Saturday, 17 June 2006

KULIKONI UGHAIBUNI:

Asalam aleykum,

Mwaka juzi gazeti maarufu duniani la TIME lilimtangaza George W.Bush kuwa “mtu wa mwaka (2004)” –au “Person of the Year” kwa lugha ya kwa mama.Katika uchambuzi wake kuhusu Bush,gazeti hilo lilimnukuu Rais huyo wa Marekani akisema kwamba “inapotokea kuwa hoja au mawazo yako yanazua mjadala au upinzani basi ni dalili kwamba yana uzito…kwa maana yangekuwa ya kipuuzi wala watu wasingejishughulisha nayo.”Alikuwa anazungumzia upinzani anaokumbana nao katika utendaji wa kazi zake za kila siku.Sio siri kuwa Bush anachukiwa na watu wengi hata ndani ya nchi yake.Lakini japo mie sio shabiki wake,namhusudu kwa jinsi anavyoweza kufanya mawazo yake yakubalike hata kwa wale ambao aidha hawayapendi au hawaafikiani nae.

Mwaka jana wakati nakuja huko nyumba,nilibahatika kukaa kiti kimoja na mama mmoja wa Kimarekani.Ni mtu mwongeaji sana,nami niliitumia nafasi hiyo kumdadisi siasa za Marekani hasa kuhusu mgawanyiko mkubwa wa kiitikadi nchini humo baina ya wale wa mrengo wa kulia(conservatives) na wale wa mrengo wa kushoto (liberals).Mwanamama huyo ambaye alinifahaisha baadaye kuwa ni mwanaharakati wa mazingira,alieleza kuwa kwa kiasi kikubwa mgawanyiko huo unachangiwa na siasa za Bush na maswahiba zake kama Dick Cheney,Donald Rumsfield,Paul Wolfowitz,na wengineo ambao wanajulikana kiitikadi kama “neo-conservatives” (sijui wanaitwaje kwa lugha yetu ya Taifa!).Miongoni mwa imani za hawa jamaa ni kuhakikisha kuwa Marekani inatumia ipasavyo nafasi yake kama Taifa lenye nguvu kabisa duniani.Kwa maana hiyo,ni “haki” yake kutumia “ubabe” wake kikamilifu ikiwa ni pamoja na kuvamia zile nchi zinazoonekana kuwa “korofi”.Ipo siku nitawazungumzia kwa kirefu jamaa hawa ambao takriban wote ni wadau wa taasisi moja isiyo ya kiserikali iitwayo “The Project for The New American Century” (Mradi wa Karne Mpya ya Marekani,kwa tafsiri isiyo rasmi).Turudi kwa yule mama.Basi akanambia kuwa japo yeye binafsi ni mpinzani wa Bush na hao neo-conservatives wenzake kuna wakati huwa “anamzimia sana” kutokana na jinsi anavyoweza kufanya maamuzi yake yatekelezwe hata pale kwenye upinzani mkubwa.Waingereza wana msemo “kama humuwezi unayeshindana nae basi bora uungane nae tu,”na ndio maana hata wale wasioafikiana na Bush mwishowe hujikuta hawana jinsi bali kuendana na mawazo au maamuzi yake.

Muda mfupi uliopita nilipata ujumbe kutoka kwa rafiki yangu flani aliyeko huko nyumbani akinijulisha kuwa kuna mwandishi mmoja ameandika makala katika gazeti flani la kila siku (la hapo Bongo) kupingana nami katika hoja ya makala yangu moja ya hivi ambayo nilimfananisha Rais Jakaya Kikwete na kiongozi wa chama cha Conservatives cha hapa Uingereza,David Cameron.Kwa mujibu wa ujumbe niliopata,mwandishi huyo aliyepingana nami anadai sikuwa sahihi kuwalinganisha wanasiasa hao .Kwa bahati mbaya hadi natayarisha makala hii nilikuwa sijapata hoja zote zilizotolewa kukosoa makala yangu.Kwa mantiki hiyo itakuwa vigumu kujibu hoja baada ya hoja bali nachoweza kusema kwanza ni kwamba makala ya mwandishi huyo ni uthibitisho tosha kuwa gazeti hili la KULIKONI ni kipenzi cha wengi,na ndio maana linazaa hoja na makala katika magazeti mengine.Pili,kama gazeti la TIME lilivyomnukuu Bush naamini makala yangu hiyo ilikuwa na uzito ndio maana ikamsukuma mwandishi huyo kuijadili japo hakuafikiana na nilichokiandika,kwa kuwa laiti ingekuwa ya kipuuzi asingepoteza muda wake kupingana nayo.”

Kwa faida ya mwandishi huyo,Kikwete anashabihiana sana na David Cameron katika maeneo flani.Kwa mfano,wote wawili wako katika vyama ambavyo kabla ya wao kushika hatamu za uongozi kwa kiasi flani vilikuwa vinaonekana kama ni vya “wateule wachache” tu.Ushindi wa tsunami kwa Kikwete ni dalili tosha kuwa hata baadhi ya wanachama wa vyama vya upinzani walimpigia kura kuonyesha kuwa kuteuliwa kwake kuwa mgombea urais kuliiongezea nguvu CCM.Hoja nyingine japo inaweza kuwa si nzito sana ni kwamba wanasiasa hao wana sifa inayofanana ya kuwa handsome,na kwa taarifa yako u-handsome unalipa sana kwenye siasa.Lakini kingine ni lugha zao wanazotumia.Wanaongea lugha za watu wa kawaida wa mtaani,yaani wanajua wananchi wanatarajia nini kwao.Ndio,Cameron anafuata siasa za mrengo wa kulia kuelekea kati (right-centre) na Kikwete kama mwana CCM nadhani atakuwa ni wa siasa za mrengo wa kushoto kuelekea kati (left-centre),na japo Cameron ni Mwingereza na Kikwete ni Mtanzania,la muhimu hapa ni jinsi wananchi wanavyowahusudu kutokana na utendaji wao.Kura za maoni hapa Uingereza zinaonyesha kuwa Cameron amempiku Tony Blair kwa kupendwa na wananchi na naamini kuwa hata kama Watanzania wataamshwa usingizini kupiga kura za maoni,Kikwete ataibuka kidedea kwa sana.Kwenye siasa umaarufu wa mwanasiasa haugemei sana kwenye itikadi zake au chama chake,sehemu aliyozaliwa au umri wake bali kukubalika kwake miongoni mwa wananchi,na hicho ndicho kilichonipelekea kuwafananisha wanasiasa hao.

Mwisho,siamini kuwa mwandishi wa makala hiyo alikuwa anatafuta umaarufu kupitia makala yangu au gazeti hili la KULIKONI,bali alikuwa anatumia haki yake ya kikatiba kutoa mawazo yake.Nampa changamoto aendelee kusoma gazeti hili ilimradi isiwe kwa nia ya kupinga kila kitu hata kama ameishiwa na hoja.Kama alivyoimba Mista Two (Joseph Mbilinyi) kwenye wimbo wake “Sugu” kwamba huwezi kuizuia mvua kunyesha,KULIKONI ni kama jua na mvua,halizuiliki.

Alamsiki.

KULIKONI UGHAIBUNI:

Asalam aleykum,

Hivi umeshawahi kuulizwa swali moja zaidi ya mara mia na kila unapoulizwa hujiskii kulizowea swali hilo?Pengine imeshakutokea.Mimi imekuwa ikinitokea mara nyingi zaidi ya ninavyoweza kukumbuka.Ilianza nikiwa huko nyumbani.Kabila langu ni Mndamba,natokea Ifakara mkoani Morogoro.Sio siri kuwa Wandamba sio kabila maarufu ukilinganisha na makabila mengine ya mkoa naotoka,kwa mfano Waluguru au Wapogoro.Kwa hiyo kila nilipokuwa naulizwa “hivi wewe ni kabila gani” na mimi kujibu “mie Mndamba” mara nyingi swali lililofuata ni “hivi Wandamba wanatoka mkoa gani?”Au wakati mwingine nilipoulizwa mkoa naotoka na kujibu Morogoro,wengi walipenda kudhani mimi ni Mluguru.Niliposema hapana,wangeniuliza iwapo ni Mpogoro.Sikuwalaumu kwa vile mara nyingi jina la mkoa unaotoka huwa linahusishwa na kabila kubwa au maarufu katika mkoa huo.Ukisema unatoka Mwanza,watu watahisi wewe ni Msukuma,ukitoka Songea watu watahisi wewe Mngoni,au Tabora watahisi wewe Mnyamwezi,na kadhalika.

