachoka kuwa hater, au pengine atakufa kwa presha kutokana na mwendelezo wako katika jambo hilo.

I hope ujumbe umefika kwa wahusika, na samahani kwa waraka huu mrefu.

PEACE AND LOVE 


Thursday, 24 April 2014

NI dhahiri sasa kuwa mjadala wa Katiba mpya, hususan kipengele cha muundo wa Muungano, unaelekea kulipeleka taifa mahali pabaya. Japokuwa dalili za Bunge Maalumu la Katiba linaweza kuishia kuwa jukumu ghali kwa walipakodi masikini, hasa baada ya kusikika madai ya baadhi ya wajumbe wa Bunge hilo kuwa posho ya shilingi 300,000 kwa siku haitoshi, lakini Watanzania wengi walikuwa na imani kwamba ‘upepo huo mbaya’ ungepita na hali ingekuwa shwari.
Hata hivyo, kadiri siku zinavyozidi kwenda ndivyo hali inavyozidi kuwa mbaya. Kinacholeta wasiwasi zaidi kwa sasa ni kuibuka kwa dalili za ubaguzi wa waziwazi, sambamba na jitihada hatari za kumwaga petroli kwenye moto kwa kuingiza udini kwa nguvu kwenye siasa.
Lakini pasi ‘kuuma maneno’ naomba nielekeze lawama zangu kwa Rais Jakaya Kikwete na chama chake - CCM. Pamoja na wasiwasi uliokuwepo awali, kwamba huenda Rais Kikwete angeendeleza desturi iliyoota mizizi ndani ya CCM kwamba kila wazo lililoanzia vyama vya upinzani (kama hilo la umuhimu wa kuwa na Katiba mpya) ni baya, na hivyo angekwamisha uwezekano wa kupata Katiba mpya, alitushtua wengi alipoonyesha dalili za kuwa amepania kwa dhati kuweka historia kwa kufanikisha suala hilo muhimu.
Mambo yalionekana kwenda vizuri licha ya jitihada za hapa na pale ndani ya CCM kulifanya suala la Katiba mpya kuwa la kiitikadi zaidi kuliko la kitaifa. Wengi mtakumbuka vijembe walivyopigwa baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani walipotaka kukutana na Rais Kikwete. Badala ya kupongeza kile kilichoonekana kama mwanzo mpya wa siasa za maridhiano, baadhi ya wanasiasa huko CCM waliwakebehi wapinzani kuwa wanataka kwenda Ikulu kunywa chai tu!
Dalili za mwanzo kuwa hatma ya suala la Katiba mpya ipo shakani zilianza kujichomoza zaidi baada ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba, chini ya Jaji Joseph Warioba kuweka hadharani Rasimu ya Kwanza ya Katiba mpya, ambapo pendekezo la muundo wa Muungano wa Serikali tatu liliwekwa bayana. Taratibu, CCM, chini ya uongozi wa Kikwete, ilianza harakati za chini chini kujaribu kuingilia mchakato wa Katiba mpya, ikiwa ni pamoja na jitihada za kubinafsisha mchakato huo.
Lakini Mungu si Athumani au John, pamoja na vizingiti vya hapa na pale, hatimaye Rais Kikwete alitangaza majina ya wajumbe 201 kutoka makundi mbalimbali ya jamii, kuingia katika Bunge la Katiba. Lakini kabla ya hapo, tayari Rais Kikwete alishatangaza mkoani Mbeya wakati wa maadhimisho ya kuzaliwa kwa CCM kwamba msimamo wa chama hicho ni Serikali mbili. Japo alitangaza msimamo huo kama Mwenyekiti wa taifa wa CCM, katika mazingira ya kawaida tu, isingewezekana kuwapo kwa mitizamo tofauti kati ya Kikwete wa CCM na Kikwete Rais.
Kuanzia hapo ikawa kama ‘jini lililopo kwenye chupa’ (a genie in the bottle) limefunguliwa. Zikaanza harakati za waziwazi ‘kulazimisha’ matakwa ya chama tawala kwamba muundo wa Muungano lazima ubaki kuwa wa Serikali mbili. Mara zikapatikana taarifa kuwa CCM imetengeneza rasimu yake ya siri.
Mara tu baada ya kikao cha Bunge Maalum la Katiba kuanza, ishara kuwa hali huko mbele inaweza kuwa si shwari zikawa zinajitokeza kila kukicha. Baada ya mshikemshike wa madai ya posho, likaibuka suala la utaratibu wa kupiga kura (yaani kura zipigwe kwa usiri au uwazi.)
