Thursday, 29 July 2010

TANZANIA imetajwa katika ripoti ya Kipimo cha Hali ya Rushwa Afrika Mashariki (EABI), kuwa na taasisi zinazoongoza kwa rushwa kwa nchi za Afrika Mashariki.

Akizungumza na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Mratibu wa sekretarieti ya Jukwaa la Wazi (TRAFO), Kaiza Buberwa, alisema kuwa utafiti huo ulifanywa kwa kushirikisha sampuli 10,469 na watu 3,231 walihojiwa kwa Tanzania.

Alisema kuwa katika utafiti huo uliofanyika chini ya wataalamu wa nchi husika, ulifanyika Febrauari na Machi ambapo nchi za Kenya, Burundi, Tanzania, Rwanda na Uganda zilihusishwa.


. Buberwa alisema taasisi zinazoongoza kwa rushwa katika Afrika Mashariki ni Jeshi la Polisi, Mahakama, Jeshi la Ulinzi na Kujenga Taifa, Wakala ya Usajili wa Vifo na Vizazi (RITA), Magereza, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi katika kutoa huduma kwa wananchi, sambamba na ajira.


Alisema kuongoza kwa taasisi hizo ni kutokana na sampuli hiyo ya watu hao, ambao walizitaja taasisi zilizokithiri kwa rushwa wakati wa kupata huduma za kijamii.

Buberwa alisema kwa kuongoza kwa rushwa katika idara nyeti za serikali kwa Afrika Mashariki, Jeshi la Polisi limechukua nafasi ya tano kwa asilimia 65.1 na Mahakama kuwa nafasi ya 10 kwa asilimia 56.4 katika utoaji wa huduma katika misingi ya rushwa.

Aidha, alisema kuwa katika ripoti hiyo haisemi Tanzania hakuna rushwa wala rushwa kidogo, ripoti inasema kwamba ni kwa kuzingatia idadi ya matukio ya vitendo vya rushwa katika idara kadhaa za umma wakati wa kutoa huduma kwa wananchi ikilinganishwa na nchi za Burundi, Kenya, Uganda na Rwanda.

Buberwa alisema kuwa baadhi ya Watanzania asilimia 85.8 wanaamini kuwa hali ya rushwa Tanzania ni mbaya, wakati asilimia 40.6 wanaamini serikali hatimizi wajibu wake katika kuondoa rushwa na kuimarisha utawala bora.

Alisema taasisi nyingine zinazofuata katika rushwa kwa utoaji wa huduma kwa jamii ni Jeshi la Ulinzi na Kujenga Taifa (JKT) asilimia 74.2, Wakala ya Usajili wa Vifo na Vizazi (RITA), asilimia 66.2, Magereza asilimia 61.9, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) asilimia 46.8, Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi asilimia 47.9.

CHANZO: Tanzania Daima

.

Wednesday, 28 July 2010

Ni dhahiri kwamba kila Mtanzania mzalendo na mwenye uchungu na nchi yetu anatamani kuona mambo yakibadilika huko nyumbani.Nchi yetu ina takriban miaka 50 tangu ipate uhuru mwaka 1961.Ukiondoa uvamizi wa nduli Idi Amin mwaka 1978-79,nchi yetu imeendelea kuwa na sifa ya kipekee ya amani na utulivu huku tukishuhudia "nyumba za majirani zetu zikiteketea".Chama tawala CCM kimekuwa kikijigamba kuwa amani na utulivu huo ni matokeo ya sera zake nzuri na uongozi uliotukuka.Haihitaji kuwa mwanafunzi wa siasa kama mie kufahamu kuwa amani na utulivu tulionao unasababishwa na uvumilivu wa Watanzania.Na ni uvumilivu huo huo unaowafanya CCM watuone wajinga,watupelekeshe watakavyo na waifilisi nchi yetu huku tukifahamu fika namna ya kuwadhibiti.Imetosha.Uvumilivu una mwisho,na mwisho huo ni sasa.

Na hata hilo suala la amani na utulivu lina utata kinamna flani.Wachambuzi wa siasa wanabainisha kuwa kutokuwa na machafuko au vita si viashiria kamili vya amani na utulivu.Hebu jiulize msomaji mpendwa,wazee wetu wastaafu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wana amani gani wakati fedha zao ziliibiwa na wajanja (mafisadi)  katika serikali ya CCM?Je wakulima wanaokopwa na vyama vya ushirika kila unapojiri msimu wa mavuno wana amani gani wakati wanashuhudia namna mavuno yao yanavyorutubisha vitambi vya mafisadi wa vyama vya ushirika?Mabaamedi wana amani gani katika mishahara ya kijungujiko wanayopewa (na inayokatwa kila siku kila glasi au chupa inapovunjika)?Watoto zetu au wadogo zetu wana amani gani wanaposoma kwenye shule zisizo na madawati huku walimu wao wakinyong'onyea kutokana na mazingira duni ya kazi?Na je watumishi wa umma wana amani gani ilhali wanapodai haki zao wanaishia kudharauliwa kuwa kura zao hazihitajiki (as if mishahara yao ni fadhila kwa kumchagua kiongozi)?

Na madereva wa daladala na mabasi ya mikoani wana amani gani ilhali askari wa usalama barabarani wanawakamua kila siku kana kwamba rushwa ni sehemu ya sheria za usalama barabarani?Na huko magerezani kuna Watanzania wangapi wasio na amani kwa vifungo vya kubambikizwa kesi,kushindwa kutoa rushwa kwa polisi au hakimu au uonevu pasipo sababu?Na dada na mabinti zetu wenye sifa stahili za kupata ajira wana amani gani ilhali kila wanapofanya maombi ya kazi wanakumbana na masharti ya "ngono kwanza,kisha ajira"?Na wagonjwa wetu wana amani gani wanapolazwa sakafuni katika wodi za hospitali mbalimbali (na hii ilimtoa machozi Supamodo Naomi Campbell)?

Mtanzania ana amani gani wakati kila siku anashuhudia namna nchi yake inavyozidi kuhujumiwa na mafisadi?Wanaoamini katika utawala wa sheria wana amani gani wanaposhuhudia mtu kama Lowassa anapewa air time kwenye televisheni ya taifa inayoendeshwa kwa fedha za walipa kodi (na mahijiano hayo hayafanyikii gerezani)?Yani fedha za walipa kodi zinatumika kusafisha watuhumiwa wa ufisadi!

Na walalahoi wana amani gani wanaposhuhudia serikali waliyoiweka madarakani,na iliyoahidi maisha bora kwa kila Mtanzania,ikielekeza nguvu kubwa katika kukumbatia mafisadi huku viongozi wa serikali hiyo wakiishi maisha ya kifahari kana kwamba Tanzania ni nchi ya "dunia ya kwanza"?Na wasafiri wanaotegemea huduma za Reli ya Kati au Tazara wana amani gani wakati usafiri wao unategemea kudra za Mwenyezi Mungu ?

Yapo mengi ya kueleza kuhusu namna CCM inavyofanya kila jitihada ya kubomoa hata kile kidogo kilichobaki kwenye "amani na utulivu".Ni dhahiri kuwa chama hiki kimevimbiwa madarakana na hakijali kuona Tanzania ikielekea kwenye korongo lenye kina kirefu.CCM inaweza kufanya kila hila ili ibaki madarakani kama ilivyowazuga Waislamu mwaka 2005 kuwa ingewapatia Mahakama ya Kadhi,lakini baada ya ushindi wa "kishindo" kwenye uchaguzi mkuu uliopita suala hilo limeendelea kuwa ngonjera tu huku akina Msekwa wakisema hili,Pinda akisema lile na Chikawe akiongea vile.Huku ni kuchochea vurugu.