Nilipokuja huku Ughaibuni swali likageuka kuwa “wewe unatoka nchi gani?”Mara nyingi napojibu “natoka Tanzania” swali linalofuata ni “hivi Tanzania iko wapi?”Wengine wanajua iko Afrika lakini hawana uhakika ni sehemu gani katika bara hiko lenye nchi zaidi ya hamsini.Kuna wakati huwa nawalaumu wanaoniuliza swali hilo kwamba hawakuwa makini kwenye somo la Jiografia,lakini yayumkinika kusema kuwa hata kama ulipata A kwenye somo hilo sio rahisi kujua kila nchi ilipo kwenye ramani ya dunia,kama isivyo rahisi kwa kila Mtanzania kujua Wandamba wanatoka mkoa gani.Hata hivyo,kila napoulizwa ilipo Tanzania,huwa natumia fursa hiyo kufanya kazi ya wenzetu tuliowapa majukumu ya kuitangaza nchi yetu kwa kueleza kuwa nchi hiyo “iko kusini mwa Kenya na Uganda,mashariki ya DRC,Rwanda na Burundi…”,na kadhalika.Wakti mwingine natumia vivutio vyetu kujibu swali hilo,yaani nasema kuwa “Tanzania ndipo ulipo Mlima Kilimanjaro,au Ziwa Victoria,au Mbuga ya Selous…”

Wakati sote tunajua kuwa ni vigumu kwa kabila Fulani kufanya kampeni ya kujitangaza (na jitihada kama hizo zikifanyika utaambiwa unaleta ukabila) kila nchi ina jukumu la kujitangaza yenyewe.Inauma ninapoangalia kwenye runinga na kuona matangazo kama hili hapa: “mtoto huyu anahitaji sana msaada wako…anapenda kujiendeleza na elimu lakini anatoka Tanzania,moja ya nchi masikini sana duniani…kwa kutoa paundi tatu kwa mwezi unaweza kuwasaidia watoto kama huyu…”Yaani nchi yetu inapata nafasi ya kusikika lakini sio kwa sifa nzuri bali umasikini wake.Na huwezi kuwalaumu wanaotoa matangazo ya aina hiyo kwa kuwa wanafanya hivyo kwa nia nzuri,na sio jukumu lao kuitangaza nchi yetu kwa mtizamo wa kuvutia watalii au vivutio vilivyopo huko.Hiyo ni kazi ya Watanzania wenyewe.

Naamini kuna watu wana majukumu ya kuitangaza nchi yetu.Hebu nikupe mfano.Uganda inadhamini kipindi Fulani kwenye kituo cha televisheni cha CNN International cha Marekani.Zambia nao wanatoa matangazo ya kuitangaza nchi yao kwenye kituo hicho na kuwakaribisha wageni waende kushuhudia Maporomoko ya Victoria.Hata Malawi,Rwanda na Burundi nao hawako nyuma,kwani nimeshaona matangazo yao kwenye gazeti maarufu duniani la TIME.Lakini sie tuko nyuma katika eneo hili.Pengine kuna watu wanaona sio muhimu kujitangaza kwa vigezo kwamba “chema chajiuza kibaya chajitembeza.”Tunachopaswa kufahamu ni kwamba katika zama hizi za ushindani wa kuvutia watalii (na hata wawekezaji wa kweli) ni muhimu sana kuitangaza nchi yako.Ukitaka kuhakikisha nayosema sio utani ingia kwenye internet na tafuta habari kuhusu vivutio vilivyopo nchini kwetu.Ni dhahiri utagundua kuwa taarifa zilizopo ni chache,na hata hizo chache hazijitoshelezi,na mara nyingi huwa zimewekwa na wasio Watanzania.Kuna watu wengi wanaoamini kuwa Mlima Kilimanjaro uko Kenya kwa vile nchi hiyo imekuwa ikiutangaza Mlima huo kama uko kwake,na sie tumekaa kimya.Ukienda kwenye tovuti ya Bodi ya Biashara za Nje (BET) wao wanaonekana wako bize zaidi na Maonyesho ya Sabasaba.Nilipotembelea tovuti yao leo ilikuwa inasema iko kwenye matengenezo lakini inakupeleka kwenye kiungo (link) ya Maonyesho ya 30 ya Kimataifa ya Dar Es Salaam (DITF),pengine kuonyesha kuwa Maonyesho hayo (ambayo ni ya mara moja tu kwa mwaka) ni muhimu zaidi kwao kuliko kuitangaza nchi yetukila siku.Angalau Bodi ya Utalii wamejitahidi kiasi japokuwa tovuti yao haina habari za kutosha kuhusu vivutio tulivyonavyo.Tuna Kituo cha Biashara (Tanzania Trade Centre) hapa Uingereza,lakini tovuti yake ni kama imeandaliwa haraka haraka kwa vile taarifa zilizopo humo sio za kutosha sana.Wahusika wasikasirike kusoma haya nayoandika kwa sababu tumewakabidhi dhamana ya kuitangaza nchi yetu.Badala ya kuchukia kukosolewa wanapaswa waone hii kuwa ni changamoto kwao.

Kilio changu kingine ni kukosekana kwa AIR TANZANIA ya Watanzania.Kama wenzetu Kenya wameweza kwanini sisi tushindwe?Angalia Wahabeshi wa Ethiopia wanavyoweza kuchuana na mashirika makubwa ya ndege duniani na kujiingizia mapato makubwa kupitia sekta ya usafiri wa anga na Ethiopian Airlines yao.Kwa kurusha Air Tanzania “the Wings of Kilimanjaro” tulikuwa tunaitangaza nchi yetu na wakati huohuo kuujulisha ulimwengu kuwa Mlima Kilimajaro uko kwetu.Tuna vivutio vingine vingi vya kuvitangaza huku nje ikiwa ni pamoja na moja ya hifadhi kubwa kabisa duniani,Selous,na ziwa la pili kwa ukubwa duniani,Victoria.

Tukubali kwamba hatujajitahidi vya kutosha na tusisubiri kuulizwa.Hatuna sababu ya msingi ya kuwa hapa tulipo,na kwa kuwa tunatambua kuwa hatujitendei haki sie wenyewe kwa kung’ang’ania kuwa katika nafasi isiyo yetu ni lazima tuchakarike sasa.

Alamsiki

KULIKONI UGHAIBUNI:

Habari za huko nyumbani

Mojawapo ya tofauti kubwa kati ya jamii ya hawa wenzetu na huko nyumbani ni namna uhuru wa kujieleza (freedom of expression) unavyothaminiwa.Of course,uhuru huo unaambatana na wajibu,kwa sababu kama wanataaluma wa kanuni za maisha wanavyosema,uhuru bila wajibu ni sawa na kukaribisha vurugu.Kadhalika,uhuru huo sio wa asilimia 100 (absolute),kwa vile hakuna kitu kama hicho duniani.Lakini ukilinganisha na huko nyumbani,yayumkinika kusema kwamba hawa wenzetu wana uhuru mkubwa zaidi wa kujieleza.Sambamba na hilo ni uhuru wa taasisi zinazopaswa kuujulisha umma nini kinaendelea katika jamii yao na hata nje ya jamii hiyo.Hapa nalenga zaidi kwenye taasisi za habari:hususan magazeti na vituo vya radio na runinga.

Kuna magazeti hapa ambayo ni mithili ya hayo yanayoitwa “ya udaku” huko nyumbani.Magazeti kama The Sun,News of the World,Daily Mirror,nk yamebobea sana katika kuibua skandali mbalimbali hapa Uingereza.Inapotokea kwamba habari flani imepotoshwa basi hao walioguswa na habari hiyo wataamua aidha kukanusha au kukimbilia mahakamani kudai fidia.Wakati mwingine watajwa kwenye habari hizo hulazimika kukiri makosa yao hadharani.Kwa mfano,juzijuzi iliripotiwa kuna Naibu Waziri Mkuu John Prescott alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na katibu muhtasi wake Tracey Temple.Katika sekeseke hilo ambalo bado halijatulia ilimzalimu Bwana Prescott kukiri kuwa yaliyosemwa na magazeti ni kweli.

Nakumbuka mwanataaluma mmoja huko nyumbani aliwahi kuvitaka vyombo vya habari kuwa na ujasiri wa kutaja majina ya watuhumiwa bila kuwa na hofu ya kuburuzwa mahakamani,iwapo vyombo hivyo vina uhakika na walinachoripoti.Hebu chukulia mfano wa habari kama hii: “kiongozi wa chama kimoja cha siasa kinachoanzia na herufi C anadaiwa kuwa na uhusianowa kimapenzi na mtangazaji flani ambaye jina lake linaanzia na herufi D…”Hivi habari kama hiyo si ni sawa na chemsha bongo kwa msomaji?Hali ilikuwa mbaya sana miaka ya nyuma kwa sababu ilikuwa ni vigumu mno kujua ni mtuhumiwa gani hasa anazungumziwa katika stori husika.Hata hivyo,kuna dalili kwamba mambo huenda yakabadilika hasa baada ya ujio wa magazeti jasiri ambayo yako tayari kwa lolote.Ukweli ni kwamba kama ushahidi upo wa kutosha hakuna haja ya kuficha jina la mhusika (labda ithibitike kuwa kumtaja kutaathiri uchunguzi,au kwa sababu za kimaadili).

