Showing posts with label SIMBA SPORTS CLUB. Show all posts
Showing posts with label SIMBA SPORTS CLUB. Show all posts

Wednesday, 17 August 2011


Sosthenes Nyoni
SIMBA, Simba ndio ulikuwa wimbo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam baada vijana hao wa mtaa wa Msimbazi kulipinza kisasi kwa ukifunga Yanga mabao 2-0 kwenye mchezo wa Ngao ya Jamii.

Simba waliofungwa kwenye Kombe la Kagame na Ngao ya Jamii mwaka jana vijana hao wa Mganda Moses Basena walizinduka na kupata mabao ya mapema kupitia kiungo Haruna Moshi 'Boban' dakika 15 na penalti ya Felix Sunzu dakika 38.

Simba iliyoanza kwa kasi mchezo huo ilifanikiwa kupata bao la kuongoza kupitia kwa Moshi 'Boban' aliyemalizia vizuri krosi ya kutoka upande wa kushoto iliyopigwa na mshambuliaji wa kimataifa wa Sunzu aliyekuwa na ushirikiano mkubwa na Emmanuel Okwi.

Mshambuliaji Sunzu alifungia Simba bao la pili kwa mkwaju wa penalti baada ya Nadir Haroub kumchezea vibaya Moshi 'Boban', kwenye eneo la hatari dakika 35. Sunzu alilazimika kuonyesha ueledi wake pale alipotakiwa kurudia penalti hiyo baada ya mwamuzi Israel Mjuni kusema Kado alitokea kabla ya kupigwa kwa penalti ya kwanza pamoja na kuwa alikuwa amefunga.

Kocha Moses Basena aliyeonekana kujifunza kwa makosa alitumia mfumo wa 4:2:3:1 na kutoa nafasi kubwa kwa Okwi, Haruna na Sunzu kutawala sehemu kubwa ya kiungo tofauti na ilivyokuwa kwenye fainali ya Kombe la Kagame.

Okwi alifanya atakalo mbele ya mabeki wa Yanga walionekana kuwa kama watu waliozidiwa na mazoezi na kukosa unyumbulifu mchezoni, huku safu ya ulinzi wa Simba chini ya mkongwe Victor Costa aliweza kuwapoteza mchezoni kabisa mshambuliaji Keneth Asamoah na Jerry Tegete.

Kiungo Haruna Niyonzima alijitahidi kuonyesha uwezo mkubwa wa kutawala mpira na kujaribu kutafuta goli kwenye mechi yake ya kwanza ya watani wa jadi, lakini alikosa msahada kutoka kwa wenzake.

Simba ilianza mashambulizi kwa kasi na dakika kwanza Okwi alikosa bao baada ya shuti lake kumgonga Haroub na kupaa juu ya goli.

Okwi alipoteza nafasi nyingine dakika 8 baada ya kuwalamba chenga mabeki wa Yanga, lakini aliugonga mpira mbele zaidi na kipa Shaaban Kado akauwahi.

Beki wa Yanga, Chacha Marwa, nahodha Shadrack Nsajigwa alipewa kadi ya njano kwa kumchezea vibaya Okwi. Naye Juma Nyoso wa Simba alipewa kadi ya njano kwa kumchezea vibaya Asamoah.

Haruna Niyonzima alipiga shuti la umbali wa mita 25 baada ya kumchungulia Juma Kaseja kwa bahati mpira huo ulipaa juu ya goli.

Kipindi cha pili Yanga iliamka baada ya kuingia Hamisi Kiiza na Rashid Gumbo lakini walishindwa kuipenya ngome ya Simba.

Yanga waliendeleza sera yao ya kugomea jezi za wadhamini wa ligi Vodacom zenye nembo nyekundu kwa kuvaaa jezi za mdhamini wao TBL tofauti na Simba wenyewe walivaa zile walizopewa na Vodacom

Vikosi Yanga; Shaaban Kado, Shadrack Nsajigwa, Oscar Joshua, Nadir Haroub, Chacha Marwa, Juma Seif, Godfey Taita, Haruna Niyonzima, Keneth Asamoah/ Gumbo, Jerry Tegete, Kigi Makasi/ Kiiza.

Simba: Juma Kaseja, Said Nasoro, Amir Maftah, Juma Nyoso, Victor Costa, Partick Mafisango, Salum Machaku/ Kiemba, Jerry Santo, Felix Sunzu, Haruna Moshi/ Gervais Kago, Emmanuel Okwi/ Kapombe.