Tanzania haiwezi kupiga hatua katika mfumo wa sasa wa kifisadi ambapo madaraka yanatolewa kwa minajili ya ushkaji huku watawala wakijiona miungu watu wenye uwezo wa kufanya watakayo hata kama yanapelekea kuhatarisha "amani na utulivu" wetu.

It's high time to say enough is enough.Na namna pekee ya kuwaadhibu CCM ni kuwanyima kura katika uchaguzi mkuu ujao.Binafsi,nina imani kubwa na Dokta Wilbroad Slaa,mgombea urais kwa tiketi ya Chadema.Ameonyesha ukomavu wa hali ya juu katika kutetea hali zetu na kupambana kwa dhati dhidi ya ufisadi.Nafasi adimu kama hizi huwa hazijirudii.Tukifanya kosa la kuiacha CCM madarakani hapo Oktoba tutaishia kujilaumu.Nia tunayo,sababu tunazo (tena elfu kidogo) na uwezo tunao (siku ya kupiga kura).Mnaopewa rushwa ili muichague CCM pokeeni kwa vile rushwa hiyo ni fedha mlizoibiwa.Wato rushwa hao hawana uwezo wa kushinikiza muwapigie kura hasa ikizingatiwa kuwa hamkuwaomba wawahonge na wanachowanhonga is in fact fedha zenu wanazowaibia kwa ufisadi.

Inawezekana ukitimiza wajibu wako

Tuesday, 27 July 2010


Mtunzi wa kitabu hiki maridhawa si mwingine bali ni mchambuzi na mwandishi mahiri wa makala,Mwalimu Nkwazi Nkuzi Mhango,Mtanzania mwenye makazi yake nchini Kanada.Licha ya ualimu na uandishi wa habari,Mhango pia ni mwanaharakati wa haki za binadamu.Miongoni mwa safu maarufu za Mwalimu Nkwazi (pichani chini) ni zile zinazopatikana katika gazeti la Tanzania Daima,ambapo hutumia jina la MPAYUKAJI MSEMAOVYO.Kadhalika,mwandishi huyu ni hodari katika fani ya kublogu,na "uwanja wake" unafahamika kama Free Thinking Unabii .Vilevile,unaweza kusoma makala za Mwalimu Nkwazi katika jarida la The African Executive
Usikose nakala ya kitabu hiki ambacho kinakuja wakati mwafaka kabisa kwa Watanzania waliochoshwa kuona nchi yao ikigeuzwa "shamba la bibi" na mafisadi wanaopita huku na huko "kuomba ridhaa yetu" warejee madarakani kutufisadi zaidi.

Monday, 26 July 2010

Pichani juu  kitabu cha cha sanaa cha comic kinachoitwa TOM & JENNY IN TANZANIA  ambacho kilikuwa kinasubiriwa kwa muda mrefu, na sasa kitabu kimetoka.Unaweza kukipata jijini Dar es salaam na vilevile wachapishaji wanaweza kuwatumia wasomaji walio nje ya Dar es salaam na Tanzania kwa ujumla.
----------------------------------------------------------------------
Joe
Baseline Africa

Alma
Alma akiwa na playwriter Greg Freeman
Alma na cast nzima ya BEAK STREET
Alma Eno, Natasha Whites na Alice Transfield
Msanii wa maigizo na filamu mwenye asili ya kitanzania Alma Eno, ameng'ara na kutikisa ulimwengu wa Theatre mjini London kwenye onyesho la mchezo uitwao BEAK STREET ulioandikwa na mwandishi maarufu Greg Freeman, na kuongozwa na Ken McClymont.

BEAK STREET ni mchezo wa kijangili ulio kwenye ulimwengu wa Mapaka. Mchezo huo umekuwa ukionyeshwa kwenye kitongoji cha West End mjini London, ambacho ni maarufu kwa majumba ya maigizo,sinema na starehe. Beak Street imeonyeshwa kwa wiki 24 sasa katika majumba ya Tabard Theatre na Theatre Delicatessen (Sekunde 30 kutoka Selfridges)

Alma Eno anacheza silka mbili kwenye igizo hili; kwanza anacheza paka teja ambaye anaweza kuuza mtu yeyote kwa maziwa ya unga.

Vilevile anacheza silka ya Chorus ambayo anakuwa nafsi ya jangili Beak. Onyesho lake limesifiwa sana na wahakiki na sasa amefanikiwa

kuingia mkataba wa kuigiza kwenye mchezo mpya wa Zip Postcode Wars ambao unaendeshwa na gwiji Ray Shell.

Alma ambaye ni mwigizaji wa kulipwa, alipata shahada yake ya sanaa na maigizo kutoka chuo maarufu cha Mountview Academy of Theatre and Art. Chuo hiki kina sifkia kwa kutoa waigizaji maarufu wa kimataifa kama Amanda Holden,Nick Moran, Ayub Khan Din mwandishi wa mchezo na sinema ya East is East and director Edward Hall. Da Eno pia ameshawahi kucheza kwenye kipindi cha televisheni ITV hapa Uingereza kiitwacho Collision. Vilevile yuko kwenye filamu ya British Art iitwayo Boggie Woogie.

Maneno ya Critics chini

Freeman and Ken have once again dipped into the absurd with their new production Beak Street - a dark comedy of noir shadows, mean streets and gangster cats, where only one thing is really certain:cats , they aint known for their loyalty

"A testament to freeman's faith in his imagination and ours"-Time Out Critics' Choice ****

"This is a fine and powerful play that pulls no punches"-Chiswick Times

"Iron-rod narrative and polished script.. imaginative staging.. all makes Beak Street excellent value for money"-Extraextra.com
------------------------------------------------------------------------
Baraka

URBAN PULSE

Tuesday, 20 July 2010

Kuna habari kuwa huenda Katibu Mkuu wa Chadema,Dkt Wilbrod Slaa,atakuwa mgombea urais wa chama hicho katika uchaguzi mkuu ujao.Kwa mujibu wa gazeti la Daily News,Kamati Kuu ya chama hicho iliyokutana jana jijini Dar imemuomba Dkt Slaa kugombea nafasi hiyo.

Kwa mujibu wa habari hizo,Naibu Katibu Mkuu wa Chadema,Zitto Kabwe,alinukuliwa akisema "Kamati Kuu (ya Chadema) imemuomba Dkt Slaa kuwa mgombea wa chama (katika nafasi ya urais)".Hata hivyo,Zitto alieleza kuwa uamuzi wa Kamati hiyo Kuu sio wa mwisho kwani itabidi mgombea urais wa chama hicho athibitishwe na Mkutano Mkuu wa chama hicho ambao umepangwa kufanyika Agosti 10.Kadhalika,Zitto hakuweza kueleza kama Dkt Slaa,ambaye gazeti hilo halikufanikiwa kumpata kuthibitisha habari hizo, amekubali ombi hilo au la.

Hata hivyo,vyanzo vya gazeti hilo katika kikao hicho (kilichokuwa kinaendelea wakati gazeti hilo linaenda mtamboni) vinaeleza kuwa Dkt Slaa,ambaye licha ya Ukatibu Mkuu wa Chadema ni Mbunge wa Karatu kwa tiketi ya chama hicho, amekubali ombi hilo.Habari hiyo ya Dkt Slaa kukubali ombi la kugombea urais kwa tiketi ya Chadema imeandikwa pia kwenye mtandao maarufu kwa habari na mijadala makini,Jamii Forums.

Dokta Slaa amejikusanyia umaarufu mkubwa miongoni mwa Watanzania kutokana na msimamo wake mkali dhidi ya ufisadi.Japo ni mapema kubashiri nafasi yake katika uchaguzi huo unaotarajiwa kufanyika mwezi Oktoba mwaka huu,ni dhahiri kuwa iwapo atasimama kama mgombea wa Chadema anaweza kutoa upinzani mkubwa kwa mgombea wa CCM,Rais (wa sasa) Jakaya Kikwete hususan katika namna chama hicho tawala kilinavyoonekana kama kichaka na hifadhi ya ufisadi na mafisadi.