Lakini kwa vile tangu awali CCM walionyesha kuwekeza nguvu zao kubwa katika suala la muundo wa Muungano wakitaka Serikali mbili, suala hilo limeteka takriban kila kipengele cha Katiba mpya, na kwa bahati mbaya au makusudi, mjadala wa muundo wa Muungano unazidi kutishia umoja na mshikamano wa taifa letu.
Japo lugha za matusi na kashfa si jambo geni kwenye vikao vya Bunge la Jamhuri, hali imezidi kuwa mbaya kwenye kikao cha Bunge Maalumu la Katiba, tunasikia baadhi ya wajumbe wakiwatuhumu wenzao kuwa mashoga, huko wengine wakienda mbali na kuhoji Uafrika wa wenzao. Lakini kama nilivyobainisha hapo juu kuwa tumeshazoea matusi na lugha chafu bungeni, kuna waliokuwa na imani kuwa “wakimaliza kutukanana, watarejea kwenye suala lililowakutanisha huko Dodoma.”
Mara vikaanza kuibuka vitisho kuwa iwapo Katiba mpya itaridhia Serikali mbili, jeshi litatwaa madaraka. Na aliyeanzisha vitisho hivi si mwingine bali Rais Kikwete katika hotuba yake ya ufunguzi wa Bunge hilo la Katiba, wiki chache zilizopita.
Lakini wakati Rais Kikwete aliliongelea suala hilo katika jukwaa la kisiasa (bungeni), mmoja wa wasaidizi wake akaamua kulitoa suala hilo katika anga za siasa na kulipeleka kwenye nyumba za ibada. Hapa ninamzungumzia William Lukuvi.
Inaniwia vigumu kupata maneno stahili ya kumwelezea mwanasiasa huyo ambaye ghafla ametokea kuwa mtu mwenye kauli chafu, hatari na za kiharamia.
Huyu mtu bila aibu wala uoga amediriki kwenda kanisani na kutangaza waziwazi kuwa jeshi litaasi pindi uamuzi wa kuwa na Serikali tatu utakapopitishwa. Naomba nitamke bayana kwamba nahisi Lukuvi ana matatizo kutokana na hatua yake ya kwenda kanisani kufanya mahubiri ya kushawishi jeshi kuasi.
Lakini anayempa jeuri Lukuvi ni Rais Kikwete, kwani naye aligusia suala hilo kwenye hotuba yake ya ufunguzi wa Bunge la Katiba. Kwa hiyo anachofanya Lukuvi ni kusambaza tu ujumbe ulioanzishwa na Rais Kikwete.
Na wakati Rais Kikwete akiwakemea “wanasiasa wanaomtukana Nyerere na Karume” amekalia kimya matusi ya Lukuvi kwa Mwenyezi Mungu (naam, kutumia nyumba ya ibada kujenga chuki na kuhamasisha uasi wa jeshi ni matusi kwa Mungu.)
Ni watu wenye upeo mdogo tu watakaochukia kusikia kwamba Nyerere na Karume wana mchango katika matatizo tuliyonayo kuhusu Muungano, hasa kwa uamuzi wao wa kulifanya suala hilo kama lao binafsi bila kuangalia madhara yake miaka kadhaa ijayo.
Mara kadhaa Rais Kikwete amekuwa akiasa kuhusu athari za kuchanganya siasa na dini. Amewahi kudai kuwa kuna maadui wa nje wanaotumia suala la dini kwa minajili ya kututenganisha.
Lakini kipi cha kushangaza ilhali kwenye chaguzi kadhaa wamekuwa wakitumia nyumba za ibada kupandikiza chuki dhidi ya wapinzani wao?
Japo hainisumbui sana iwapo Katiba mpya haitopatikana, napata wasiwasi kuona uhuni wa kisiasa (political thuggery) ukihalalishwa kwa kisingizio cha ‘kuhubiri athari za Serikali tatu.’
Lakini nani wa ‘kuokoa jahazi’? Rais Kikwete anakemea wanaowatukana Nyerere na Karume, lakini anapuuza matusi ya wasaidizi wake kwa Jaji Warioba.
Nimalizie makala hii kwa kumkumbusha Rais Kikwete kwamba mwakani ataondoka madarakani na kurejea uraiani. Asipotengeneza mazingira mazuri kwake na kwa Watanzania, janga hili linalopikwa na akina Lukuvi litamwathiri naye pia.
Ni muhimu kwa Rais kuweka kando ushabiki wa kisiasa na kuchukua hatua za makusudi kuepusha nchi kutumbukia kwenye machafuko yanayochochewa na mahubiri ya ubaguzi na kuitumia dini kwa minajili ya kisiasa.