CHANZO: Mwananchi

Sunday, 15 May 2011


Wakati wenzetu mnasherehekea timu "zenu" kama Manchester United kuchukua ubingwa,akina sie bado tupo na Simba na Yanga zetu licha ya ubabaishaji wao wa hali ya juu.Kanuni nyepesi ya kumudu kuzipenda klabu hizi kongwe za Tanzania ni kuweka hisia mbele ya busara/akili (putting emotions in front of common sense).

Kwa bahati ya mtende,wana Msimbazi tumepata fursa ambayo laiti tukiitumia vema basi tutapiga hatua kubwa ya kushiriki Ligi ya Mabingwa.Kwa sasa sitaki hata kufikiria itakuwaje kwenye Ligi hiyo,iwapo tutafanikiwa,maana timu zilizopo huko ni hatari.Anyway,kwa muda huu ngoja tushangilie habari hizi njema (hata kama ni ushindi wa mezani)

Simba yawang’oa Mazembe Afrika
• Sasa kuwavaa Wamorocco jijini Khartoum

na Mwandishi wetu, CAIRO, Misri


WEKUNDU wa Msimbazi, Simba ya jijini Dar es Salaam, imeshinda rufaa yake iliyokata dhidi ya mabingwa mara mbili mfululizo wa Ligi ya Mabingwa Afrika 2009 na 2010, TP Mazembe ya DR Congo.

Sasa TP Mazembe imeondoshwa kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa kwa kosa la kumchezesha mchezaji batili.

Huo ni uamuzi wa Kamati ya Mashindano ya Shirikisho la Soka (CAF), baada ya kupitia rufaa iliyokuwa imewasilishwa na Simba, kupinga TP Mazembe kumchezesha Janvier Besala Bokungu.

Bokungu (22), beki aliyezaliwa Kinshasa, akiwa mchezaji wa TP Mazembe mwaka 2007, alihamia Esperance ya Tunisia kabla ya kurejea mwaka huu.

Kwa mujibu wa CAF, Kamati ya Mashindano iliamua kushughulikia suala la nyota huyo baada ya Simba kuwasilisha pingamizi kwamba amechezeshwa isivyo halali.

Kamati hiyo imebaini kuwa kwa TP Mazembe kumchezesha Bokungu, ilifanya kosa kwa mujibu wa kifungu namba VIII kinachohusiana na ulaghai. Aidha, kifungu kingine kilichoipa Simba ushindi ni ibara ya 24 na 26 inayohusu uhalali wa mchezaji na ibara ya 29 ya kanuni za michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Kwamba TP Mazembe ilimchezesha Bokungu ambaye bado ni nyota wa Esperance, kwani mkataba wake na wakali hao wa Tunisia, utafikia ukomo Juni mwaka huu, ingawa TP Mazembe wanasisitiza ni mchezaji wao halali.

“Janvier alifuata taratibu zote kuvunja mkataba wake na si Esperance wala Mazembe yenye tatizo na mchezaji huyu, kwa sababu amejiunga nasi kwa maridhiano,” alisema Meneja Mkuu wa Mazembe, Frederic Kitengie.

Simba chini ya Mwenyekiti wake Ismail Aden Rage, ilimkatia rufaa Bokungu, licha ya kung’olewa katika raundi ya kwanza ya michuano hiyo kwa jumla ya mabao 6-3.

Katika mechi ya kwanza ambayo ilichezwa mjini Lubumbashi, Simba ilifungwa mabao 2-1 kabla ya kupigwa 4-1 kwenye marudiano Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.

Kutokana na maamuzi hayo, sasa Simba itakipiga na mabingwa wa Morocco, Wydad Casablanca jijini Khartoum, Sudan, ambako itapigwa mechi moja tu ili kumpata atakayeingia katika kapu la timu nane bora, ambazo zitacheza ligi ndogo.

Tayari zilizotinga nane bora ni Ahly ya Misri, Raja Casablanca ya Morocco, Enyimba ya Nigeria, Esperance ya Tunisia, MC Alger ya Algeria, Al Hilal ya Sudan na Coton Sport ya Cameroon.

Wakati Simba wakifurahia kushinda rufaa, wakali hao wa Morocco, nao wanafurahia kurejea kwenye michuano hiyo kwani tayari walishang’olewa na TP Mazembe kwa jumla ya mabao 2-1.