SIKU moja baada ya Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete kueleza umma wa Watanzania kwamba ongezeko la magari na kero ya msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam ni dalili ya maisha bora, wanazuoni na wanasiasa nchini wameikosoa kauli hiyo na kuilaani vikali.

Wamesema kauli hiyo ni dalili tosha kwamba CCM imekosa mwelekeo halisi ya maendeleo ya nchi hivyo haistahili kuendelea kutawala kwa kuwa haina dira ya kubali maisha ya Watanzania.

Mhadhiri katika kitivo cha Sayansi ya Siasa ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Bw. Bashiru Ally aliliambia Majira kuwa ni aibu kwa kauli hiyo kutolewa na kiongozi wa nchi aliyebeba dhamana ya taifa zima.

Alisema ongezeko la fedha, majumba ya kifahari kwa watu wachache na foleni za magari jijini Dar es Salaam hakuwezi kuchukuliwa kama kipimo cha maisha bora kwa kuwa hivyo si vigezo vinavyopaswa kutumiwa kupima kiwango cha maendeleo katika nchi yoyote duniani.

Alisema maisha bora na maendeleo yoyote katika nchi yanapaswa kupimwa kwa kuzingatia ongezeko la watu, upatikanaji wa ardhi, siasa safi na uongozi bora mambo ambayo bado ni ya taabu na yanayozua migogoro mikubwa nchini.

"Kauli hii inanikumbusha kauli ya hayati Korimba (Horance), kuwa CCM haina dira wala mwelekeo, huwezi kupima maisha bora ya mwananchi wa Masasi au Kagera kwa kuangalia foleni za magari Dar es Salaam, laiti kama Mwalimu (Nyerere) na Sokoine (Moringe) wangekwepo leo kauli hii ingewapandisha presha," alisema Bw. Bashiru.

Alisema ni vema Rais Kikwete akaangalia uwiano wa ngezeko la foleni hizo na uboreshaji wa miundombinu hususan barabara, shule na mfumko wa bei za bidhaa na thamani ya fedha ambavyo vimekuwa vikiporomoka kwa kasi katika kipindi cha uongozi wake.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Bw. Freeman Mbowe, alisema kauli hiyo inaonesha jinsi serikali ya CCM isivyokuwa na jambo la kujivunia kwa wananchi katika kipindi chote cha miaka mitano iliyopita.

Alisema kimsingi msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam inasababishwa na ukosefu wa miundombinu ambayo chimbuko lake ni uongozi mbovu ulioko madarakani.

Alisema kinachotokea Dar es Salaam si kuboreka kwa maisha ya wananchi bali ni ongezeko la tabaka kati ya walionacho na wasio nacho hasa masikini walioko vijijini hali ambayo inasababisha ongezeko la watu mijini wasiokuwa na ajira wala mahali pa kulala.

"Foleni za magari Dar es Salaam si dalili ya maisha bora, na kama ukifanya utafiti utagundua kuwa foleni kubwa ni katika baadhi ya barabara zinazoelekea kwa matajiri wachache ambao baba, mama na watoto kila mmoja ana gari lake, sasa maendeleo ya watu wachache huwezi kuyatumia kupima kiwango cha maisha ya Watanzania wengine," alisema Bw. Mbowe.

Naye Mhadhiri Mwandamizi katika Kitivo cha uchumi na Biashara Chuo Kikuu cha Dar Salaam, Profesa Humphrey Moshi, alisema si sahihi kwa rais wa nchi kupima maisha ya Watanzania wachache wengi kwa kutumia mfano wa watu wachache wenye uwezo wa magari.

Alisema licha ya ukweli kuwa ongezeko la idadi ya watu wanaomiliki magari linaweza kutumika kuonesha ongezeko la kipato kwa wananchi lakini haikuwa sahihi kwa kiongozi wa nchi kupima maisha ya Watanzania kwa kuangalia wenye uwezo wachache walioko Dar es Salaam.

Alisema Dar es Salaam ni mji wa kibiashara wenye viwanda, mashirika na taasisi karibuni zote za serikali ambazo katika shughuli za kawaida zinahitaji usafiri wa magari, hivyo kuna uwezekano kuwa foleni kubwa husababishwa na magari ya taasisi, hizo lakini si mabadiliko ya maisha ya Watanzania.

"Magari mengi si ya watu binafsi, idara nyingi za serikali ziko hapa, kuanzia ikulu, bunge, wizara zote, taasisi binafsi, mashirika ya dini, viwanda na wafanyabiashara mbalimbali ambao ndio wamiliki wa magari, sio wananchi wa kawaida, sasa huwezi kusema kuwepo kwa foleni za magari ya idara hizi ni maisha bora kwa wananchi," alisema Prof. Humpherey.

Alisema maendeleo yanapimwa kwa kuangalia maisha ya jumla si ya mwananchi mmoja mmoja, ikiwa ni pamoja na kuangalia uwezo wa kuzalisha mali wa wananchi, thamani ya fedha, kiwango cha elimu na uimara wa sekta za viwanda na kilimo, na si kuangalia msongamano wa magari yaliyokosa barabara za kupita.

Akihutubia wana CCM na wananchi wa Mkoa wa Dar es Salaam katika mkutano wa kuwatambulisha wagombea urais, mgombea mwenza na Rais wa Tanzania Visiwani katika viwanja vya Mnazi Mmoja, Rais Kikwete alisema ongezeko kubwa la magari na kusababisha msongamano wa magari ni mijawapo ya dalili za maisha bora.

CHANZO: Majira

Monday, 19 July 2010

Foleni za magari ni maisha bora-JK
Monday, 19 July 2010 05:33
*Asema watakakamatwa kwa rushwa CCM haitawatetea

Na Peter Mwenda

MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Kikwete ametamba kuwa chama hicho kwa miaka mitano iliyopita kimeinua maisha ya Watanzania akitoa mfano wa Jiji la Dar es Salaam kuwa foleni za magari zinatokana na wananchi kuwa na maisha bora.

Alitoa kauli hiyo jana wakati akizungumza katika mkutano ulioandaliwa na CCM Mkoa wa Dar es Salaam kwa ajili ya kumpongeza Rais Kikwete kuchaguliwa kuwa mgombea pekee wa urais kwa asilimia 99.16, Dkt. Ali Mohammed Shein kuchaguliwa kuwa mgombea wa Urais Zanzibar na Dkt. Mohamed Gharib Bilal kuteuliwa kuwa Makamu wa Rais.

"Hapa Dar es Salaam taabu ya msongamano wa magari inaonesha hali ya maisha ni bora, sasa tunahangaika jinsi ya kuondoa msongamano, kuanzia mwakani tutaanza kujenga barabara za juu," alisema Rais Kikwete.

CHANZO: Majira

Hivi kumbe maendeleo yanapimwa kwa msongamano na foleni za magari!Vipi kama foleni hizo ni matokeo ya mindombinu isiyoendana na mahitaji?Vipi kama wingi wa magari hayo ni matokeo ya ufisadi-aidha ya wizi na ubadhirifu wa mali ya umma na ukiukwaji wa taratibu mbalimbali eg ukwepaji kodi stahili bandarini na TRA?

Na je,foleni hizo za magari zinaendana vipi na idadi ya Watanzania wanaumudu mlo wao kila siku?Je wingi wa magari unaendana na idadi ya wamiliki wa magari?Nauliza hivyo kwa sababu wengi tunafahamu kuwa wakati kuna wachache wenye msururuwa magari na majumba ya kifahari kuna wengine wengi tu ambao hata fedha ya kununulia baiskeli hawana,achilia mbali uhakika wa nauli ya daladala.

