Thursday, 5 August 2010

SERIKALI ya Awamu ya Nne imeendelea kukumbwa na jinamizi la matumizi mabaya ya fedha za umma (ufisadi), baada ya kubainika kuwa imetumia sh trilioni 1.7 kwa kipindi cha mwaka 2008/2009 bila maelezo ya kina.

Uchambuzi huo ni ule uliotolewa na Shirika lisilo la kiserikali la ‘Agenda Participation 2000’ juu ya ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) iliyotolewa hivi karibuni, umethibitisha kuwepo kwa ufisadi mkubwa wa fedha za walipa kodi.

Uchambuzi wa ripoti hiyo ya CAG kwa mwaka 2008/2009, umeonyesha ufisadi wa kutisha serikalini kwa kiasi cha sh trilioni 1.7 uliofanyika ndani ya mwaka huo.

“Jumla ya fedha za serikali ambazo ama zilitumiwa vibaya au wahusika wameshindwa kutoa maelezo ya kuridhisha jinsi fedha hizo zilivyotumiwa inafikia shilingi trilioni 1.7. Kwa kweli fedha hizi ni nyingi sana…”, ilisema sehemu ya taarifa hiyo ya shirika hilo.

Kiasi hicho kilichofujwa ni sawa na fedha zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya bajeti ya Wizara ya Elimu na mafunzo ya Ufundi na ile ya Miundombinu katika mwaka huo wa fedha.

Kiasi hicho pia ni sawa na mara mbili ya fedha zilizokuwa zimetengwa mwaka huo kwa ajili ya Wizara ya Afya ambayo ilipata sh bilioni 589 na mara nne ya kiasi kilichokuwa kimetengwa kwa ajili ya Wizara za Kilimo na Maji, ambazo zilitengewa shilingi bilioni 379 na shilingi bilioni 309 katika mwaka wa bajeti wa 2008/2009.

Kwa ujumla, ufisadi huo unahusisha makadirio ya fedha zilizotumiwa vibaya katika eneo la manunuzi yasiyo ya kawaida ya sh bilioni 12.8, masuala ambayo hayakushughulikiwa tangu kaguzi zilizopita sh bilioni 95.7 na misamaha ya kodi ya sh bilioni 752. 3.

Maeneo mengine ni udhaifu katika ulipaji wa mishahara uliofuja sh bilioni 3. 078, masuala yahusuyo malipo ya marupurupu sh milioni 395.8, ukiukwaji katika ununuzi wa magari wa sh bilioni 4. 018, pamoja na kiasi cha sh bilioni 203.2 zilizotumiwa vibaya au kupotea katika serikali za mitaa.

Katika ufisadi huo, Wizara ya Maliasili na Utalii ndiyo imetajwa kama mfano wa kusikitisha wa wizara zilizotumia vibaya fedha za umma.

Sehemu ya ufisadi uliofanyika ndani ya wizara hiyo inahusisha ubadhirifu wa sh milioni 12 zilizolipwa kama mishahara zaidi ya viwango halali vya mishahara ya wafanyakazi na sh milioni 53 zilizolipwa bila kutolewa viambatanisho vya kuhalalisha malipo hayo.

Sh milioni 445 pia zilitumika kulipa wastaafu, marehemu na wafanyakazi walioachishwa kazi, fedha ambazo walengwa hawakujitokeza kulipwa lakini hazikurudishwa hazina.

“Jambo jingine la kusikitisha ni kwamba Wizara ya Maliasili na Utalii ilishindwa kueleza yalipo mapato ya jumla ya shilingi bilioni 19.6,” ilisema sehemu ya uchambuzi huo wa Agenda Participation ikirejea ripoti ya CAG.

Mbali na wizara hiyo ya Maliasili na Utalii, wizara, idara au taasisi nyingine za umma zilizopata taarifa mbaya za fedha kutoka kwa CAG ni Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Jeshi la Polisi na Ofisi ya Makamu wa Rais.

Nayo Serikali ya Norway imeendelea kudai kurudishiwa sh bilioni 2.6 zilizotumiwa vibaya na Wizara ya Maliasili na Utalii.

Hata hivyo, katika taarifa ya bajeti ya wizara hiyo ya mwaka huu wa fedha, wizara hiyo ilisema kuwa ingeilipa Serikali ya Norway fedha hizo.