Wakati hali ikiwa hivyo, leo Wekundu wa Msimbazi Simba, wanatarajiwa kufanya mkutano mkuu wa mwaka kwenye bwalo la Maofisa wa Polisi Oysterbay jijini Dar es Salaam, ikiwa ni mwaka mmoja tangu uongozi wa Mwenyekiti Ismail Aden Rage kuingia madarakani.

Kwa mujibu wa Rage, mkutano huo utakuwa na ajenda za mawasilisho ya mapato na matumizi ya fedha za mwaka, sambamba na kuwasilishwa kwa bajeti ya mwaka ya Kamati ya Utendaji na mengineyo.

Alisema ni mara ya kwanza Simba kuwasilisha taarifa za mahesabu ya mwaka mapema, jambo ambalo walijiandaa kabla ya uchaguzi mkuu, ikiwa ni mojawapo ya mapendekezo yaliyomo ndani ya katiba.

Uongozi wa Rage uliingia madarakani Mei 9 mwaka jana, baada ya uongozi wa mwenyekiti aliyemaliza muda wake, Hassan Dalali, kumaliza miaka mitatu ya uongozi wake.

CHANZO: Tanzania Daima

Sunday, 3 April 2011


Japo mechi ni ngumu sana,na maandalizi yalikuwa duni, historia ya Wana-Msimbazi Simba Sports Club kwenye michuano ya kimataifa ni ya kupigiwa mstari.Na hilo linatupa matumaini ya kuweka historia nyingine kwa kuwafunga hao Wakongomani TP Mazembe na hatimaye kuwavua ubingwa.

Laiti Mazembe wangekuwa na uhakika wa ushindi dhidi ya Simba katika mechi ya awali basi wasingehangaika kutaka kutoa rushwa kwa waamuzi na hatimaye kuwatishia vifo laiti wangemwaga siri hiyo baada ya waamuzi hao kukataa.Habari hiyo nimeisoma HAPA

Kila la heri wana Msimbazi

Saturday, 20 March 2010


MNYAMA AUA ZIMBABWE. Andrew Kingamkono, Harare.

MABINGWA wa soka Tanzania Bara Simba wameirarua Lengthens ya Zimbabwe mabao 2-0 katika mechi ya kuwania kombe la Shirikisho la chama cha soka Barani Afrika CAF iliyofanyika kwenye uwanja wa Rufaro,nchini Zimbabwe.

Mpira ulianza kwa kasi ambapo katika dakika ya 3 Lengthens FC 'Happy People' waliwakosa Simba.

Katika kipindi cha kwanza mabeki wa kati wa Simba Joseph Owino na Kelvin Yondani walikuwa wakijichanganya sana na kuonekana kutoelewana,ambapo kuna wakati bado kidogo wasababishe bao ila mshambuliaji wa Lengthens,Uzukamanda alipiga shuti ambalo lilidakwa na kipa wa Simba Juma Kaseja.

Katika dakika ya 32 Simba ilipata bao la kwanza lililofungwa na Mohamed Banka kwa mpira wa adhabu baada ya kupasiwa na Joseph Owino. Mpira huo wa adhabu ulitokea baada ya Ramadhan Chombo kuangushwa nje ya 18.

Simba iliandika bao la pili katika dakika ya 34 ambalo lilifungwa na Mussa Hassan Mgosi kwa kichwa baada ya kuunganisha mpira wa adhabu uliopigwa na Joseph Owino kutoka winga ya kulia.

Joseph Owino alipiga mpira huo wa adhabu baada ya Nico Nyagawa kufanyiwa faulo.

Lengthens ilitawala mchezo kwa muda.lakini Simba walionekana kurudi mchezoni japokuwa Lengthens walionekana kumiliki zaidi soka kwa kucheza soka ya pasi fupi fupi.

Katika dakika ya 44 na 47 Altwell Nyawima wa Lengthens FC alikosa mabao mawili ya wazi.

Mpaka mapumziko Simba ilikuwa ikiongoza kwa mabao 2-0. Lengthens katika kipindi cha kwanza ilikuwa ikipeleka mashambulizi yao katika winga ya kushoto ambapo alikuwepo beki Haruna Shamte aliyechukua nafasi ya Juma Jabu ambaye alikuwa jukwaani akishuhudia pambano,lakini beki Kelvin Yondani alifanya kazi ya ziada kuzuia mashambulizi ya Lengthens.