Na je inawezekana Rais hajafahamishwa na wasaidizi wake kuhusu ongezeko la 'TZ ELEVEN' i.e. watembea kwa miguu ambao hawafanyi hivyo kama sehemu ya mazoezi ya viungo mbali ukosefu wa nauli?Au hawajamwambia kuhusu idadi ya 'mikweche' ambayo licha ya kusababisha foleni inachangia uwezekano wa ajali?Na inawezekana pia wasaidizi wake hawajamfahamisha kuwa mingi ya 'mikweche' hiyo iko barabarani baada ya wamiliki kutoa 'kitu kidogo' kwa askari wa usalama barabarani?

KAMWE MAJIBU RAHISI KWENYE MASWALI MAGUMU HAYAWEZI KULETA UFUMBUZI WA MATATIZO YETU!SINTOSHANGAA TUKISKIA HATA KUONGEZEKA KWA WENYE VITAMBI (INCLUDING WALE WENYE VITAMBI VYA KWASHAKOO) NAKO NI DALILI YA MAISHA BORA!

Sunday, 18 July 2010

Jumatatu iliyopita,gazeti la Mwananchi lilikuwa na habari yenye kichwa 'DAWA YA UKIMWI YAGUNDULIWA'.Siku mbili baadaye,gazeti hilohilo lilikuwa na habari yenye kichwa 'MWAKYUSA: TUMSHUKURU MUNGU KWA DAWA YA UKIMWI'.Binafsi,niliposoma habari ya kwanza nilipatwa na mshangao kuwa inakuwaje habari nzito kama hiyo isipate uzito mkubwa kwenye vyombo vya habari vya kimataifa.Kama kawaida yangu,unapojitokeza utata kuhusu habari,nika-google 'HIV cure'.Tofauti na ilivyoripotiwa na gazeti hilo la Mwananchi,matokeo ya search yangu hayakukuwa na jibu la uhakika.

Nilishtushwa zaidi na kauli ya Waziri wa Afya,profesa wa utabibu,Davidi Mwakyusa,alivyoingia kwenye mkumbo wa 'kushangilia kupatikana kwa dawa ya ukimwi' pasipo kufanya utafiti wa kutosha.Na mahala rahisi pa kufanya utafiti wa aina hiyo ni mtandaoni.

Na pengine katika hali inayoweza kutafsiriwa kama 'kumpa darasa Profesa Mwakyusa',msomi mwezie Profesa Fred Mhalu wa Chuo Kikuu cha Tiba na Afya Muhimbili,ametoa tahadhari kuhusu habari hiyo ya ugunduzi wa dawa ya ukimwi.Msomi huyo ambaye ni Mkuu wa Idara ya Microbiology na Immunology,na ambaye amekuwa akijihusisha na tafiti kuhusu ugonjwa huo,amebainisha kuwa kilichogundulika ni protein antibody tu,na inabidi kusubiri mpaka chanjo itakayoweza "kutekenya" (stimulate) antibody hiyo itapopatikana,na kwa sasa haiwezekani kusema hatua hiyo itachukua muda gani.

Profesa Mhalu ametahadharisha pia kuwa huko nyuma kulishawahi kuwa na ripoti kama hizo lakini hazijaweza kuzaa matokeo yanayotarajiwa.Hata hivyo,alisema kuwa hatua iliyofikiwa ni ya kutia matumaini kwenye mwelekeo wa kupata tiba kamili japokuwa hawezi kutamka kwa hakika kuwa ufumbuzi wa tatizo hilo umeshapatikana.

Awali,Profesa Mwakyusa alinukuliwa akisema "Kama ni kweli dawa hiyo imepatikana, ni jambo la kumshukuru Mungu kwa kuwa Ukimwi ni ugonjwa ambao umeiathiri sana dunia."Ama kwa hakika usingetarajia kauli ya 'kimtaani' (layman's language) kutoka kwa mtu mbaye licha ya kuwa Waziri mwenye dhamana katika suala la Afya lakini pia ni msomi katika fani ya utabibu.Japo ni vizuri kumshukuru Mungu kwa taarifa za kutia matumaini kama hiyo,lakini watu wenye dhamana na hususan wasomi kwenye taaluma ya utabibu wanatarajiwa kutoa kauli zinazoelemea zaidi kwenye facts badala ya hisia za binafsi.Pengine kabla ya kutoa kauli hiyo iliyoongeza uzito katika habari husika,Waziri Mwakyusa angeweza kufanya 'quick search' kwenye simu (kama sio kompyuta) yake na kupata facts sahihi kisha kuwaeleza Watanzania ukweli kuhusu habari hiyo.

Kwa mujibu wa kiongozi wa utafiti uliopelekea habari hiyo,Dakta Garry Nabel wa Taasisi ya Taifa ya Allergy na Magonjwa ya Kuambukiza ya Marekani,protini zilizogunduliwa,yaani antibodies hizo,zinatumiwa na mfumo wa kinga ya mwili kutambua na kushambilia vimelea vya maradhi kama bakteria na virusi."Nina kuhusu chanjo ya ukimwi kwa sasa kuliko ilivyokuwa miaka 10 iliyopita",alisema mtafiti huyo katika kauli iliyopelekea msisimko wa aina yake sehemu mbalimbali duniani.

Virusi vya ukimwi hushambulia mfumo wa mwili kujikinga na maradhi na hivyo kumwacha mwathirika katika hatari ya maambukizi na maradhi.Tangu virusi hivyo vigunduliwe takriban miaka 30 iliyopita,wanasayansi wamekuwa wakihangaika pasipo mafanikio kupata tiba na kinga ili kudhibiti ukimwi.Inakadiriwa kuwa kufikia mwaka juzi kulikuwa na watu milioni 33 walioambukizwa virusi hivyo hatari.

Wakati dunia kwa ujumla ingetamani tiba ya ugonjwa huo hatari ipatikane hata leo,ni muhimu kwa wenye dhamana ya kuuhabarisha umma kuwa makini wanapotoa taarifa za kitaalamu zinazohitaji ufafanuzi makini ili kuepuka kutoa matumaini yasiyoendana na ukweli.Kwa kifupi,hadi sasa hakuna dawa ya ukimwi.Kilichogundulika ni hizo antobodies,na bado kuna hatua mbalimbali za kitabibu na kitaratibu kabla haijathibitishwa rasmi kuwa tiba au dawa ya ugonjwa huo imepatikana.

Lengo la makala hii sio kuvunja matumaini ya walioanza kuamini kuwa 'dawa ya ukimwi imepatikana' bali ni kutoa ufafanuzi ambao naamini utawasaidia walioathirika kuzingatia ushauri wa kitaalam na kwa sote kwa ujumla kujichunga kwa kuepukana na ngono zembe.

Friday, 16 July 2010


Urban Pulse Production inawaletea burudani na matukio yaliojiri ndani ya Michuano ya kumtafuta Miss & MR East Africa UK 2010 yaliyofanyika  3rd July 2010 Mjini London.

Katika kinyang'anyiro hicho binti Randa Shelbly kutoka Eritrea alinyakua kombe la miss east Africa UK wakati mchizani Degnite Abdeta Dauggie ndio alichukua Mr East Africa UK.

Wadau karibuni kushuhudia tukio hili la kipekee kwa kubofya hapo chini.