Siyalaumu magazeti yanayoshindwa kutaja majina ya wahusika katika skendo flani japokuwa nayapa changamoto kufanya hivyo.Siyalaumu kwa sababu sio kosa lao,sio uoga,bali ni mazingira yaliyopo.Siasa za nchi yetu baada ya uhuru hadi mwanzoni mwa miaka ya 1990 zilikuwa zimegubikwa na usiri mkubwa.Kutaja madhambi ya kiongozi ilikuwa dhambi,na hapa tunazungumzia kuanzia ngazi ya mtaa hadi taifa.Usiri sio mbaya kama unatumiwa kwa manufaa ya wengi,lakini kwa bahati mbaya baadhi ya watu walikuwa wanautumia kuficha maovu yao.Waliofilisi mashirika ya umma walinufaika sana na siasa za usiri.Viongozi hawakuwa tayari kusikia kauli nyingine zaidi ya sifa,na kuwakosoa ilikuwa ni kujichimbia kaburi.Kwa hiyo,hali tuliyonayo sasa ni matokeo ya miongo kadhaa ya kuishi katika siasa za kusifia na si kukosoa.

Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni miongoni mwa maeneo ambayo yameathiriwa sana na kutokuwepo uhuru wa kutoa mawazo sambamba na uoga wa kuadhibiwa unapoongea kinyume na matakwa ya wakubwa.Nilikuwa sijazaliwa wakati mataifa haya yanaungana,na sijafanya utafiti wa kutosha iwapo Muungano huo ulifanywa kwa ridhaa ya wadau (wananchi) au yalikuwa ni maamuzi tu ya viongozi.Miaka nenda miaka rudi watu wamekuwa wakiongea “chini ya uvungu” kwamba Muungano huu una matatizo mengi tu japokuwa yanaweza kutatuliwa pale penye nia.Baadhi ya viongozi wamekuwa wanakwepa kuzungumzia matatizo yaliyopo kwa madai ya “kukwepa jinamizi la Muungano.”

Hivi karibuni kumekuwa na harakati za kisheria na kisiasa kuhusu Muungano.Kundi la Wazanzibari limefungua kesi kuhusu Muungano,Mchungaji Mtikila nae anaonekana kuukalia kooni Muungano,na viongozi wa serikali kutoka Bara walikutana na wale wa viswani kujadiliana kuhusu suala la Muungano.Juu ya hayo serikali ya awamu ya nne ina waziri anaeshughulikia suala la Muungano.Hata hivyo,kauli za Waziri Kiongozi wa Zanzibar Samsi Vuai Nahodha kuwa suala la mafuta ni la kisiwa hicho pekee,sio kitu cha kukiacha kipite hivihivi tu.Scotland,sehemu ya muungano unaounda United Kingdom (Uingereza) ina utajiri mkubwa wa mafuta.Lakini japokuwa kumekuwa na kelele za hapa na pale kuhusu muungano huo,utajiri wa mafuta haujawahi kuipa kiburi Scotland ifikirie kujitoa katika muungano huo au itumie mapato yote ya mafuta peke yake.Sasa kelele zimeanza hata kabla hayo mafuta hayajapatikana huko Zanzibar,je yakipatikana si ndio itakuwa mshikeshike!

Mimi nadhani suala la Muungano linazungumzika.Ikibidi kufanya kura ya maoni kujua matakwa ya sasa ya wananchi kuhusu Muungano,basi na ifanyike bila kuogopa matokeo yake.Siasa za kuogopana na kubembelezana zimepitwa na wakati,na iwapo itathibitika kuwa upande mmoja wa Muungano hauridhiki na muundo au kuwepo kwake,basi jitihada za dhati zifanyike kupata ufumbuzi.Tukiendelea na siasa za usiri na kujidanganya kwamba kila kitu kinakwenda vizuri,si ajabu siku moja Muungano huu ukavunjikia mahakamani.Hiyo itakuwa aibu sana hasa kwa wale wanaodai kukwepa “jinamizi la kuvunjikiwa na Muungano.”Inatokea huko Serbia-Montenegro,inaweza pia kutokea huko nyumbani iwapo wanasiasa wetu hawatafanya jitihada za makusudi.

Alamsiki

KULIKONI UGHAIBUNI

Asalam aleykum.

Hapa Uingereza kuna chama cha siasa kinachoitwa British National Party au kwa kifupi BNP.Hiki ni chama kinachofuata siasa za mrengo wa kulia kabisa,far right kwa “lugha ya mama.”Siasa za namna hiyo ndio zilizokuwa zinahusudiwa na Manazi chini ya Hitler na Mafashisti chini ya Mussolini.Hawa jamaa wa BNP ni wabaguzi waliokithiri.Majuzi wakati wa uchaguzi mdogo huko England mmoja wa watu muhimu katika BNP,Dokta Phill Edwards (jina lake halisi ni Stuart Russell) alizua mjadala mkubwa kuhusu siasa za chama hicho pale alipotoa matamshi ya kuchefua dhidi ya watu weusi.Alirekodiwa kwa siri na kituo cha televisheni cha Sky akisema kuwa watu weusi wana IQ (uwezo wa akili) ndogo,na watoto weusi wakikua sanasana wataishia kukaba watu (vibaka au majambazi).Aliendelea kusema,hapa namnukuu “suala hapa sio kama tunawachukia watu weusi bali ni kama wao ni tishio kwa amani,utulivu na utamaduni wa jamii ya Kiingereza…watoto weusi wakikua watanyonya uchumi wetu na kujaza magereza yetu na pengine kukukaba…huko Afrika kusini mwa jangwa la Sahara hakuna ustaarabu wowote,na hakuna maendeleo ya sayansi…”Kwa kweli ilikuwa inauma kuangalia upuuzi huo kwenye runinga,lakini ni hali tunayoishi nayo hapa kila siku.

Miongoni mwa mambo “halali” yanayowapa nguvu wabaguzi hawa ni vitendo vya baadhi ya wageni na hasa weusi kujihusisha na uhalifu au mambo mengine yasiyofaa katika jamii.Kwa wao,samaki mmoja akioza basi wote wameoza,yaani mtu mmoja mweusi akihusika kwenye uhalifu basi watu wote weusi ni wahalifu.Na kwa BNP sio weusi tu wanaolengwa.Chama hicho kilipata “pumzi” ya kutosha kupinga sera za uhamiaji na ujio wa wageni hapa Uingereza baada ya matukio ya kujilipua mabomu kwa kujitoa mhanga mjini London mwezi Julai mwaka jana. “Vita” ya BNP dhidi ya wageni ikapamba moto na sasa walengwa wakuu wakawa watu wenye asili Asia (hasa Wapakistani).Watatu kati ya waliojilipua mabomu ya muhanga walikuwa Waingereza wenye asili ya Pakistani,na kwa chama hicho cha kibaguzi hiyo ilikuwa sababu tosha ya kuwajumuisha watu wenye asili ya Pakistani na Asia kwa ujumla,na wageni wengine kuwa ni tishio kwa maisha ya Taifa hili.

Huko nyubani moja ya mambo ambayo Watanzania tunajivunia sana ni jinsi “tunavyojichanganya” bila kujali kabila,dini au jinsia.Nikisema “kujichanganya” namaanisha ushirikiano,upendo na maelewano,na sio kukosa msimamo kama maana halisi ya neno ilivyo.Niliwahi kusikia stori flani siku za nyuma inayohusu timu moja ya soka kutoka nchi flani ya jirani.Wachezaji wa timu hiyo walipokuwa wanafanya mazoezi walikuwa wanavuta umati mkubwa wa wakazi wa mji wa Arusha,ambako kulikuwa na michuano ya kimataifa.Kilichokuwa kinawashangaza wachezaji hao ni jinsi watazamaji walivyokuwa “wanajichanganya” kana kwamba ni watu wa kabila moja.Nchi wanayotoka wachezaji,kama zilivyo nchi kadhaa za Afrika,inasifika sana kwa ukabila.Inasemekana katika nchi hiyo ni nadra watu wanaotoka makabila tofauti kuwa marafiki wa dhati.Sasa walipoona baadhi ya watazamaji “wanagongeana sigara” na kutia stori kana kwamba wanaishi nyumba moja,ilikuwa ni jambo la kushangaza sana kwao.Huenda waliondoka Arusha wakiwa na fundisho flani.
Rafiki yangu mmoja,Profesa Tunde Zack-Williams,aliwahi kuniambia kwamba napaswa kujivuna kuwa Mwafrika kutoka Tanzania.Alinieleza kwamba kwa uzoefu wake mwenyewe kama mwanataaluma na Mwafrika,Watanzania ni watu waliojaliwa na “karama” ya mshikamano,upendo na umoja,na wanawaheshimu sana wageni bila kujali wanatoka wapi.Profesa huyo ni mzaliwa wa Sierra Leone,nchi ambayo imeathiriwa sana vita vya wenyewe,na amekuwa akiwasaidia sana kitaaluma vijana wa Kiafrika.Rafiki yangu mwingine anayetoka Sudan aliniambia kwamba alishangaa sana alipofika Tanzania kwa mara ya kwanza,kwa sababu licha ya nchi yetu kuwa na makabila zaidi ya 120 hakuona dalili zozote za watu kubaguana kwa misingi ya kikabila.