Thursday, 17 April 2014

NIANZE kwa kutoa pole kwa Watanzania kwa janga la mafuriko ambalo linaendelea kusababisha madhara makubwa katika maeneo mbalimbali huko nyumbani.
Japo taarifa zinazosikika zaidi kuhusu mafuriko hayo ni za hali ilivyo Jijini Dar es Salaam, taarifa zinaonyesha kuwa janga hilo linaendelea kusababisha madhara katika sehemu nyingine mbalimbali za nchi yetu.
Kwa vile Taifa bado lipo katika kipindi cha majonzi kufuatia wenzetu kadhaa waliokwishapoteza maisha kutokana na mafuriko hayo, sambamba na maelfu waliopoteza mali zao, inaweza kuwa si wakati mwafaka sana kuanza kunyoosheana vidole. Hata hivyo, kituko kimoja kilichojitokeza mwishoni mwa wiki iliyopita kinaleta haja ya kuwekana sawa wakati tunakabiliana na janga hili.
Jumamosi iliyopita, kulipatikana taarifa iliyoambatana na picha inayomwonyesha Mstahiki Meya wa Manispaa ya Ilala, Jerry Silaa, akiwasili mjini Mwanza kwa shughuli za kichama. Ikumbukwe kwamba siku hiyo hali ilikuwa mbaya sana Jijini Dar es Salaam kutokana na mafuriko yaliyosababishwa na mvua kubwa zinazoendelea kuonyesha sehemu mbalimbali huko nyumbani.
Ili kukupa mlolongo sahihi wa matukio, naomba ninukuu kauli husika kuhusiana na tukio hilo. Awali, kutokana na kushangazwa na uwepo wa Meya Silaa jijini Mwanza huku wananchi wake wakikabiliwa na janga la mafuriko, nilibandika picha iliyoambatana na maelezo
Meya wa Ilala Jerry Silaa katika shughuli za kichama muda huu huko Mwanza,” na kuuliza “Mheshimiwa, una taarifa za mafuriko Dar?” Kisha nikaandika tena, “Hawa ndio viongozi wenu. Manispaa ya Ilala ipo katika mafuriko, Meya wa Ilala Jerry Silaa yupo kichama Mwanza.
Baada ya muda mfupi, Meya Silaa alijibu, namnukuu,
Nakuomba radhi kama ungependa niwe Dar nikizuwia mvua isinyeshe.” Kisha akaandika tena “I hate cheap politics (nachukia ‘siasa nyepesi’). Mabonde yote yamejengwa. Mnategemea mito itapumulia wapi? I have remarkable record kwenye rescue missions (nina rekodi ya kupigiwa mfano kwenye jitihada za uokoaji.)” Lakini hakuishia hapo, akaendelea kudai kwamba, “Kwangu wahanga (wa mafuriko) ni kwa wanaoathirika kwa madaraja kukatika iliyosababishwa na watu kujenga mabondeni.” Na katika ‘kuhitimisha’ mjadala huo, Meya Silaa akatoa tuhuma kwamba “Najua viongozi wengi huwa wanaombea watu hata wafe wakabebe jeneza kuonekana wanajali lakini ni unafiki.”
Naomba niweke wazi ya kuwa sina tatizo na Meya Silaa binafsi ila kwa hakika kauli zake zilizosheheni dharau na kiburi zilinikera sana. Na si mimi pekee bali Watanzania kadhaa katika mitandao mbalimbali ya kijamii pia walishutumu kauli za kiongozi huyo wa Manispaa ya Ilala.