Libeneke Oye

asanteni na Wote Mbarikiwe

Frank Eyembe
Urban Pulse Creative



Wednesday, 14 July 2010

Nimekumbana na swali hili tangu udogoni:Alianza kuku,au lilianza yai?Kama alianza kuku,alitoka wapi ilhali sote twajua kuku anatoka kwenye yai?Na kama lilianza yai,lilitoka wapi wakati tunafahamu kuwa yai hutagwa na kuku?Baada ya kukosa jibu lenye mantiki niliamua kuachana na swali hali maana kujihangaisha kutafuta jibu ilikuwa kazi bure.Nahisi hata nawe msomaji umeshakumbana na swali hilo mara kadha wa kadha.

Lakini hatimaye kitendawili hicho kimepata ufumbuzi.Kwa mujibu wa gazeti la bure la Metro,watafiti wa Kiingereza wanasema kuwa kuku ndiye aliyeanza kabla ya yai kwa vile yai linaweza kupatikana tu kwa chembechembe za protini zinazopatikana katika mifuko ya uzazi ya kuku.

"Imekuwa ikidhaniwa kwa muda mrefu kuwa yai ndilo lililoanza kabla ya kuku lakini sasa tuna ushahidi wa kisayansi kuwa kwa hakika alianza kuku kabla ya yai",alisema Dakta Colin Freeman kutoka Chuo Kikuu cha Sheffield,aliyeshirikiana na watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Warwick.

"Protini hiyo ilitambuliwa kabla na ilihusishwa na uzalishaji wa yai lakini kwa kuchunguza kwa undani tumegundua namna gani protini hiyo inavyowezesha hatua hiyo (ya kutengeneza yai).

Protini hiyo-inayofahamika kitaalam kama ovocledidin-17 (OC-17) inafanya kazi kama kichocheo (catalyst) kuharakisha maendeleo ya yai.

Wanasayansi hao walitumia kompyuta yenye uwezo wa hali ya juu (supercomputer) ifahamikayo kama HECToR,ambayo ipo jijini Edinburgh,Scotland, kukuza (zoom) hatua zinazoonyesha jinsi yai linavyozalioshwa.

Ilibainika kuwa OC-17 ni muhimu katika kuanzisha kukomaa (crystallization)-hatua ya awali katika uundwaji wa gamba la yai.Protini hiyo hugeuza calcium carbonate kuwa chembechembe za calcium (calcite crystals) ambazo ndizo zinazounda gamba la yai,huku zikitengeneza gramu 6 za gamba katika kila masaa 24.

Profesa John Harding,pia kutoka Chuo Kikuu cha Sheffield,alisema kuwa ugunduzi huo unaweza kuwa na matumizi mengine pia."Kufahamu namna gani kuku wanatengeneza mayai ni jambo la kupendeza lakini pia linaweza pia kutupatia vidokezo katika namna ya kutengeneza vitu vipya".

Imetafsiriwa kutoka gazeti la Metro toleo la leo.

Tuesday, 13 July 2010


A politician had an accident and dies.

His soul reaches the Paradise and found St. Peter at the entrance.

-- "Welcome to Paradise! Before you could get in, there is a little problem... We rarely seen politicians here, you know… So we do not know what to do with you..."

-- "I see, no problem just let me enter." says the politician.

-- "I though I would like to let you in but I have higher orders as it´s known… We will do the following: You pass one day in Hell and one day in Heaven. You can then choose where to spend eternity."

-- "It is not necessary, I have already decided. I want to stay in Heaven." says the politician.

-- "Sorry, but we have our rules."

So, St. Peter takes him to the elevator and he comes down, down to Hell. The door opens up and he sees himself in the middle of a beautiful golf course.

In essence, the club where were all his friends and other politicians with whom he had worked. All very happy.

He was greeted, embraced and then they started to talk about the good times when they got rich at the expense of the people.

They played golf, relaxed and then ate lobster and caviar.

Who was also present was the devil, a very friendly guy who spent all the time dancing and telling jokes. They enjoyed themselves so much that before they realize it was time to go.

After a lot of redundant hugs and words of farewell he enter into the elevator.

He rises, rises and the door opens up again. St. Peter was expecting him.

-- Now it´s the time to visit the Paradise.

He spends 24 hours in paradise among a group of happy souls who go from cloud to cloud playing harps and singing. All went very well and before he noticed the day comes to an end and St. Peter returns.

-- "Now what? You spent one day in Hell and one day in Heaven. Now choose your eternal home."

He thought for a minute and answered:

-- "Look, I never thought to make this decision… The Paradise is very good but I think I'll be much better in Hell."

Then St. Peter takes him back to the elevator and he comes down, down to hell.

The door opens up and he saw himself in the midst of a massive ground full of garbage and a horrible smell. He saw all his friends with the clothes torn and very dirty searching the rubble and putting it in black bags. He also saw some of his friends in dispute to take pieces of rotten food.

The devil put the arm by the politician´s shoulder.

-- "I do not understand?" Mumble the politician. -- "Yesterday I was here and it even had a beautiful golf course, a club, lobster, caviar and we danced and had fun all the time. Now I see that it´s only full of very smelly garbage and my friends are totally tear down!"

The devil looks at him… Ironically smiles and says:

-- "Yesterday we were in campaign season before election. Now we have your vote... I´m sorry, this is the reality!"

SOURCE Hubpages

Kuna tofauti moja ya msingi katika Twitter na Facebook (social media nazizipendelea zaidi),nayo ni namna watu wawili wanavyounganishwa na huduma hizo.Wakati nikiomba kuunganishwa na mtumiaji wa Facebook,na kukubaliwa inamaanisha nitaweza kuona profile yake na updates mbalimbali,kwenye Twitter habari ni tofauti.Nikiamua "kumfuata" (following) mtu,haimaanishi kuwa mtu huyo automatically naye "atanifuata".

Lakini katika mazingira ya kawaida,na pengine kistaarabu,kama mtu ameamua "kukufuata" huko Twitter,unapungukiwa nini ukirejesha "fadhila" kwa kumfuata mtu huyo?Au ndio usupastaa kwamba wanaokufuata ni wengi kuliko unaowafuata?Ofkoz,inaweza kuwa vigumu "kumfuata" kila "anayekufuata" ukiwa na "wafuasi" maelfu kadhaa lakini si vigumu kama wafuasi wako ni mia na kitu tu.

Naandika haya nikitambua kuwa uamuzi wa mtu kukufuata ni suala la mtu binafsi.Na kwa vile mtu ahajalazimishwa kumfuata mtu mwingine inaweza kupelekea hoja yangu kuonekana haina umuhimu.Nachojaribu kupigia mstari hapa ni ustaarab wetu wa Kiafrika.Katika mazingira ya kawaida,kama jana nilikutana nawe nikakusalimu,leo pia tumekutana nikakusalimu na kesho inakuwa hivyohivyo,basi kistaarabu inatarajiwa kuwa kesho kutwa nawe utaanzisha salamu.Kinyume cha hivyo,tafsiri itakuwa aidha unaringa au huhitaji salamu yangu.Ni katika mantiki hiyohiyo,kama mtu ameamua kukufuata (hata kama wewe ni maarufu mara elfu kuliko huyo mfuasi) basi ni tarajio la mfuasi huyo kuwa nawe utamfuata.Si lazima lakini ni katika masuala ya ustaarab tu.

Kama unaafikiana nami,basi pengine fanya jambo la kupendezesha roho za wale wanaokufuata lakini wewe hujaamua kuwafuata:WAFUATE PIA.Haigharimu chochote,haikupunguzii umaarufu ulionao,na zaidi,itakufanya uonekane huna dharau.

Ni ushauri wa bure tu.