Hata hivyo,katika siku za hivi karibuni kumeanza kujitokeza dalili za baadhi ya watu kuchoshwa na “ujiko” huo tulionao ndani na nje ya Afrika.Binafsi,nafanya utafiti unaohusu masuala ya dini na siasa.Sintoongelea sana utafiti huo kwa vile bado “uko jikoni” lakini miongoni mwa matokeo yake ya awali ni dalili kuwa kuna watu au vikundi flani vya jamii vinavyotumia dini kujenga mpasuko katika jamii kwa manufaa yao binafsi.

Kibaya zaidi ni dalili kwamba baadhi ya Watanzania ambao tuna haki ya kuwaita “wageni” wanapoanza kujiingiza kwenye kuleta chokochoko kwenye jamii yetu iliyozowea amani.Siku zote tumekuwa tukiheshimiana na kupendana bila kujali kuwa flani alizaliwa Ifakara au New Delhi.Lakini kama BNP inavyopata “nguvu halali ya kusema ovyo” pindi wageni “wanapoharibu” inaweza kufika mahali Watanzania wazawa wakaanza kujenga chuki dhidi ya wale ambao licha ya “ugeni” wao wanachochea mpasuko katika nchi yetu.Na si “wageni” tu bali hata wale wanaotumia nafasi zao za juu katika jamii kutukoroga.Waasisi wa Taifa letu walifanya kazi kubwa sana kutufikisha hapa tulipo,na nawausia Watanzania wenzangu tusifumbe macho pale wale tulikowakaribisha kwa upendo (na maswahiba zao) wanapoanza kutuletea dharau na chokochoko kwenye nchi yetu.

Alamsiki

KULIKONI UGHAIBUNI:

Asalam aleykum wasomaji wapendwa wa gazeti hili.

Leo tuzungumzie muziki.Muda mfupi uliopita nilikuwa nasoma makala flani kumhusu msanii wa kizazi kipya Albert Mangwea.Yalikuwa ni mahojiano kati ya msaanii huyo na tovuti ya Darhotwire.com.Niliguswa sana na kilio cha msanii huyo ambacho kimekuwa pia kikisikika kutoka kwa takribani kila msanii wa Bongofleva.Kuna wajanja flani,(hapana,hawa si wajanja,bali ni WEZI) ambao wamekuwa wakiwanyonya vijana wetu bila hata chembe ya huruma.Wezi hawa wanafahamika zaidi kwa jina la “wadosi”.Binafsi sijui kwanini wanaitwa wadosi lakini la muhimu hawa sio jina wanaloitwa bali unyonyaji wanaowafanyia wasanii wetu.

Pengine kabla ya kujadili wizi wa mchana mweupe unaofanywa na wadosi hao,tuangalie maendeleo ya Bongofleva huko nyumbani na huku Ughaibuni.Mimi ni mfuatiliaji sana wa mambo yanayotokea huko Bongo. “Ibada” yangu ya kila asubuhi inaanza kwa kutembelea tovuti za ki-Tanzania ili kujua yanayojiri huko.Sasa,kabla ya kuja huko mwaka jana mwishoni mwa mwaka jana nilikuwa nahisi kuwa habari kwamba Bongofleva imeikamata Tanzania kwa “kasi ya tsunami” ni porojo tu.Lakini nilipokuja nilishihudia mwenyewe jinsi gani hatimaye nyimbo zinazotengenezwa na kuimbwa na Watanzania zilivyokamata soko na mioyo ya wapenzi wa muziki.Wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu nilibahatika kushuhudia tamasha la “Piga Kura au Upigike” kwenye viwanja vya Biafra Kinondoni.Licha ya picha kadhaa nilizochukua kwa ajili ya kuwajulisha marafiki zangu hapa,nilijionea jinsi gani watu wa rika mbalimbali wanavyovutiwa na kazi za wasanii wa muziki wa kizazi kipya.Nadiriki kuamini kuwa mashabiki waliofika viwanja hivyo walikuwa wanawakilisha karibu kila kona ya jiji la Dar es Salaam.Kitu kingine nilichobaini ni kwamba jinsi gani wasanii wanavyotumika katika masuala ya muhiu kwa Taifa.

Nakumbuka niliwahi kusoma katika gazeti moja la huko nyumbani kwamba msanii Juma Nature “alimfunika” mwenyeji wake-mgombea aliyemwalika msanii huyo katika kampeni zake.Yaani watu walikuwa na kiu zaidi ya kusikia muziki wa Nature kuliko hotuba ya mheshimiwa huyo.Na pengine umati kubwa uliojitokeza kwenye mkutano huo ulifuata buridani hiyo ya bure.Yayumkinika kusema kuwa mchango wa wasanii katika kufanikisha uchaguzi,na hata kuwapatia ushindi baadhi ya wagombea,ulikuwa mkubwa.Kwa bahati mbaya,au pengine kwa makusudi,baada ya kukamilisha kazi ya kuhamasisha jamii kuhusu uchaguzi na wagombea,wasanii wetu wamerudi kulekule walikokuwa:wamesahauliwa na wanaendelea kunyonywa.

Napenda kuwafumbua macho wasanii wetu kwa kuwaambia kuwa muziki wao huku guhaibuni unauzika sana miongoni mwa watu waliotoka Afrika Mashariki.Wamuulize Banana Zorro aliyealikwa hapo London kwenye pati ya Muungano,wamuulize Mr Nice,Ray C na TID,na Profesa J ambaye nasikia amewachengua vilivyo huko Sweden na Holland.Wasanii wa nyumbani wakija huku wanababaikiwa kama vile akina Shaggy au Sean Paul wanavyobabaikiwa wakija huko nyumbani.Lakini,safari za nje sio jambo la kukurupuka tu,ni kitu kinachotaka maandalizi.Kwa mantiki hiyo si lazima kusafiri ili kunufaika na kazi za sanaa bali hata kutafuta namna ya kupenyeza muziki katika soko la kimataifa kunaweza sana kuwainua wasanii wetu.Hivi wasanii wetu wanajua kuwa CD zao huku zinauzwa hadi paundi 10 (zaidi ya shs 24,000/=)?Nimesoma kwenye internet kwamba tarehe 12/06/2006 kampuni moja iitwayo Townsend Records itatoa CD iitwayo Bongoflava (Swahili Rap from Tanzania) ambayo itauzwa paundi 10.99 (takriban shs 27,000/= kwa exchange rate za leo).Sijui kama na hawa ni wadosi au la,lakini huo ni uthibitisho kuwa Bongoflava ina soko zuri tu kuhu Ughaibuni.Na watu wanapenda kweli kazi za wasanii wa nyumbani.Niliporudi kutoka Tanzania jamaa zangu kibao walikuwa wananiulizia kama nimekuja na CD za Bongofleva.Kila mmoja anasema wanaposikia wasanii wetu wanakumbuka sana nyumbani.

Mheshimiwa Kikwete alinukuliwa akiwataka Watanzania walioko nje kuwasaidia wenzao walio nyumbani hasa katika nafasi za masomo.Ujumbe huo unaweza pia kupanuliwa na kuwahusisha wasanii wa nyumbani,kwa maana kuwa Watanzania walio nje hasa wale wenye upeo na mambo ya muziki wawasaidie wasanii wetu wa nyumbani kwa namna yoyote ile inayowezekana.Lakini ili hilo liwezekane wasanii wetu hawana budi “kuchangamka.”Wanaoitwa “wadosi” wanawanyonya na kuwaibia kwa vile wanajua dhahiri kuwa wasanii hao hawana njia mbadala.Jamani,dunia siku hizi imekuwa kama kijiji (japo ni kinadharia) na unachohitaji ni kwenda tu kwenye internet café na kuperuza kurasa za mtandao kujua wapi unaweza kupata huduma au kuuza ulichonacho kwa mtu aliye bara jingine.Hapa ndipo umuhimu wa shule (elimu) unapojidhihirisha.Lakini hata kama shule haipandi,si unaweza kumwomba rafiki yako akusaidie kutafuta soko la kazi zako za sanaa nje ya nchi?

Serikali inapaswa kuwasaidia wasanii wetu kwa kuipa meno sheria ya hatimiliki.Sambamba na hilo ni wasanii wenyewe kusimama kidete kutetea maslahi yao badala ya kuendelea kulalamika au kufikiria kuingia kwenye fani nyingine kukwepa wizi wa kazi zao.Pia wasione aibu kuomba msaada kwa wenzao walio nje.Mwisho naiomba serikali ipanue vita dhidi ya wala rushwa na majambazi na kujumuisha “wadosi” pia.

Alamsiki

KULIKONI UGHAIBUNI

Mambo yakoje huko nyumbani?Natumaini kila mmoja anawajibika kwa namna yake katika ujenzi wa Taifa.