“Taarifa ya CAG pia inaonyesha utendaji usioridhisha katika nyanja ya mikopo iliyokuwa ikisimamiwa na taasisi za serikali kwa ajili ya wajasiriamali wadogo wadogo miongoni mwa wanawake na vijana nchini.

“Kwa mfano jumla ya sh milioni 355 zinazodaiwa kutolewa kwa wajasiriamali wanawake na vijana hazikuonyeshwa jinsi zilivyotumika. Taarifa za fedha kutoka halmashauri 41 hazikupatikana,” ilieleza taarifa hiyo.

Mashirika ya umma na mamlaka kama vile Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Shirika la Bima la Taifa (NIC), Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Shirika la Taifa la Umeme (TANESCO), Mamlaka ya Bandari (TPA) na Mfuko wa Hifadhi wa Serikali za Mitaa (LAPF) ni maeneo mengine ya upotevu mkubwa wa fedha.

Kwa mfano, ilithibitishwa kuwa jumla ya sh bilioni 58 zilizokuwa zimetolewa kama mkopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu mwaka 2006, mpaka sasa hakuna uhakika wa kulipwa kwa fedha hizo ambazo zilitolewa dhamana na serikali.

“Kinachowasikitisha wengi ni kwanini serikali bado inashindwa kuziba mianya ya baadhi ya maofisa wake kuendelea kutafuna fedha za umma,” umehitimisha muhtasari wa wachambuzi wa wanaharakati hao.


Usikose kutembelea blogu ya Dokta Wilbroad Slaa, mgombea kiti cha urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).Blogu hiyo inayoitwa Friends of Slaa- Marafiki wa Slaa  inapatikana katika anuani ya mtandao http://www.friendsofslaa.blogspot.com

SHIRIKA la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), limesema rushwa iliyojitokeza katika mchakato wa kura za maoni za CCM, ni hatari kwa mustakabali wa taifa.

Kufuatia hali hiyo shirika hilo limewataka Watanzania hasa vijana, kutokubali kununuliwa katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi Oktoba mwaka huu.
“Katika vitu vya kushangaza ni jinsi wagombea ubunge na udiwani wa CCM walivyokuwa wakishindana kutoa rushwa ili wachaguliwe na wananchi,” alisema Meneja Mradi wa Kusaidia Uchaguzi wa UNDP, Oskar Lehner.

Lehner alisema hayo jana jijini Dar es Salaam katika kongamano la siku mbili lililowakutanisha zaidi ya vijana 140 kutoka mashirika mbalimbali yasiyokuwa ya kiserikali na wale wa vyuo vikuu.

Kwa mujibu wa Lehner, uuzaji wa shahada za kupigia kura katika uchaguzi, ni sawa na kuuza malengo ya baadaye katika maisha ya watu hivyo ni vyema Watanzania wakafahamu kwamba mustakabali wa maendeleo ya nchi upo katika kipindi hiki cha Uchaguzi Mkuu.

UNDP inatoa kauli hiyo baada ya vyombo mbalimbali vya habari kuripoti rushwa katika mchakato mzima wa kura za maoni za CCM kuwapata wabunge na madiwani watakaogombea katika uchaguzi ujao.

“Angalieni jinsi matendo ya rushwa yalivyoripotiwa katika mchakato wa kampeni na upigaji kura za maoni ya kuchagua mgombea ubunge na udiwani wa CCM," alisema na kuongeza.

“Wananachi na hasa vijana mjihadhari na kujiepusha na rushwa katika uchaguzi, eleweni kuwa, kuuza shahada yako ya kupigia kura, ni sawa na kuuza malengo ya baadaye katika maisha yako,"

“Mafanikio na maendeleo ya baadaye ya nchi, yapo katika mikono yenu hasa katika kipindi hiki cha Uchaguzi Mkuu.”

CHANZO: Mwananchi

RAIS Jakaya Kikwete amewekewa pingamizi kortini kugombea urais mwaka huu kwa madai ya matumizi mabaya ya madaraka na ufujaji wa fedha za umma katika safari zake za nje.

Hayo yameelezwa na Mwalimu Mstaafu na Mkazi wa Dar es Salaam, Bw. Paul Mhozya ambaye amefungua kesi katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam kupinga mgombea huyo katika uchaguzi wa Oktoba 31, mwaka huu.