Saturday, 10 July 2010

Kwa mara ya tatu ndani ya wiki moja askari wa jeshi la polisi amejiua kwa kujipiga risasi.Haya si matukio ya kuyachukulia kimzaha kwani licha ya ukweli kuwa vifo vya askari hao ni pigo na doa kwa jeshi hilo lakini pia inawezekana kesho na keshokutwa,Mungu aepushie mbali,tunaweza kusikia askari amemwagia risasi raia kadhaa wasio na hatia kabla ya kutoa uhai wake mwenyewe.Kuna tatizo ndani ya jeshi hilo lakini kama ilivyo ada kwenye maeneo mengine wahusika wanaendelea kujifanya mbuni kwa kuficha vichwa kwenye shimo huku mwili ukibaki nje.

Nilibahatika kufanya kazi na polisi kwa muda mrefu tu na kwa hakika utawahurumia ukisikia na kuona matatizo wanayokabiliana nayo kimaisha na kiutendaji kazi.Kubwa zaidi ni hali ya maisha yao hususan kwenye suala la makazi.Nenda Kilwa Road,Oysterbay au Temeke na shuhudia mazingira wanayoishi wanadola hao,na utakubaliana nami kuwa si vigumu kwao kukumbwa na shinikizo la kisaikolojia.Hebu tafakari kuhusu askari anayekesha lindoni Masaki,Mikocheni,Upanga,Oysterbay,nk kwa vigogo na kushuhudia watu wanavyokula keki ya taifa wakati mwanadola huyo anaishi maisha ya chini kabisa licha ya mchango wake mkubwa katika usalama wa nchi.Ni dhahiri anaweza kupatwa na mawazo kuwa maisha na kazi aliyonayo havina thamani.

Lakini pia kuna unyanyasaji unaotawala kwenye vyombo vyetu vya dola ambapo viongozi ni miungu watu huku wakipata maslahi manono kupindukia ukilinganisha na wale wanaowaongoza.Na hiyo sio huko polisi tu bali hata katika ofisi nyinginezo-za dola na zisizo za dola-ambapo viongozi hujijengea ukuta mrefu wa kuwatenganisha na wanaowaongoza.Vikao kati ya viongozi na watumishi wa ngazi za chini hutawaliwa na vitisho vinavyokwaza kero na malalamiko ya askari wa ngazi za chini kusikika.

Pasipo kutafuta ufumbuzi wa haraka katika wimbi hili la polisi kujiua kwa risasi basi tuwe tayari kushuhudia balaa.Silaha haziui watu,bali watu hutumia silaha kujiua au kuua wengine.Sasa kama askari wetu tunaowakabidhi silaha wanaweza kujiua kama njia ya ufumbuzi wa matatizo yao binafsi,yayumkinika kubashiri kuwa siku moja wanaweza kabisa kuua watu wengine kabla ya kujiua wao wenyewe.

Tusipoziba ufa tutajenga ukuta.Hebu soma habari kamili katika kiungo kifuatacho

Hebu soma habari kamili kwa kubonyeza KIUNGO HIKI.

Friday, 9 July 2010

UJUMBE KUTOKA URBAN PULSE: Karibuni tena wadau wote wa kuangalia sehemu ya pili ya mada ya Uraia Pacha kutoka kwa Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa Bernard Membe wakati akitoa hotuba kwenye Diaspora hapa Mjini Ukerewe tarehe 26.3.2010

Pia Mh Membe alisoma ujumbe kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh Jakaya Kikwete akiwasifu na Kuwapongeza Watanzania katika Diaspora. Tafadhali Bonyeza chini kuangalia Video

Thursday, 8 July 2010


Imetumwa na mdau FRANK EYEMBE wa Urban Pulse

Wednesday, 7 July 2010


Demokrasia katika jamii isiyojali utawala bora ni sawa na kufukia makaratasi ardhini kwa matarajio ya kuota mmea wenye matunda ya noti.Ni mithili ya kualika timu ya Taifa ya Brazil kwa mabilioni ya shilingi kisha mechi husika ituache na bili kubwa pasipo manufaa yoyote.Hebu tafakari.Mwezi Oktoba Watanzania kwa mamilioni yao watapiga kura kumchagua Rais na Wabunge.Japo shughuli hiyo ni ya siku moja tu,maandalizi yake yanagharimu mabilioni ya shilingi.Wenyewe wanasema ndio gharama ya demokrasia.Lakini baada ya uchaguzi,wengi-kama sio wote-wa tutakaowachagua watasahau kabisa kwanini tumewachagua,huku wakiwa bize kutafuta namna ya kufidia gharama walizotumia kuingia madarakani.

Zamani hizo tuliambiwa kuwa demokrasia ni pamoja na uwepo wa vyama vingi vya siasa.Takriban miongo miwili baadaye Watanzania wameshuhudia namna uwepo wa vyamahivyo vingi vya siasa ulivyoshindwa kulikwamua taifa letu kutoka kwenye lindi la umasikini.Sanasana umasikini umekuwa ukizidi kuongezeka huku wanasiasa wetu wakibadili kauli mbiu kila baada ya muhula (kwa mfano kutoka Ari Mpya,Kasi Mpya na Nguvu Mpya kuwa Ari Zaidi,Kasi Zaidi na Nguvu Zaidi).Tumeshuhudia pia mlolongo wa sera,mikakati,mpingo na vitu kama hivyo,from MKUKUTA to MKURABITA to KILIMO KWANZA.Na kwa mawazo mapya hatujambo,shughuli ipo kwenye utekelezaji.

Siku chache zilizopita nilitundika makala kuhusu utata wa kauli za Waziri wa Sheria na Katiba Mathias Chikawe na zile za Makamu Mwenyekiti wa CCM Pius Msekwa kuhusu suala la uanzishwaji Mahakama ya Kadhi.Wakati Waziri Chikawe aliahidi kuwa mahakama hizo zingeanza kazi mwakani,Msekwa alitamka bayana kuwa suala hilo haliwezekani.Hadi leo hakuna ufafanuzi uliotolewa kuhusu suala hilo ila kilicho bayana ni kuwa CCM imeamua kuachana nalo baada ya kuliingiza kwenye manifesto yake ya Uchaguzi mwaka 2005.Kwa vile sie ni mahiri zaidi wa kuhangaika na mambo kwa mtindo wa zimamoto tunasubiri liwake la kuwaka ndipo tuanze kuhangaika namna ya kudhibiti.Taasisi zenye majukumu ya kuwa proactive (yaani kuazuia majanga kabla hayajatokea) ziko busy zaidi na kuhakikisha CCM inarejea madarakani kwa ushindi wa kishindo badala ya kujishughulisha na jukumu lao la msingi la kulinda na kutetea ustawi wa taifa letu.Kwao,siasa (yaani CCM) ndio nchi na ndio kila kitu.

Majuzi umejitokeza utata mwingine wa kauli kati ya mawaziri wawili waandamizi kuhusu suala la uraia wa nchi mbili (dual citizenship).Na kichekesho ni kwamba tofauti na ule mgongano wa kauli kati ya Chikawe na Msekwa,safari hii mgongano wa kauli za mawaziri hao umejiri ndani ya jengo la Bunge katika kikao kinachoendela cha bajeti ya mwaka 2010/11.Awali,Waziri wa Mambo ya Ndani Lawrence Masha alilieleza Bunge Tukufu kuwa serikali imeamua kuwa huu sio wakati mwafaka kwa suala la uraia wa nchi mbili,na kwamba serikali anaangalia uwezekano wa kuanzisha ukaazi wa kudumu (permanent residency).Waziri Masha alieleza kuwa serikali inaandaa hoja kuhusu suala hilo la permanent recidency kwa minajili ya kuileta bungeni ijadiliwe. "Huu sio wakati mwafaka kuruhusu uraia wa nchi mbili,serikali inaangalia uwezekano wa kuanzisha ukaazi wa kudumu badala ya uraia wa nchi mbili", alisema Masha.