Kuna jamaa mmoja hapa anaitwa David Cameron.Huyu ni kiongozi wa chama cha wahafidhina (Conservative Party).Nia yangu si kuzungumzia wasifu wake,bali nataka nimlinganishe na mwanasiasa nyota wa huko nyumbani kwa muda huu,au kwa lugha ya “kwa mama” tunaweza kumuita “a man of the moment.” (kwa tafsiri ya haraka, “staa wa muda huu”).Nadhani msomaji mpendwa umeshajua ni nani ninayemzungumzia.Lakini hapa namuweka kando kidogo ili nikupashe kuhusu huyo Bwana Cameron na chama chake cha Conservatives (au Torry,kama kinavyojulikana hapa).Kwa tafsiri nyepesi hawa Conservatives ni watu wenye mrengo wa kulia na ndio wapiga kelele wakubwa kuhusu sera za uhamiaji na nyinginezo ambazo zinawagusa makabwela hususan wale ambao si wazawa wa hapa.Pengine jeuri kubwa ya wahafidhina hawa inatokana na uwezo wao wa kifedha.Fedha wakati mwingine huwa na tabia ya kumfanya binadamu asiwafikirie wenzie aliowazidi kiuwezo,na aghalabu anapowafikiria basi huwa ni kwa manufaa yake binafsi.

Kuibuka kwa Cameron kulichochewa zaidi na mwelekeo usioridhisha wa chama chake katika chaguzi mbalimbali.Wachambuzi wengi wa mambo ya siasa walikuwa wanahusisha mwenendo mbaya wa chama hicho na kile kinachoitwa kuwa “out of touch.”Nitafafanua.Chama kilicho “out of touch” ni kile ambacho machoni mwa watu wa kawaida kinaonekana kama hakijihusishi na maslahi ya walio wengi.Kwa mfano,hawa wahafidhina kwa miaka kadhaa wamekuwa wakikumbatia zaidi Waingereza weupe hasa wale wa tabaka la juu na la kati huku wakiwasahau wale wa tabaka la chini pamoja na Waingereza wengine ambao ni “wakuja” (kwa mfano wale wenye asili ya Asia,Caribbean,Afrika,n.k).Pia wamekuwa wakiwaona wageni (ikiwa ni pamoja na wanafunzi wanaochangia mamilioni ya paundi kwenye uchumi wa nchi hii) kama watu wanaokuja kuharibu uchumi,utamaduni na mazingira ya hapa.

Baada ya Waziri Mkuu wa mwisho kutoka Conservative kushika wadhifa huo,John Major,alipoangushwa na Tony Blair mwaka 1997,chama hicho kimebadilisha viongozi kadhaa lakini bila mabadiliko hayo kuwanufaisha kwenye chaguzi mbalimbali.Ndipo katika mchakato huo alipoibuka Bwana Cameron,kijana (ana miaka 40 tu),ana mvuto na haiba ya kutosha.Huyo bwana aliamua kuwapa wenzake kitu “laivu” kwamba chama chao hakina mvuto kwa wapiga kura,kinaonekana kuwa kiko zaidi kwa maslahi ya mabwanyenye kuliko makabwela,na hakizungumzi “lugha ya mtu wa kawaida mtaani.”Kuna mengi ya kumzungumzia huyo bwana lakini kilichonisukuma kuandika makala hii ni jinsi navyomuona anafanana na Jakaya Kikwete.Ukiachilia ukweli kwamba wote ni handsome lugha wanayoongea inafanana:lugha inayomgusha mtu wa kawaida na sio makundi flani tu katika jamii hususan wale wenye nguvu za kiuchumi.

Jakaya amenukuliwa mara kadhaa akiwausia viongozi wenzie kwamba wako madarakani kuwahudumia hao waliowaweka madarakani.Sio dhambi kuwa karibu na matajiri lakini ukaribu huo usiwe kwa ajili ya kuwaumiza wasio nacho.Utajiri sio dhambi,na kuna matajiri kadhaa (mfano Mzee Mengi huko nyumbani au Bill Gates huko Marekani) ambao utajiri wao umekuwa faraja kwa mamilioni ya wale wasio nacho.Matajiri wa aina hii ni muhimu kwao kuwa karibu na viongozi wa serikali,vyama vya siasa na taasisi nyingine kwa vile ni kwa ukaribu huo ndio miradi mbalimbali wanayoifadhilia inaweza kuwa na manufaa kwa wananchi.

Juzijuzi nilimwona Bwana Cameron kwenye luninga akiwa kwenye mtaani wakati wa kampeni za chama chake kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa kwa upande wa England.Jinsi alivyokuwa akijichanganya na watu ilitosha kabisa kumfanya hata mtu aliyekuwa akikichukia chama cha wahafidhina afikirie upya.Siku chache baadae nikasoma kwenye mtandao kuwa Jakaya ameweka historia kuwa Rais wa kwanza wa Tanzania kutembelea wafungwa magerezani.Yalipotokea mauaji ya kutatanisha ya wale wachimba madini wa Mahenge hakukawia kuunda tume,na kinyume ya ilivyozoeleka mara baada ya kupewa ripoti na tume akaweka matokeo hadharani.Aliporejea tu kutoka Kusini mwa Afrika hakukawia kwenda kuwaona majeruhi wa tukio la uporaji wa fedha za NMB pale Ubungo,na kutoa maagizo papo hapo.Lakini si Jakaya pekee bali hata “luteni” wake Lowassa.Ghorofa lilipoanguka Keko hakusubiri kuletewa taarifa bali alikwenda kujionea mwenyewe na kuchukua hatua hapohapo, “mafuriko” yalipoielemea Sinza hakukawia kwenda kushuhudia hali ilivyo na kuwaamuru wahusika wachukue hatua za haraka.

Laiti kasi mpya,ari mpya na nguvu mpya aliyokuja nayo Kikwete itaweza kufikia hatua ya kuigwa na viongozi kuanzia ngazi ya serikali ya mtaa,kata,tarafa,wilaya na mkoa,basi muda si mrefu Bongo itakuwa sehemu ya neema.Na mwenyewe Jakaya amekuwa akisema kuwa Tanzania yenye neema inawezekana.Enyi viongozi mliolala hebu amkeni,msisubiri kuamshwa.Jisikieni aibu pale mnapokwenda kinyume na spidi ya kiongozi wenu mkuu.

Alamsiki

KULIKONI UGHAIBUNI

Asalam aleykum,

Siku za nyuma niliahidi kwamba iko siku nitawaletea stori kuhusu “mateja” wa huku Ughaibuni.Ndio,tatizo la matumizi ya madawa ya kulevya linawaumiza vichwa watu kadhaa huku Ughaibuni.Kuna vijana wadogo kabisa ambao wanashawishika kujiingiza katika kubwia unga.Ni vigumu kutabiri mafanikio ya jitihada za serikali na taasisi mbalimbali katika mapambano yao dhidi ya ulevi huo haramu na hatari.

Hivi karibuni nilipewa habari za kusikitisha sana.Kijana mmoja mwenye umri usiozidi miaka 18 alikutwa amekufa huku sindano aliyoitumia kujidungia adawa ya ulevya ikiwa inaning’inia kwenye mkono wake.Huyo kijana namfahamu vizuri kwa vile siku moja aliwahi kufika hapa ninapoishi akiwa ameongozana na rafiki yangu mmoja mwenye asili ya Afrika Mashariki.Kilichonivutia zaidi kuhusu kijana huyo ni kauli zake ambazo lazima nikiri kuwa mara nyingi kwa hapa zinatolewa na wanasiasa kuliko wananchi wa kawaida.Alikuwa akionyesha kuchukizwa kwake na watu wanaowabagua wenzao kwa vile tu ni wageni au wana rangi tofauti na wao.Kimsingi,alikuwa akilaani suala zima la ubaguzi.Kwa umri wake mdogo,nilimwona kama ni mtu mwenye upeo mkubwa sana.Kwa wakati huo sikujua kabisa kuwa pamoja na busara zake,kijana huyo alikuwa akiweka rehani roho yake kwa kubwia unga.Pengine lishe bora na huduma mbalimbali zinazopatikana kirahisi ndizo zilikuwa zinamsaidia kuficha “uteja” wake,kwani kama tujuavyo wengi si vigumu kumtambua m-bwia unga kwa kumwangalia tu.

Alienisimulia kuhusu mauti yaliyomkumba kijana huyo alinijulisha kwamba aliemletea marehemu madawa hayo ya kulevya alikuwa ni rafiki yake ambae walikuwa wanasoma darasa moja.Kwa lugha nyingine,wawili hao walishirikiana katika kuleta mauti ya mmoja wao.Huo ni ushirika wa mauti,na hilo ndio linanipeleka kwenye mada yangu ya pili kuhusu ujambazi uliotokea hivi karibuni pale Ubungo uliopelekea vifo na majeraha kwa waliosalimika.