Kipindi cha pili kilianza ambapo kulikuwa hakuna mabadiliko ya wachezaji kwa pande zote mbili. Lengthens walianza kipindi hicho kwa kasi na walikosa mabao mawili ambapo shuti la Nhamo liligonga mwamba.

Simba ilifanya mabadiliko ambapo iliwatoa Mike Barasa na Nico Nyagawa na nafasi zao kuchukuliwa na Jabil Aziz na Ulimboka Mwakingwe. Pia Lengthens iliwatoa Steven Matsangaise,Nhamo,Mparati na kuwaingiza Mike Mhunsu,Patrick Makuwaza.

Mabadiliko hayo yaliisaidia Lengthens kurudi mchezoni ambapo katika dakika ya 72 bado kidogo Nyawima afumanie nyavu.Pia katika dakika ya 76 Nxawma alikosa bao akiwa na kipa Juma Kaseja.

Simba ilipata Shambulizi la maana katika dakika ya 83,lakini mshambuliaji Mussa Mgosi alipiga shuti ambalo lilipaa juu ya mwamba.

Kiujumla beki ya Simba inastahili pongezi kwa kucheza kwa kujituma na kuzuia kwa hali ya juu.

Katika mechi hiyo mchezaji wa Simba Haruna Shamte alipewa kadi ya njano kwa kumchezea vibaya Dylaan Chiroodza.

Simba ilifanya mabadiliko tena kwa kumtoa Ramadhan Chombo na kumuingiza Jerry Santo.

Mchezo wa Simba dhidi ya Lengthens ulihudhuriwa na mashabiki wachache kwa sababu jana ilikuwa ni siku ya kazi.

Kikosi cha Simba kilikuwa; Juma Kaseja,Haruna Shamte,Salum Kanoni,Kelvin Yondani, Joseph Owino,Mohamed Banka,Nico Nyagawa,Hillary Echesa,Mussa Hassan Mgosi,Mike Baraza na Ramadhan Chombo.

Lengthens:Makuvarara Lovemore, Mteili Richard,Mparati Tawanda,Machoma Casper,Mono Goderey, Bruce Tshuma,Richard Mteki,Patrick Nshamo,Altwell Nyawima,Asmir Ozukakamanda na Tawanda Mparati.

Mbali na mchezo huo, Caps United ya Zimbazwe itacheza na Morroca Swallows kesho wakati mabingwa wa Zimbabwe Gunners wataonyeshana kazi na Al Ahly ya Misri waliowasili hapa juzi.

CHANZO: Mwananchi.

Sunday, 14 March 2010


Wana-Msimbazi mmeweka rekodi nzuri na inayostahili pongezi.Tunataraji mtatafsiri rekodi hiyo kwa kufanya vema katika michuano ya kimataifa.Penye nia pana njia.
POINTI za Simba sasa zimetosha na imeibuka bingwa wa soka Ligi Kuu Tanzania Bara kwa mwaka 2009/2010, lakini ikiwa ni mara ya 17 kwa klabu hiyo kutwaa ubingwa huo.

Hatua hiyo inatokana na ushindi wa mabao 2-0 iliyoupata jana dhidi ya Azam kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam katika mchezo wa ligi hiyo uliokuwa mkali na wa kusisimua ambao ni wa raundi ya 20.

Kutokana na matokeo hayo, Simba imefikisha pointi 56 ambazo haziwezi kufikiwa na timu yoyote katika ligi hiyo, ambapo Yanga iliyofikisha pointi 45 ikishika nafasi ya pili ikishinda michezo yake mitatu iliyosalia itafikisha pointi 54.

Chereko, nderemo na vifijo vya mashabiki wa Simba vilitawala Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam mara baada ya filimbi ya mwisho ya mwamuzi Ibrahim Kidiwa ambayo iliashiria mwisho wa mechi kati yao na Azam.

Baada ya mpira kumalizika wachezaji wa Simba walizunguka uwanja wakiwapungia mikono mashabiki wao, ambao wengi wao walikuwa wamevalia fulana zenye maneno Simba Bingwa 2009/2011, huku wakiwa wanaonekana wenye furaha isiyo kifani baada ya kutwaa ubingwa huo, huku wakiwa na rekodi safi ya kutopeza mechi yoyote kwenye ligi hiyo na ikiwa imetoka sare mara mbili tu kati ya mechi 20 ilizocheza.