Wakati Masha akisema hivyo,Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Bernard Membe alilieleza Bunge hilohilo kuwa serikali imeridhia suala la uraia wa nchi mbili na kwamba Wizara yake iko kwenye mchakato wa kuwasilisha suala hilo kwenye kikao cha Barza la Mawaziri.Pia Membe alieleza kuwa anafanya mawasiliano na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) ili kupata baraka zao kutokana na suala hilo kuwa la Muungano.Akihitimisha hoja ya bajeti ya wizara hiyo, kwa mwaka wa fedha 2010/2011, Waziri Membe alisema siyo dhambi, Watanzania kutafuta riziki nje ya nchi na ni haki yao kubaki na uraia wa Tanzania.Alisema wakati umefika kwa Watanzania, kupatiwa haki yao ya msingi kwani licha ya kuwa ni manufaa kwao pia ni manufaa kwa nchi kutokana na fursa ya kuongeza pato la taifa.

Kadhalika,inadaiwa kuwa Waziri Membe aliwaeleza Watanzania waliohudhuria mkutano wa Diaspora jijini London hivi karibuni kwamba suala hilo limeshajadiliwa na baraza la mawaziri na linasubiri kuwasilishwa bungeni ili upitishwe au kupingwa na wabunge.Mimi sikuhudhuria Mkutano huo wa Diaspora kwa vile niliamini ungenipotezea muda wangu tu kwa sababu viongozi wetu ni mahiri sana katika kuahidi mambo mazuri kwenye hadhara,na hujifanya wasikivu sana lakini utekelezaji ni zero,sifuri,zilch!

Ni dhahiri kwamba mmoja kati ya mawaziri hawa anadanganya.Wakati sina la kusema kuhusu kauli ya Waziri Masha,kauli za Waziri Membe huko Bungeni na London zinaleta utata unaoweza kuyumkinisha kuwa kuna urongo wa namna flani.Je kauli ipi ni sahihi kati ya hiyo alotoa London kuwa suala hilo limeshajadiliwa na Baraza la Mawaziri na hiyo ya bungeni kuwa suala hilo bado liko wizarani huku likifanyiwa mchakato wa kulipeleka kwenye Baraza la Mawaziri?

Unajua kwanini mmoja wao anadanganya?Sababu ni kadhaa,lakini kwa ufupi,moja,ni kwa vile mdanganyifu huyo anafahamu bayana kuwa wabunge wanaoelezwa suala hilo wapo bize zaidi kufikiri namna watakavyorudi bungeni baada ya uchaguzi (sambamba na kuwazia posho zao nono za vikao vya bunge) kuliko kumkalia kooni waziri aeleze kinagaubaga.Ndio maana mwanzoni mwa makala hii nilibainisha uselessness ya demokrasia yetu.Tunapoteza mabilioni ya shilingi (sambamba na muda wetu kusikiliza porojo za "mkituchagua tufafanya hiki na kile") kuwachagua watu wa kutuwakilisha bungeni lakini wakishafika huko wanakuwa bize zaidi na maslahi yao binafsi.

Pili,anayedanganya kati ya mawaziri hao anafahamu kuwa aliyemteua hatamwajibisha.Kama kuna mtu alimudu kumzuga Rais kwa kuchomekea ishu kadhaa kwenye muswada wa sheria za gharama za uchaguzi na kisha akasalimika,kwanini basi mdanganyifu huyo katika suala hili la uraia mbili awe na hofu?

Tatu,waziri anayedanganya kati ya hao wawili anafahamu udhaifu wa Watanzania katika kudai haki zao za msingi.Kiongozi anaweza kudanganya waziwazi kwenye umati wa watu lakini bado akaishia kupigiwa makofi na vigeregere.Ule wimbo wa "Ndio Mzee" wa Profesa Jay unawakilisha hali halisi ya namna Watanzania wengi wanavyoridhia kuzugwa na wanasiasa wababaishaji.Hebu angalia namna harakati za kuirejesha tena madarakani CCM zinavyopamba moto huko nyumbani.Kwa mgeni,anaweza kudhani labda chama hicho ni kipya na hakihusiki kabisa na kashfa za ufisadi,kubebana,kubomoa uchumi wetu na madudu mengine chungu mbovu yanayoifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi masikini kabisa duniani licha ya raslimali lukuki iliyojaaliwa kuwa nazo.Binafsi naamini kuwa unyonge huo wa Watanzania umechangiwa sana na siasa za chama kimoja ambapo kiongozi alikuwa mithili ya Mungu-mtu,hakosei,lazima ashangiliwe hata akiongea utumbo,sambamba na suala la kujikomba kwa viongozi kwa matarajio ya kujikwamua kwa namna moja au nyingine.

Na kwa vile vyama vya upinzani vimetuthibitishia kuwa uwezo wao katika kuing'oa CCM madrakani ni kama haupo,basi mazingaombwe kama hayo ya Chikawe na Msekwa,na haya ya sasa kati ya Masha na Membe yataendelea kuwepo kwa muda mrefu sana.Unaweza kuhisi kama nimekata tamaa vile kwa namna ninavyoandika.Hapana,ila safari yetu ni ndefu sana,na tatizo sio urefu tu bali ni kiza kilichotanda kwenye njia yetu ambayo imejaa mashimo kadhaa.Ni sawa na kipofu kumsaka paka mweusi kwenye chumba chenye giza ilhali paka huyo hayumo chumbani humo.

Tuesday, 6 July 2010

Kushoto ni Urban Pulse Director Baraka Baraka,TV Personality Sporah Njau,Landlady Lucy na Young Moogs
Urban Pulse CEO Frank Eyembe na Jackson Mugisha,Mtanzania Pekee Aliyeshiriki Kwenye Mr & Miss East Africa
Wageni na Washindani
Producer wa Muziki Josh Mbajo na Producer wa Filamu Frank Eyembe
Mc Moseh na Urban Pulse
Fyah Sister First Lady wa Urban Pulse
Kundi la Utamaduni Kutoka Zimbabwe
Washindani Wakiwa Katika Mavazi ya Kitamaduni
Urban Pulse Princes Ordain na Young Jos Wakifunika
Baadhi ya Warembo
Mshindi Randa Shelby Kutoka Eritrea
Mshindi Dawggie kutoka Ethiopia
Washindi
Warembo

Sunday, 4 July 2010

Kwanza naomba samahani kwa kupotea kwa zaidi ya wiki sasa.Afya iliyumba kidogo.Napenda kutumia fursa hii kuwashukuru wote walionitumia meseji za kunitakia afya njema.Bwana Amesikiliza sala na dua zenu.

Jana,katika pitapita zangu mtandaoni nilikutana na habari kwamba Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki,Juma Mwapachu,amewashukia wasomi wa vyuo vikuu kwa kuwapotosha wananchi kuhusiana na serikali kujiunga na soko la pamoja la Jumuiya ya Afrika Mashariki lililofunguliwa majuzi.

Kwa mujibu wa habari hiyo,Balozi Mwapachu alitoa kauli hiyo kufuatia ya baadhi ya wasomi kudai kuwa soko hilo linaweza kuwaathiri watanzania katika ushindani wa ajira.Akizungumza jana kwenye ufunguzi wa maonyesho ya 34 ya biashara ya kimataifa yanayoendelea jijini Dar es Salaam, Balozi Mwapachu alisema wasomi hao ambao wamesomea uchumi, wameshindwa kusema ukweli kuhusiana na kujiunga na soko hilo, na kusababisha wananchi kuingia uoga.

Alisema wasomi walipaswa kuwa mstari wa mbele kuwaelimisha wananchi kuhusu jumuiya hiyo na faida zake badala ya kuwapotosha wananchi kuhusu suala hilo na kusababisha baadhi ya nchi wanachama wa jumuiya hiyo kuhofia.