Kuonyesha yeye ni kiongozi anaewajali mno wananchi wake,matra baada ya kurejea nchini akitoka ziarani kusini mwa Afrika,Rais Jakaya Kikwete alikwenda kuwajulia hali waliojeruhiwa na majambazi katika tukio hilo la Ubungo.Mheshimiwa Kikwete alinukuliwa na vyombo vya habari akisema kwamba anaamini kuwa kulikuwa na njama ndani ya benki iliyoibiwa fedha hizo kwa vile isingekuwa rahisi kwa majambazi hayo kuvamia tu gari lenye fedha bila kuwa na taarifa sahihi.Wafanyakazi waliohusika kuvujisha taarifa za fedha hizo kwa majambazi watakuwa hawana tofauti na yule kijana aliempelekea unga rafiki yake na hatimaye kumsababisha mauti.Waliovujisha taarifa hizo walikuwa na ushirika wa mauti na majambazi waliofanya unyama huo.Hivi tunapokuwa kazini si huwa tunaunda kitu kama undugu kwa vile muda mwingi tunautumia tukiwa pamoja na pengine kushirikiana katika mambo ya nyumbani kama vile harusi na misiba?Sasa unapotoa taarifa kwa majambazi wenye silaha za moto ili kuwawezesha kuvamia gari ambalo mfanyakazi mwenzio yupo humo si ni kama unamtengenezea mauti mwenzio?Jamani,hivi fedha zinatupeleka kupoteza utu wetu na kutothamini uhai wa wenzetu!Kwa hakika walioshiriki kwa namna yoyote katika kufanikisha uporaji huo wanastahili kusakwa kwa udi na uvumba na hatimaye kupatiwa kibano wanachostahili.Kwa “waliouza ishu” hiyo kwa majambazi wanakuwa wametenda dhambi kuu mbili:kuwasaliti wafanyakazi wenzao ambao aidha waliuawa au kujeruhiwa,na pia walishiriki katika ujambazi huo kwa vile wao ndio hasa waanzilishi wa mpango mzima.Hiyo si kusema kwamba majambazi waliohusika hawana hatia,lakini iwapo waliotoa taarifa hizo wasingewajulisha majambazi kwamba siku flani,muda flani,katika gari flani kutakuwa na shilingi bilioni moja ni dhahiri kwamba tukio hilo lisingetokea.

Kwa upande mwingine,ni muhimu kwa taasisi zetu za fedha kuwa makini zaidi wanaposafirisha fedha kutoka sehemu moja kwenda nyingine.Hivi kweli benki kama NMB inashindwa kununua gari moja ambalo ni maalumu kwa ajili ya kusafirishia fedha?Uzuri wa magari kama hayo ni kwamba licha ya kutoa usalama mkubwa kwa mali inayosafirishwa,maisha ya wanaosafirisha mali hiyo nayo yanakuwa salama zaidi ukilinganisha na magari ya kawaida.Natambua kuwa yapo makampuni binafsi ya ulinzi ambayo yanamiliki magari ya aina hiyo.Lakini siwezi kuilaumu NMB moja kwa moja kwa kutokodi huduma hiyo kwa vile kumbukumbu zinaonyesha kuwa siku za nyuma walinzi wasio waadilifu walishawahi kuingia mitini na mamilioni ya fedha wakiwa katika gari maalumu la kusafirishia fedha.

Hata hivyo,kuwa na gari maalumu la kusafirishia fedha bila kuwa na watumishi waadilifu ni sawa na kulala ukiwa kwenye chandarua chenye dawa lakini kimekufunika kuanzia kichwani hadi kiunoni tu,na hapohapo kuamini kuwa unawadhibiti mbu.Uaminifu,uadilifu na kuthamini maisha ya wenzetu ni vitu muhimu sana na lazima kwa kila Mtanzania.

Alamsiki

KULIKONI UGHAIBUNI:

Mambo?

Siku chache zilizopita nilibahatika kuwa na maongezi na babu mmoja wa Kiskotishi ambaye kwa maelezo yake mwenyewe yeye ni “mkazi wa dunia nzima” (global citizen).Babu huyo anadai kuwa dunia ingekuwa mahala bora sana kama kusingekuwa na mipaka na sheria kali za uhamiaji.Na katika kutimiza azma yake ya kuwa mkazi wa dunia nzima anadai ametembelea takribani nchi 10 katika kila bara.Sijui kama alikuwa anasema ukweli au “ananifunga kamba” tu.Katika maongezi yetu hayo aligusia jambo flani ambalo liliniingia sana na ambalo ndio mada yangu ya wiki hii:UZALENDO.

Kwa mujibu wa babu huyo,enzi zao wakiwa vijana suala la uzalendo lilikuwa likitiliwa mkazo sana.Alidai kuwa japo kwa sasa hali ni tofauti kidogo lakini bado nchi nyingi za magharibi zinatilia mkazo sana suala hilo.Alieleza kwamba akiwa kijana babu yake alikuwa akimwambia kuwa mazingira mazuri watakayoyaweka wakati huo yatakuja kuvinufaisha zaidi vizazi vijavyo.Baba yake pia alikuwa akimweleza hivyo hivyo.Na yeye alipokuwa mtu mzima alikuwa akiwaeleza wanae hivyohivyo.Na sasa anasema amekuwa akitoa changamoto ya aina hiyohiyo kwa wajukuu wake.Furaha aliyonayo ni kwamba utabiri wa babu na baba yake umetimia.Maendeleo yaliyopo hivi sasa yamechangiwa na msingi mzuri uliojengwa karne kadhaa zilizopita.Na kilichowasukuma hao waliotengeneza misingi hiyo si kingine zaidi ya uchungu wao kwa taifa lao na vizazi vijavyo.

Huko nyumbani kuna tatizo kuhusiana na suala la uzalendo.Wapo wapuuzi fulani ambao wanaendesha mambo utadhani hakuna kesho au labda Tanzania haitakuwepo miaka 50 ijayo.Na hawa ndio baadhi yao waliripotiwa kutishia maisha ya waandishi wa KULIKONI na THIS DAY kwa sababu magazeti hayo yameapa “kula nao sahani moja” (kuwaweka hadharani).Hawa ni watu ambao hawana uchungu si kwa nchi yao tu bali hata kwa wajukuu zao.Ukweli ni kwamba mtu anayekula fedha iliyotolewa kwa ajili ya ujenzi wa shule hana upeo wa kufikiria kwamba kwa kufanya hivyo huenda wajukuu wa mtoto wake wa mwisho watakaopaswa kwenda shule miaka 20 ijayo wanaweza kukosa nafasi hiyo kwa upuuzi uliofanyika mwaka 2006.Kuna watu wanafanya mchezo na maisha ya Watanzania wenzao kwa kutumia fedha za wenzao bila hata kuwashirikisha hao waliowekeza.Jamani,hata sheria za kawaida mtaani si kwamba bwana au bibi harusi mtarajiwa hawezi kutumia michango ya harusi yake mwenyewe pasipo kuwajulisha wanakamati?Sembuse hao ambao wamekabidhiwa fedha ambazo baadae wanapaswa kuzirejesha kwa wahusika!Nadhani mnaniapata hapo.

Wabadhirifu wa mali za umma na wala rushwa ni sawa na majambazi tu.Ni majambazi ambao silaha yao kubwa ni dhamana walizokabidhiwa kuwatumikia wananchi.Majambazi hawa wanachoiba sio fedha tu bali hata haki za Watanzania wenzao.Na kama walivyo majambazi wengine,hawa wakishahisi kuwa wanafahamika hukimbilia kutumia silaha kuu mbili:rushwa na vitisho.Kama gazeti linachimba maovu yanayofanywa na watu flani wasio na uchungu na nchi yao,basi waandishi wa gazeti hilo watafuatwa ili “wadakishwe kitu kidogo kuua soo.”Na itapoonekana kuwa gazeti hilo na waandishi wake wako ngangari katika kutetea maslahi ya Taifa na hivyo kukataa kuuza taaluma yao kwa kupokea rushwa basi hapo ndipo vitakapoanza vitisho.Sio huko nyumbani pekee ambako waandishi wa habari wanaovalia njuga kufichua maovu katika jamii wanakumbana na vitisho kutoka kwa wahusika.Mwaka 1996,Veronica Guerin, mwandishi wa habari wa kike huko Northern Ireland alipigwa risasi na kuuawa kutokana na makala za uchunguzi kuhusu biashara ya madawa ya kulevya nchini humo.Mwaka juzi,waandishi kadhaa wa magazeti ya Daily Record na Sunday Mail ya hapa Uingereza waliripoti kupokea vitisho kutokana na habari za uchunguzi walizokuwa wakiandika kuhusiana na magenge ya uhalifu.Kadhalika,mwaka jana waandishi wa habari wa magazeti kadhaa nchini Italia waliripoti kupokea vitisho baada ya kuripoti tuhuma za rushwa kuhusiana na klabu ya soka ya Genoa ya nchini humo.

Mifano hiyo michache inaonyesha ni jinsi gani watu waovu wanavyopenda kuendelea na maovu yao bila kubughudhiwa.Lakini haiwezekani watu wenye uchungu na nchi yetu wawaachie kufanya ufisadi wao wapendavyo.Naamini kila mzalendo anaelitakia mema Taifa letu atahakikisha kuwa wanahabari wanaosimama kidete kuwafichua wala rushwa na wabadhirifu hawabughudhiwi hata kidogo.Mjenga nchi ni mwananchi na mvunja nchi ni mwanachi pia.Tukiendelea kuwalea hawa majambazi wa mali na haki zetu basi tujue kuwa sio tu tunajitengezea “future” mbaya bali pia vizazi vijavyo vitatuhukumu kwa kuwaachia watu wachache wasio na uchungu na nchi yetu kutuharibia mambo.Tukiamua kwa nia moja tunaweza kuwadhibiti majambazi hao.