Akizungumza na Majira jana, Bw. Mhozya alisema amefungua pingamizi hilo chini ya hati ya dharura akiitaka mahakama kulisikiliza mapema kabla kampeni kuanza, hivyo akaishauri CCM kuteua mgombea mbadala mapema, badala ya kusubiri uamuzi wa mahakama.

Katika hati ya mashtaka yenye sababu kumi za kuiomba mahakama imuengue Rais Kikwete kwenye kinyang'anyiro cha urais Bw. Mhozya anasema, rais ametumia nafasi aliyopewa kwa mambo binafsi, amekiuka katiba na kuvunja haki za binaadamu pamoja na matumizi holele ya fedha za watanzania kwa mambo yake mwenyewe.

Gazeti la The Citizen toleo la jana lilimkariri Bw. Mhozya kuwa aliwahi kufungua kesi ya kikatiba kama hiyo mwaka 1993 dhidi ya Rais Mstaafu, Ali Hassan Mwinyi kuwa alivunja katiba kwa kuruhusu Zanzibar kujiunga na Jumuiya ya Kiislamu (OIC), lakini ikatupwa na Jaji Barnabas Samatta kuwa mamlaka ya kumwondoa rais madarakani yalikuwa mikononi mwa bunge peke yake, chini ya kifungu cha 46A cha katiba.

Bw. Mhozya alisema amefikia uamuzi wa kufungua kesi hiyo kutokana na ujeuri uliooneshwa na Rais Kikwete katika miaka mitano ya uongozi wake, hivyo ni vema akazuiwa kuurudia kwa kumzuia asirudi madarakani.

Alisema anayo orodha ndefu ya mambo mabaya aliyofanya Rais Kikwete wakati wa uongozi wake, ambayo anatarajia kuyatumia kama ushahidi na uthibitisho wa malalamiko aliyopeleka mahakamani, ambayo anaamini yatakubaliwa na kumwondoa kwenye kinyang'anyiro.

"Mwenyekiti wa Tume ya uchaguzi (NEC), Jaji Lewis Makame alikwishasema kuwa tume iko tayari kupokea pingamizi dhidi ya mgombea yoyote kwa maslahi ya umma na kuwa itachukua hatua stahili, ninasubiri kauli ya mahakama na ninaamini itasikiliza hoja zangu na kuzifanyia kazi," alisema.

Alisema kuwa yeye kama Mtanzania anayo mamlaka chini ya ibara ya 30 (3) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufungua kesi dhidi ya uvunjaji wa ibara yoyote ndani ya katiba hasa zinazohusu haki za binaadamu.

Ibara ya 30 (3) inasema "Mtu yeyote anayedai kuwa sharti lolote katika Sehemu hii ya Sura hii au katika sheria yoyote inayohusu haki yake au wajibu kwake limevunjwa, linavunjwa au inaelekea litavunjwa na mtu yeyote popote katika Jamhuri ya Muungano, anaweza kufungua shauri katika Mahakama Kuu"

Bw. Mhozya anasema pamoja na kuwa Rais ana kinga kisheria lakini Kikwete hana kinga ya kuwekewa pingamizi kama mgombea kwa sasa, ndio maana akaamua kufungua kesi hii wakati huu badala ya kusubiri atakaposhinda na kuwa rais, kwani atakuwa na uwezo wa kutumia kinga yake.

Alisema katika kipindi cha uongozi wake rais amefanya safari za ughaibuni zisizo za lazima nyingi kwa fedha za umma, jambo ambalo limesababisha wananch wengi kuishi maisha ya taabu na umaskini mkubwa, huku akidai kuwa urais ni suala binafsi, akisema kuwa ndio maana alimteua mwanawe kumtafutia wadhamini.

Alisema sheria inaitaka NEC kutoa muda wa ziada kwa chama ambacho mgombea wake amekufa au ameshindwa kuendelea kukiwakilisha, ili chama hicho kiweze kuteua mgombea mwingine, hivyo anaamini kuwa baada ya pingamizi hilo kukubaliwa mahakamani, NEC itawaamuru CCM kufanya hivyo kwa kuwaongezea muda.