Hata hivyo, pamoja na ushauri wa wengi kwamba hata kama hakuwa na nia mbaya katika kauli hizo basi labda aombe radhi, Mheshimiwa huyo alipuuzia ushauri huo. Mie ni muumini mkubwa wa uhuru wa kujieleza. Hata hivyo, ni muhimu kutambua kwamba uhuru pasi nidhamu ni uhuni. Japo kila kiongozi ana uhuru wa kujieleza kama mwananchi yeyote yule, uhuru huo unaambatana na wajibu wa kiongozi husika kwa umma.
Kwa busara za kawaida tu, shughuli za kichama zilizompeleka Meya Silaa huko Mwanza hazikuwa na uzito mkubwa zaidi ya janga la mafuriko Jijini Dar es Salaam ambapo manispaa ya mheshimiwa huyo ilikuwa ni miongoni mwa maeneo yaliyoathiriwa sana.
Lakini busara zaidi zingeweza kutumika baada ya mheshimiwa kutambua kuwa suala hilo limezua hisia hasi miongoni mwa wananchi, na angeweza kujibu kistaarabu tu, kwa mfano, “ninatarajia kurejea Dar es Salaam  haraka kushirikiana na wananchi wenzangu katika janga hili” badala ya kauli ya kebehi kuwa ‘anaomba radhi kwa anayependa awepo Dar es Salaam  kuzuwia mvua isinyeshe.’
Hivi Rais Jakaya Kikwete alipofanya ziara ya maeneo mbalimbali yaliyoathiriwa na mafuriko hayo alifanya hivyo ili kuzuwia mvua au mafuriko hayo? Na je Makamu wa Rais Dk. Bilal na viongozi wengineo walionusurika katika ajali ya helikopta wakati wakitaka kuanza ukaguzi wa athari za maafa ya mafuriko walitarajia wangezuwia mafuriko hayo?
Ninaamini Meya Silaa anafahamu fika kwamba tunapokwenda kuwajulia hali wagonjwa haimaanishi kuwa tutawaponyesha, tunapokwenda misibani haimaanishi kuwa tutawafufua marehemu. Kumjulia hali mgonjwa au kujumuika msibani ni ustaarabu tuliyojijengea katika mila zetu kuonyesha kuwa TUNAJALI. Na kisaikolojia inaonyesha kuwa mhanga wa tukio lolote lile hupata faraja pindi anapotambua kuwa kuna wanaomjali.
Katika moja ya majibu yangu kwake, nilimfahamisha bayana Meya Silaa kwamba tatizo kubwa la wengi wa viongozi wetu ni kuzowea kusifiwa tu lakini wakikosolewa hukimbilia kudai ni ‘cheap politics.’
Waingereza wanasema “wrong is just that, wrong” (kisicho sahihi kipo hivyo hivyo, hakipo sahihi). Kiongozi kuzipa kipaumbele shughuli za kichama ilhali wananchi wanahangaika na janga la mafuriko si sahihi, na hakuna excuse katika mazingira ya aina hiyo.
Japo Meya Silaa anaweza kuwa sahihi kulaumu ujenzi wa mabondeni kama moja ya sababu zinazochangia mafuriko, lakini kwa hakika mamlaka husika kwa mfano Manispaa ya Ilala inayoongozwa na Meya Silaa zinahusika kwa namna moja au nyingine. Kuwalaumu tu wakazi wa mabondeni hakuwezi kuleta ufumbuzi wa tatizo. Ni muhimu kuelewa kwanini wakazi hao wa mabondeni wanaendelea kuishi maeneo hayo licha ya tishio la mafuriko.
Kwa uelewa wangu, wengi wao ni masikini ambao wanaoishi katika ‘nyumba za mbavu za mbwa’ na ni vigumu mno kwao kumudu kununua ama kujenga nyumba bora katika maeneo salama, achilia mbali huo uwezo wa kununua japo kiwanja.