Alamsiki.

KULIKONI UGHAIBUNI:

Asalam aleykum,

Leo tuzungumize michezo,hususan soka.Kwa takriban wiki nzima sasa habari ya soka iliyotawala katika vyombo vya habari vya hapa Uingereza ni kuhusu suala la mchezaji mahiri wa klabu ya Manchester United na timu ya Taifa,Wayne Rooney.Ishu yenyewe ni kwamba ilidaiwa kuwa Rooney alikuwa na madeni yanayofikia pauni 700,000 (takribani shilingi milioni 140 za huko nyumbani) aliyokuwa akidaiwa na makampuni ya kamari (betting).Inasemekana tayari amemalizana na wadai wake.Wapo waliomlaumu mchezaji huyo kwa kutumia vibaya fedha zake,lakini wengine wamemtetea kwamba haikuwa ubaya kutumia kipato chake kinachotokana na ajira yake.

Ndio,soka huku Ughaibuni na hata katika baadhi ya nchi za huko Afrika ni ajira.Ni ajira ambayo inamwezesha mtu kama Rooney kutumbukiza zaidi ya shilingi milioni 100 kwenye kamari.Pointi yangu sio uhusiano wa soka na kamari bali soka kama ajira.Tukirudi huko nyumbani,siku chache zilizopita klabu kongwe za Simba na Yanga zilichimba mkwara kuwa zingesusia ligi kuu ya Bara iwapo mgao wa mapato ungeendelea kuwanufaisha zaidi wengine badala ya wao wanaovuja jasho dakika 90.Binafsi niliguswa sana na hoja za klabu hizo japokuwa kwa bahati mbaya nasikia wakongwe hao wamenywea katika kutimiza azma yao ya kutaka “kieleweke.”Sijui kuufyata huko ni kwa vile viongozi wa klabu hizo walitoa hoja hiyo kama kutingisha kiberiti,au sijui ni ubabe wa vyama vyetu vya michezo huko nyumbani!Lakini naamini klabu hizo zilikuwa na hoja ya msingi kabisa.

Pambano lao la mwisho liliingiza milioni 98 kama sijakosea.Lakini kila klabu ikaambulia shilingi milioni 23.6 tu.Kwa kweli huo ni sawa na uonevu.Mapato hayo yalitokana na umaarufu wa klabu hizo,hivyo zenyewe ndio zilipaswa kunufaika zaidi na mapato hayo.Nadhani klabu hizo zilistahili kupata kiwango kikubwa zaidi ya hicho hasa ikizingatiwa kuwa timu hizo kwa sasa ni kama za kulipwa kutokana na kuwa na wachezaji kadhaa wa kigeni ambao mishahara yao ni ya juu.Jitihada za kuzigeuza klabu hizo kuwa kampuni zimekuwa zikikwama mara kwa mara.Kwa hiyo tofauti na klabu kubwa za huku Ughaibuni ambazo zinaendeshwa kwa mfumo wa kampuni hivyo kutotegemea sana mapato ya uwanjani,chanzo kikuu cha mapato kwa vilabu vyetu vya nyumbani ni mapato yanayotokana na watu wanaoingia uwanjani kushuhudia mechi zao.

Imenisikitisha sana kuona hoja ya klabu hizo imekufa kienyeji.Lakini sikushangaa sana kwa vile sio siri kwamba vilabu vyetu huko nyumbani vinaendeshwa kwa ubabaishaji sana.Kwanza kwa Simba na Yanga hawapaswi kutegemea mapato ya uwanjani kama chanzo pekee cha mapato.Japo hoja ya klabu hizo kugeuzwa kuwa kampuni bado ni ya muhimu sana ingawaje wenyewe wanapuuzia,vipo vyanzo vingine kadhaa vya mapato ambavyo vimetelekezwa.Kwa mfano,kwa kutengeneza kalenda 100,000 zenye picha za wachezaji ambazo zingekuwa katika ubora unaostahili na kuziuza angalau kwa shilingi 500 kila moja,klabu ingejiingizia shilingi milioni 50.Hilo linawezekana kabisa hasa kwa vile gharama za utengenezaji wa kalenda sio kubwa sana na kuna uwezekano wa kupatikana wadhamini wa kugharamia mradi wa aina hiyo.
Kwa mtizamo wangu,watu wanaopaswa kubeba lawama zaidi katika suala zima la ubabaishaji kwenye vilabu vyetu ni hao wanaoitwa wanachama.Hao ndio wanaochagua viongozi wabovu,na ni haohao ambao hawakawii kwenda mahakamani kupinga uongozi ambao wao wenyewe waliuweka madarakani.Wanang’ang’ania kujiita wanachama wakati mchango wao mkubwa katika kuendesha klabu hizo ni kwenda kwenye vyombo vya habari kutaka uongozi wa klabu ujiuzulu,au kocha hafai au wakati mwingine kusema lolote tu ili wasikike hewani.Kama kweli wanachama wa Simba na Yanga wangekuwa wenye mwamko unaostahili basi naamini wangetumia nguvu za wingi wao kuhakikisha hoja zilizotolewa na viongozi wao kuetetea maslahi ya klabu hizo zinashinda.Badala ya hoja hizo kuonekana ni ajenda binafsi za Wambura au Kifukwe zingekuwa ni hoja za klabu na wanachama wa Simba na Yanga.

Kulalamika bila kutoa ufumbuzi wa tatizo ni sawa na kulikuza tatizo.Kwa hiyo,nawajibika kutoa mchango wangu katika kupata ufumbuzi.Nadhani Tenga na wenzie wa TFF wanapaswa kuliangalia upya suala la mgao wa mapato kwa klabu,na sio kwa Simba na Yanga pekee bali vilabu vyote.Vilabu vina haki ya kudai ziada ya wanachokipata kutokana na jitihada zo uwanjani.Kuhusu uendeshaji wa vilabu,Serikali inapaswa kuingilia kati kwa kutengeneza sera ambayo haitotota fursa ya uababishaji,iwe wa viongozi au wanachama.

Alamsiki.

KULIKONI UGHAIBUNI

Habarini za huko nyumbani.Hapa shwari.

Mada yangu ya leo najua dhahiri itawakera wateule wachache wa aina flani.Lakini kabla ya kuwapa somo ngoja tuongelee suala la imani na dini hapa napoishi.Nilipofika hapa kwa mara ya kwanza nilionyeshwa majengo kadhaa ambayo hapo awali yalikuwa makanisa lakini sasa yamegeuzwa kuwa kumbi za disko na klabu za usiku.Na hao walioyageuza makanisa hayo kuwa sehemu za starehe wala hawakujishughulisha kubadili mwonekano wake bali wameyaacha yatoe ushuhuda kuwa huko nyuma yalikuwa sehemu za ibada.Nilipofanya udadisi kwa wenyeji niliambiwa kuwa makanisa hayo yaliuzwa baada ya kuwa matupu kutokana na ukosefu wa waumini.Wengi wa waumini wa makanisa ya mji huu naoishi ni aidha wageni (waliotoka nje ya nchi hii kama mimi) au vikongwe.Na si ajabu kukuta kanisa lenye uwezo wa kuchukua watu 500 likiwa na waumini 50 tu.

Binafsi sina majibu ya moja kwa moja kuwa tatizo la hawa wenzetu ni nini.Ila nachofahamu ni kwamba kuna watu kadhaa ambao wanajitambulisha kuwa hawana dini,au hawaamini kuwa kuna Mungu.Pengine labda kwa vile wengine wamezaliwa na kukuta maisha ni mteremko basi hawaoni umuhimu wa kuamini kuwa kuna Mungu.Hata hivyo,imani ni suala la mtu binafsi hivyo pengine si mwafaka kuhoji kwa nini flani anaamini au haamini kuwepo au kutokuwepo kwa Mungu.Japo mie ni muumini wa aina flani huwa sisiti kuwasifu wale wasio waumini lakini hawaoni aibu kuelezea msimamo wao wa kidini.Kwa lugha nyingine watu hao sio wanafiki,wanaelezea bayana kile wanachokiamini au kutokiamini.

Kuna tatizo la msingi huko nyumbani japokuwa natambua dhahiri kwamba watu wengi hawapendi kujadili mambo ya dini.Tatizo hilo ni UNAFIKI.Hivi ndugu zanguni,kama imani unayoifuata na kujidai nayo inakukataza kuvuta sigara si bora usivute tu kuliko kuwachanganya watu?Baadhi ya viongozi wetu wa dini wamekuwa mstari wa mbele sana kuwakemea wale ambao wanakwenda kinyume na imani zao,lakini wakati huohuo viongozi hao wanashirki kwenye maovu wanayoyakemea.Ndio tunatambua kuwa mara nyingi viongozi wetu wa dini wana wafadhili wao nje ya nchi,lakini hicho sio kigezo cha wao kuishi maisha tofauti kabisa na wafuasi wao.Utakuta katika kijiji flani ambacho kimegubikwa kabisa na umasikini,kiongozi flani wa dini anaishi kama yuko peponi vile.Na bila huruma,huku akitumia kisingizio cha maandiko matakatifu,anawashurutisha waumini wake kujipigapiga kuongeza sadaka wanazotoa.Pengine ni ule msemo kuwa alie nacho atazidi kuongezewa na yule asie nacho atanyang’anywa hata kile kidogo alichonacho.