"Sasa kwa vile sheria inasema NEC itawaongezea muda wa kuteua mgombea mwingine, mimi nashauri wakateua kabisa mgombea mwingine na kumshauri niliyemwekea pingamizi kujitoa, hii itaepusha kupoteza muda pindi pingamizi likikubaliwa, hakuna jinsi," alisema Bw. Mhozya.



Alisema yeye anahofia zaidi mustakabali wa nchi na vizazi vijavyo kuliko anavyohofia maisha yake, hivyo pamoja na vitisho anavyopata bado hataogopa kusimamia ukweli na kuwafichua waovu kama anavyofanya.

"Nimetoka mahakamani leo (jana), nilikwenda kuwaona makarani wa wanipatie 'samansi'(hati ya kuhudhuria mahakamani iliyo na tarehe ya kusikilizwa kesi) lakini walisema bado haijatoka naamini itatoka hivi karibuni ili tukasikilizwe. Matatizo yapo na nilikwisha yazoea," alisema Bw. Mhozya.

CHANZO: Majira

Wakati hayo yakimkumba JK,aliyekuwa Mbunge wa CCM (Bariadi) Andrew Chenge a.k.a Mzee wa Vijisenti nae anakabiliwa na tishio la pingamizi kutoka kwa mmoja ya wana-CCM waliokuwa wakiwania nafasi ya kupitishwa kugombea ubunge kwa tiketi ya chama hicho
. Bonyeza HAPA Kusoma Zaidi Kuhusu Chenge.

Natoa wito kwa wanachama walioomba nafasi lakini wakakosa, jamani msiwe chanzo cha mifarakano ndani ya chama, KAZI ZIPO NYINGI,TUNAWEZA KUTEUANA, fanyeni kazi ya ushindi kwa chama chetu,” .Hayo si maneno yangu bali ya Rais Jakaya Kikwete aliyoyatoa siku alipochukua fomu za kuogombea tena urais kwa tiketi ya CCM.Ni kweli kazi zipo nyingi ikiwa ni pamoja na kilimo au biashara lakini haiingii akilini kwa watu waliokataliwa na wananchi kupewa nafasi kwa mlango wa "kuteuana".

Hili ni tatizo sugu katika siasa za Tanzania.Utakuta mtu ameboronga sehemu moja kisha anahamishiwa sehemu nyingine.Yayumkinika kusema kuwa kuteua "rejects" hao sio tu matumizi mabaya ya ruhusu inayotolewa na katika kufanya teuzi mbalimbali bali pia ni dharau ya moja kwa moja kwa wananchi.

Haiwezekani kwamba nchi yenye watu zaidi ya milioni 40 iwe na kikundi kidogo tu cha watu wenye uwezo wa kuwa viongozi.Na kibaya zaidi kikundi hicho kikijumuisha watu waliokataliwa na wananchi katika chaguzi au maombi yao ya kutaka wachaguliwe kuongoza.

Na ukiingia kiundani zaidi kuangalia tabia hii isiyopendeza,unaweza kuyumkinisha kuwa hata uteuzi wa Dkt Gharib Bilal unaangukia kwenye eneo hilohilo.Bilal alitaka ridhaa ya vikao vya CCM kuwa mgombea wa Zanzibar lakini "kura hazikutosha".Hata hivyo,katika kile kinachoelezwa kama kujenga mshikamano miongoni mwa wana-CCM,Bilal aliteuliwa na JK kuwa mgombea mwenza wake.Kwa maana nyingine,mtu aliyekataliwa na kikundi kidogo (kikao cha CCM kilichpiga kura kumpata mgombea urais wa Zanzibar) anaweza kuwa Makamu wa Rais wa Watanzania milioni 40 na ushee pindi JK akishinda katika uchaguzi ujao.