Mabao mawili yaliyofungwa moja katika kila kipindi na mshambuliaji Mkenya wa timu hiyo, Mike Barasa ndio yaliyoiwezesha Simba kuwavua rasmi ubingwa watani zao wa jadi, Yanga, huku ikiwa imesaliwa na mechi mbili mkononi ikiwemo ile dhidi ya watani zao hao itakayochezwa Aprili 11 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Bao la kwanza la Simba lilifungwa dakika ya saba kwa kichwa na Barasa ambaye aliunganisha krosi ya Mkenya mwenzie Hillary Echesa na kuwafanya mashabiki wa Simba kushangilia baada ya kuenea kwa maneno ya uzushi kuwa mnajimu mmoja alitabiri Simba ingepoteza mchezo na isingeweza kutwaa ubingwa.

Baada ya bao hilo Simba ambao walionekana kupania, walilisakama lango la Azam na dakika mbili baada ya bao hilo, Ulimboka Mwakingwe alipiga krosi ndani ya eneo la hatari lakini Musa Hassan ‘Mgosi’ akiwa katika nafasi nzuri ya kufunga alishindwa kumiliki mpira huo, hivyo kupoteza nafasi hiyo. Huku Simba wakionekana kutandaza kandanda safi na kufanya washangiliwe na mashabiki wao waliofurika uwanjani hapo kushuhudia timu yao ikitwaa ubingwa baada ya kuukosa kwa takribani miaka mitatu, walianza kupooza mashambulizi na hivyo kuanza kutoa nafasi kwa Azam ambao walionekana kutawala sehemu ya kiungo kipindi cha kwanza.

Kutokana na udhaifu huo Azam walipeleka mashambulizi kadhaa, langoni mwa Simba na katika dakika 35 washambuliaji John Bocco, Danny Wagaluka walishindwa kupachika bao kufuatia krosi ya Malika Ndeule, baada ya Bocco kuikosa na kipa Juma Kaseja kuuwahi kabla ya kumfikia Wagaluka.

Bocco alikosa bao pale shuti lake alilopiga akiwa kwenye ukingo wa eneo la hatari na kudakwa na Kaseja, dakika mbili baadaye mshambuliaji huyo alijaribu tena shuti kali ambalo lilimtoka Kaseja kabla hajaliwahi na kulidaka tena.

Kipindi cha pili kilianza kwa Azam kufanya mabadiliko ya kuwaingiza Ally Manzi na Mau Ally badala ya Said Sued na Wagaluka.

Mabadiliko ambayo yalionekana kuongeza uhai katika safu ya ushambuliaji ya Azam na kuleta sekeseke kadhaa kwenye safu ya ulinzi ya Simba ambayo ilikuwa ikiongozwa na Kelvin Yondani na Juma Nyosso, kwani Manzi alionekana kumsumbua beki wa kushoto, Juma Jabu.

Simba ilifanya mabadiliko yake ya kwanza dakika ya 55 kwa kumtoa Ulimboka Mwakingwe na nafasi yake kuchukuliwa na Uhuru Selemani na dakika ya 57 nusura Mohamed Banka apachike bao la pili baada ya kupiga shuti kali la adhabu ambalo liligonga mwamba wa juu na kurejea uwanjani huku, kipa Vladimir Niyonkuru akiwa ameshapoteza hesabu, lakini walinzi wake waliokoa.

Dakika ya 60 Azam walijibu shambulio hilo pale Manzi alipomtoka Jabu na kupiga krosi safi ambayo Bocco alichelewa kuinganisha wavuni, dakika mbili baada ya Azam kukosa bao hilo, Uhuru Seleman alitoa pasi ya kubetua kwa Barasa aliyekuwa kwenye eneo la hatari ambaye bila ajizi aliukwamisha mpira wavuni na kuipatia Simba bao la pili.

Yanga iliyokuwa ikitetea ubingwa huo, yenyewe imetwaa kombe hilo mara 21.

CHANZO: Habari Leo.

Saturday, 31 October 2009


Picha kwa hisani ya Michuzi.

MNYAMA KAUA LEO!SUBIRIA TIFU LITAKALOIBUKA JANGWANI BAADA YA KIPIGO HICHO.

Categories

Unordered List

Sample Text

Blog Archive

Labels

Follow Us on FaceBook

Popular Posts

Recent Posts

Recent Comments

Recent Premium Themes

Your Links

Flickr

Powered by Blogger.

Blog Archive

Followers

Download

Your Links

Blogger Tricks

Popular Posts

Recent Posts

Text Widget