Kinachokera zaidi ni hili ni suala la baadhi ya viongozi wa madhehebu flani kuwa na watoto mtaani huku sheria za madhehebu yao haziwaruhusu kufanya hivyo.Hivi unapomzalisha mwanamke ambae huwezi kumuoa kwa vile majukumu uliyonayo yanakukataza kufanya hivyo si ni sawa tu na kumharibia maisha huyo mwanamke uliezaa nae.Tatizo hili ni sugu sana hususan maeneo ya vijijini.Kinachosikitisha ni ukweli kwamba waumini wanafahamu kuwa kiongozi flani wa dini anaishi kinyume na maadili lakini hawachukui hatua yoyote zaidi ya kulalamika chinichini.Mimi binafsi nina mifano hai ya baadhi ya viongozi wa madhehebu yangu ambao wana watoto lukuki mitaani.Baadhi yao wanatoa huduma kwa wazazi wa watoto hao lakini wengine wamewatelekeza tu.Hawa watu ni wanafiki ambao hawastahili kuachwa wanaendeleza uhuni kwa kisngizio kuwa daraja walilofikia haliwezi kutenguliwa.Mitume wetu waliishi maisha ya uadilifu ambayo yalishabihiana kwa asilimia mia moja na kile walichokuwa wakikihubiri.Na sio kwenye uzinzi tu,bali hata kwenye dili za kibiashara.Wapo wanaopokea kitu kidogo ili,kwa mfano,mtu akiagiza gari lake kutoka nje apunguziwe ushuru kwa vile linaonekana limeagizwa na taasisi ya kidini.Huu ni ukwepaji wa kodi ambao joho la utumishi wa Mungu halipaswi kuwa ngao ya kuzuia mhusika kuchukuliwa hatua za kisheria.

Hivi majanga kama ukimwi yataondoka vipi iwapo baadhi ya wale wanaopaswa kukemea vitendo vya ngono kwa vile vinavunja amri ya Mungu nao ni washiriki wa vitendo hivyo?Ndio,maandiko yanataka tufuate yale yanayosemwa na sio matendo ya msemaji lakini katika hali halisi mzazi anayeendekeza ulabu hawezi kueleweka pale anapomkemea mwanae anaefuata mkumbo wake.

Tafadhalini jamani,naomba mhubiri kile mnachokiamini na kukifuata ili kuwasaidia kuwafikisha peponi hao naowahubiria.Na hilo si ndio jukumu lenu?

Alamsiki

KULIKONI UGHAIBUNI

Asalam aleykum wasomaji wapendwa wa makala hii.

Leo nina hasira.Muda mfupi kabla ya kuandika makala hii niliongea na mzazi wangu huko Ifakara.Akanisimulia stori mmoja ambayo kimsingi ndio iliyonifanya niwe na hasira.Hata hivyo,naomba niwatoe hofu kwamba hasira nilizonazo haziwezi kupoteza ladha ya makala hii.

Mzee ana matatizo ya moyo.Sasa kama unavyojua mambo ya miji midogo kama Ifakara.Hospitali zipo lakini wataalamu ni wachache.Lakini kwa kumbukumbu zangu wakati flani aliwahi kunieleza kwamba kuna daktari mmoja mwenye zahanati yake binafsi mjini hapo ambae inaaminika kuwa ni mtaalam wa mambo ya moyo.Katika maongezi yetu kwenye simu aliniambia kuwa moyo bado unamsumbua.Nikamuuliza kwanini asiende kwa huyo mtaalam wa magonjwa ya moyo.Jibu alilonipa ndilo lililonifanya nipandwe na hasira niliyonayo hadi sasa.Anasema kwamba jirani yake aliyekuwa akisumbuliwa na matizo ya moyo alikwenda kumuona huyo daktari hivi karibuni,lakini jibu alilopewa lilimfanya mgonjwa huyo kurudi nyumbani akiwa na ugonjwa mwingine mpya:hofu ya kufa.Kisa?Aliambiwa na mtaalamu huyo wa moyo kwamba hivi “kwanini wewe ambaye umebakiwa na wiki mbili tu za kuishi (kutokana na umri wako mkubwa) unataka kutibiwa moyo badala ya kuuacha usimame wenyewe muda ukifika”!

Laiti maelezo hayo ya mzazi wangu yangekuwa yanatoka kwa mtu wa kawaida tu nisingeamini kwamba nchi yetu ina baadhi ya watu wanaojiita madaktari ambao wanaweza kukiuka maadili ya kazi yao kwa kiwango hicho!Nadhani hata ukienda gereji na gari lililochoka sana,bado mafundi makenika watakupa matumaini ya namna flani badala ya kukibilia kukwambia kwamba ukalitupe gari lako.Na hapo tunazungumzia kitu ambacho unaweza kukinunua kipya.Maisha hayawezi kununuliwa upya.Tukirudi kwenye stori niliyopewa na mzee,basi jirani yake (ambaye si kama amekula chumvi sana) tangu alipoambiwa na daktari kwamba amebakiwa na wiki mbili kufa,amepatwa na hofu ya ajabu.Kwani kuna mtu ambaye haogopi kufa?Na hasa kama umepewa tahadhari kama hiyo na daktari.Mzee wangu baada ya kusikia stori hizo kutoka kwa jirani yake alinieleza bayana kwamba bora aendelee kuugua kuliko kwenda kwa daktari ambae amegeuka kuwa mtabiri wa urefu wa maisha ya wagonjwa.Nilimpoza kwa kumwambia kuwa naamini huyo daktari alieongea upuuzi huo hajui wajibu wake na anakiuka tu maadili ya kazi yake.

Laiti jirani ya mzee wangu angekuwa amekumbana na kioja hicho hapa Ughaibuni huenda angejikuta anapata utajiri wa ghafla endapo angefungua mashtaka dhidi ya daktari aliemtishia uhai wake.Sio siri,hawa wenzetu wanatoa kipaumbele kikubwa sana kwa suala la afya sambamba na kuhakikisha kuwa watumishi katika sekta ya afya wanatekeleza majukumu yao kwa kufuata maadili.Na sio katika sekta ya afya pekee bali sehemu nyingi zinazotoa huduma za moja kwa moja kwa wananchi zinabanwa sana kuhakikisha kuwa huduma hizo zinatolewa katika kiwango stahili.Pengine kingine kinachowasaidia viongozi katika taasisi mbalimbali za huduma hapa Ughaibuni ni ile tabia ya kufuatilia nini kinachoongelewa kuhusu huduma zinazotolewa na taasisi zao.Mganga mkuu akisoma gazeti na kukuta malalamiko kuhusu hospitali yake,hapuuzi bali atakimbilia kumjibu mlalamikaji huyo kuwa atachunguza suala lililolalamikiwa.Na haishii kutoa ahadi tu bali hatua lazima zitachukuliwa.Lakini kinachosikitisha huko nyumbani ni ile kuona gazeti flani limeripoti kuwa hospitali flani “imeua” mgonjwa na wala husikii habari hiyo ikikanushwa au kukubaliwa na uongozi wa hospitali husika.

Sehemu nyingi zinazotoa huduma huko nyumbani zina masanduku ya kutoa maoni.Lakini lile vumbi unaloliona kwenye mengi ya masanduku hayo linatosha kuthibitisha kuwa masanduku hayo ni sawa na urembo tu kwenye makorido ya sehemu husika.Kwa mtizamo wangu,nadhani tatizo la msingi ni ile tabia iliyojengeka kwa baadhi ya watumishi kwenda kazini kuonekana tu wamekwenda kazini na mwisho wa mwezi wapate mishahara yao,na si kwenda kutumikia wale wanaowafanya wapate mshahara.Unadhani mtumishi wa benki anaejua dhahiri kwamba ni fedha za wateja ndio zinaiwezesha benki hiyo kuwepo na kumlipa mshahara,atamdharau mteja anaekuja hapo kupata huduma?Kama mtumishi anajiona hataki “kubughudhiwa” na wanaohitaji huduma kazini kwake,si alale tu nyumbani,au aache kazi?Tuone kama hatakufa kwa njaa.Kumbe basi kinachompa shibe (kazi) ni sharti akiheshimu na kukitumikia kwa moyo wake wote.

Alamsiki

Categories

Unordered List

Sample Text

Blog Archive

Labels

Follow Us on FaceBook

Popular Posts

Recent Posts

Recent Comments

Recent Premium Themes

Your Links

Flickr

Powered by Blogger.

Blog Archive

Followers

Download

Your Links

Blogger Tricks

Popular Posts

Recent Posts

Text Widget