Tumekuwa tukishuhudia teuzi za mabalozi wetu nje ya nchi,wenyeviti wa bodi za wakurugenzi wa taasisi mbalimbali,wakuu wa mikoa na wilaya na nafasi mbalimbali zinazojazwa kwa teuzi zinazofanywa na rais zikijazwa na "rejects"-watu walionyimwa ridhaa ya kuongoza na wananchi lakini wanaishia kuwa viongozi kwa mlango wa nyuma.Yaleyale ya aliyekuwa Katibu Mkuu wa UWT,Hasna Mwilima.Kikundi kidogo katika jumuiya hiyo ya akinamama wa CCM kilimkataa,huku sababu kuu ikitajwa kuwa ni uongozi mbovu.Lakini siku chache baadaye,Rais akamteua mwanamama huyo kuwa Mkuu wa Wilaya.Busara kidogo tu zinaweza kubainisha kuwa kuwa mtu alokataliwa kuongoza UWT hawezi kuwa "rais wa wilaya" (DC) lakini kwa vile Katiba inamruhusu Rais kuteua yeyote amtakaye,analotaka liwe litakuwa.

Ni katika mazingira haya ndio maana tetesi kuwa Lowassa,Waziri Mkuu aliyelazimishwa kujiuzulu kutokana na ufisadi wa Richmond,atarejea madarakani pindi JK akishinda hapo Oktoba zinazidi kupata nguvu kwa vile Rais akiamua iwe na itakuwa.Na kwa vile Watanzania wanasifika kwa upole wao,hakutokuwa na "kelele" za kupinga uteuzi huo.

Nguvu anazopewa Rais kwenye Katiba hazimaanishi ajifanyie mambo anavyotaka bali ni kwa minajili ya kuwatumikia Watanzania kwa ufanisi.Lakini kwa upande mwingine,lawama zinaweza kuelekezwa kwa taasisi zinazomshauri Rais kuhusu teuzi mbalimbali (ikiwa ni pamoja na kuchunguza 'usafi' na uwezo wa wateuliwa watarajiwa) kwa sababu inaelekea kwa wao,kila jina linaloletwa na Rais ni 'safi'.Professionalism na ethics zinawekwa kando kwa minajili ya kumfurahisha mkuu wa nchi.

Sunday, 1 August 2010

Taarifa zinaeleza kuwa msanii mkongwe wa muziki wa Bongoflava,Joseph Mbilinyi a.k.a Sugu,ameshinda kura za maoni za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema)kuwania nafasi ya kuogmbea ubunge wa jimbo la Mbeya Mjini.

Kila la heri Mr Sugu.Jitihada zako zinapaswa kuwa fundisho kubwa kwa idadi kubwa ya wasanii (hususan wa Bongoflava) ambao kwa wao photo-ops (kuuza sura) na watawala wetu is everything despite having been USED AND ABUSED by same watawala kila unapojiri uchaguzi.

That's wassup,Sugu!

Baada ya kusubiriwa kwa muda mrefu,hatimaye kampuni ya HTC imetangaza rasmi kwamba watumiaji wa simu aina ya HTC DESIRE watapatiwa toleo jipya (version 2.2) la mfumo wa kuendesha simu (operating system -OS- ya Android linalofahamika kama Frozen Yorghut (Mtindi wa Mgando) kwa kifupi Froyo.Kwa mujibu wa taarifa mbalimbali,Froyo itaanza kusambazwa hewani (OTA-over the air) wiki hii kwa wenye HTC Desire ambazo "hazijafungwa" (unlocked) na baadaye kwa "zilizofungwa" (locked) kabla ya kusambazwa kwa simu nyingine zinazotumia OS hiyo ya Android.

Inatarajiwa kuwa Froyo itaziboresha zaidi simu za Android,kwa mfano HTC Desire,ambayo inalinganishwa kwa karibu na "mama wa simu zote",Apple iPhone.Binafsi,nimekuwa nikitumia HTC Desire kwa takriban miezi mitano hivi na kwa hakika ni simu iliyojitosheleza kwa takriban kila kitu.Tatizo pekee hadi sasa,na ambalo limepatiwa ufumbuzi kwenye toleo la Froyo,ni kutoweza kuhifadhi Apps (applications) kwenye memory card hivyo kupelekea simu kuwa na Apps za muhimu tu ilhali kuna maelfu kwa maelfu ya Apps kwenye "soko" la vidude hivyo (Market).

Categories

Unordered List

Sample Text

Blog Archive

Labels

Follow Us on FaceBook

Popular Posts

Recent Posts

Recent Comments

Recent Premium Themes

Your Links

Flickr

Powered by Blogger.

Blog Archive

Followers

Download

Your Links

Blogger Tricks

Popular Posts

Recent Posts

Text Widget