Lakini eneo jingine ambalo pengine Meya Silaa hawezi kuligusia ni ujenzi unaokiuka taratibu za mipango-miji, unaofanywa na matajiri ambao fedha zao zinawawezesha kupindisha kila aina ya sheria. Wanaoishi mabondeni ni wahanga wanaathiriwa zaidi na kanuni za kiasili za maji kujaa kwenye mabonde, lakini ujenzi holela unaoathiri mfumo wa maji taka ni uingiliaji wa makusudi wa jitihada za binadamu kukabiliana na mafuriko.
Mvua ikinyesha maji yanajaa, na kwa vile mitaro inayopaswa kuyaongoza maji hayo katika maeneo maalumu imezibwa, maji hayo yatamwagikia eneo lolote lile, hata kama si bondeni.
Kuhusu kauli za Meya Silaa, nilimfahamisha kwamba ana bahati ni meya wa manispaa nchini Tanzania kwani laiti angekuwa  meya kwa hapa Uingereza, kisha akaenda mji mwingine kwa shughuli za kichama ilhali wananchi wake wanakabiliana na janga la mafuriko, kungekuwa na uwezekano mkubwa wa harakati za kumng’oa madarakani. Moja ya sifa ya uongozi si tu kujali wananchi bali pia kuonyesha uongozi hasa katika nyakati za majanga.
Kauli hizo zisizopendeza za Meya Silaa zimekuja katika kipindi ambacho Taifa letu lipo katika mchakato wa kupata Katiba mpya. Pengine tukio hili laweza kuwa angalizo muhimu kuhusu Katiba hiyo mpya.
Kwa mfano, je, Katiba hiyo itamwezesha mwananchi wa kawaida kumwajibisha kiongozi ‘mwenye kauli zisizofaa’? Suala hapa si tu katika kauli za kiongozi (iwapo zinafaa au la) bali suala zima la uwajibikaji.
Nimalizie makala hii kwa kurejea kauli ya Rais Jakaya Kikwete wakati alipofanya ziara katika maeneo mbalimbali kuangalia athari za mafuriko, kwamba “mafuriko hayaepukiki na wajibu wa Serikali ni kuwasaidia waathirika.”
Mafuriko kama maji kujaa kutokana na wingi wa mvua hayaepukiki, lakini mafuriko kama ukosefu wa miundombinu bora ya kukabiliana na mafuriko ni suala lililo ndani ya uwezo wetu. Kuna tofauti kati ya mafuriko yanayosababishwa na maji kuvuka kingo za Mto Kilombero huko Ifakara, na mafuriko katika maeneo yasiyo mabondeni jini Dar yanayochangiwa na mfumo duni wa kushughulikia majitaka.
Na japo ninaafikiana na kauli ya Rais kwamba wajibu wa serikali ni kuwasaidia waathirika (sijui ni wapi hao tukirejea kauli ya Meya Silaa) lakini kuna mengi yaliyo ndani ya uwezo wa serikali yanayoweza kupunguza idadi ya waathirika wa majanga kama mafuriko. Kubwa zaidi ni kujijengea uwezo wa kukabiliana na majanga badala ya kusubiri janga litokee ndipo tuanze kutafutana. 


Categories

Unordered List

Sample Text

Blog Archive

Labels

Follow Us on FaceBook

Popular Posts

Recent Posts

Recent Comments

Recent Premium Themes

Your Links

Flickr

Powered by Blogger.

Blog Archive

Followers

Download

Your Links

Blogger Tricks

Popular Posts

Recent Posts

Text Widget