Alisema kabla ya kufungua milango hiyo aliweza kuzunguka katika kila nchi kwa ajili ya kuzungumza na wadau mbalimbali kuhusu suala hilo, lakini wananchi wamekuwa waoga na kusababisha kutoa maoni mbalimbali ya kupotosha.

"Niwashaangaa sana wasomi tena wamesomea uchumi, lakini wamekuwa wa mbele kuwapotosha wananchi kuhusu soko la pamoja la jumuiya ya Afrika Mashariki, hii imesababisha wanachi washindwe kujiamini na kufikiri kuwa wanaweza kukosa ajira,"alisema Mwapachu.

Alisema watanzania wengi wanawaogopa wakenya kwa madai kuwa wanaweza kushindwa kuingia kwenye ushindani wa soko la ajira.

Nadhani kwa mtu mwenye uelewa mkubwa kama Balozi Mwapachu kutoa kauli hizo ni jambo la kusikitisha sana na ni uthibitisho mwingine wa namna maslahi binafsi na ya kisiasa yanavyowekwa mbele ya maslahi ya taifa,sambamba na kupuuza ushauri wa kitaalam.

Yayumkinika kuamini kuwa kwa wadhifa wake kama Katibu Mkuu wa Jumuiya hiyo,ni lazima Mwapachu aipigie debe ili iendelee kuwepo kwani kinyume chake ni kuwa hatakuwa na ajira.Hata hivyo,laiti Mwapachu angeangalia mantiki ya hoja za wasomi (ambazo kwa hakika ziko shared na hata "wasio wasomi") badala ya kuwashambulia kama kundi la kijamii (yaani kujadili hoja badala ya kumjadili mtoa hoja)angeweza kabisa kufahamu kwanini wanaonyesha wasiwasi wao.

Hivi kama kabla ya ujio wa soko la pamoja la Jumuiya hiyo tayari wageni (licha ya hao wanaotoka Kenya na nchi nyingine za Jumuiya) tayari soko la ajira na bidhaa limetawaliwa kwa kiasi kikubwa na wageni,kwanini basi tusihofu kuwa "kuhalalisha" huko kutapelekea hali kuwa mbaya zaidi kwa Watanzania?

Na wakati Mwapachu anatoa porojo zake kuhusu mafanikio ya soko la pamoja,mbona hatuambii yeye na viongozi wenzie wa Kitanzania wameshafanya jitihada zipi kuhamasisha Watanzania kumudu ushindani uliopo na ujao?Siafikiani na mawazo potofu ya Mwapachu kuwa tatizo la Watanzania ni uoga.Na hata kama tatizo lingekuwa ni uoga basi bado hoja ingekuwa iwapo uoga huo ni halali au potofu kwani uoga kama uoga sio dhambi au kosa kama unajengwa kutokana na mantiki.Tatizo la msingi linalowakabili Watanzania kukabiliana na changamoto za mfumuko wa nguvu za nje katika soko la ndani la ajira na bidhaa ni complex sana,na makala hii fupi haiwezi kujadili yote bali itaangalia kwa ufupi.

Kwa upande wa biashara,kuna tatizo sugu la urasimu ambalo kwa kiasi kikubwa linachangiwa na ufisadi.Urasimu kuanzia kwenye utaratibu wa kuandikisha biashara hadi kwenye masuala ya kodi.Sijawahi kufanya biashara lakini nina marafiki kadhaa wanaojaribu kumudu maisha yao kwa kujihusisha na biashara.Kwa kifupi,ajira ya Mtanzania kwa kutegemea biashara ni suala gumu sana.Katika mazingira ya kawaida sio rahisi kwa biashara kudumu kwa angalau miezi kadhaa kama mhusika hatokuwa tayari kutoa chochote kitu kwa wahusika.Yayumkinika kusema kuwa ili biashara halali ishamiri vema ni lazima ikaribishe illegality ya namna flani,yaani uharamu wa biashara ili kuwa halali.

Na wakati Watanzania wengi tu wangependa kujishughulisha na biashara zao kihalali ili wamudu maisha yao,wanakumbana na ushindani kutoka kwa wenzao "wanaobebwa" na vigogo.Hivi mfanyabiashara anayelipa mlolongo wa kodi huku anauza bidhaa za ndani atamudu vipi kupambana na mfanyabiashara anayeagiza vitu kutoka nje (huku vingine vikiwa feki) lakini anavilipia kodi pungufu au halipi kodi kabisa?Ni dhahiri biashara ya huyo "anayebebwa" itashamiri zaidi kuliko ya huyo mnyonge anayejikongoja peke yake.

Lakini pia kuna suala la utamaduni wa kuthamini baidhaa za nje kuliko za ndani.Baadhi ya wachambuzi wanaeleza kuwa miongoni mwa madhara ya utandawazi ni kuibuka kwa mapambano kati ya vitu vya nje dhidi ya vya ndani au vya asili.Hapa simaanishi kuwa kila element ya utandawazi ni mbaya.Sasa kama serikali yetu inaagiza kila kitu kutoka nje kwa ajili ya matumizi yake huku ikiwaacha mafundi seremala wetu "wakidodewa" na samani zao,na hiyo ni kabla ya ufunguzi wa soko hilo,sasa kwanini wasomi wasihofu kuwa soko hilo linaweza kuwa habari mbaya zaidi kwa Watanzania wengi?

Tukija kwenye ajira,hali ndio mbaya zaidi.Wakati Watanzania wamekuwa mahiri zaidi kupeleka watoto wao Kenya na Uganda,wenzetu hao wamekuwa wakileta nguvu kazi yao ya ziada kuchukua nafasi mbalimbali za kazi.Na kama ilivyo kwenye suala la bidhaa,waajiri wetu nao wanaelekea kuwa na ugonjwa uleule wa kuthamini zaidi wageni kuliko wazawa.Mwapachu alipaswa kutueleza ni Watanzania wangapi wana ajira nchini Kenya,Uganda au Rwanda kulinganisha na raia wa nchi hizo waliokamata ajira hapo nyumbani kabla ya ujio wa soko la pamoja.Najua hawezi kusema hilo sio kwa vile hana takwimu (na inawezekana kabisa akawa hana) bali anafahamu kuwa kwa kweka hilo bayana atalazimika kuungana na hofu walionayo wasomi na Watanzania wengine.

Kilichoua Jumuiya ya awali ya Afrika Mashariki ni kuweka siasa mbele ya maslahi ya nchi.sambamba na kupuuza ushauri wa wataalamu.Na akina Mwapachu ambao walikuwa watu wazima muda huo wanataka kurejea makosa hayohayo.Wanajifanya vipofu wa ukweli kwamba ni vigumu kuwa na ushirikiano wa maana palipo na viwango tofauti vya maendeleo kati ya nchi husika.Tunafahamu vema uchumi wa Kenya,Uganda na Rwanda unavyofanya vema zaidi ya uchumi wetu.Sasa kama tunafahamu hilo kwanini basi tusihofu kuwa soko hili jipya linaweza kufanya hali kuwa mbaya zaidi?Au Mwapachu na wenzake wanadhani kuwa ukigusana na tajiri nawe unapata utajiri?They are completely wrong.Mahusiano ya mwenye uwezo wa kiuchumi na mwenye uwezo duni mara nyingi huishia kumnufaisha zaidi mwenye uwezo kwani nguvu ya uchumi inapelekea kuwa na nguvu kwenye maeneo mengine pia.

Akina Mwapachu wanapaswa kufuatilia kwa karibu mambo yanayoyumbisha jumuiya ya Ulaya ambapo nchi kama Uingereza zimeendelea kuwa na msimamo wa kujihusisha kwa kiasi flani tu na sio kwa asilimia 100 kwa vile wanatambua kuwa kuna nchi zenye uchumi duni zinazotarajia ushirikiano huo uwanufaishe wao zaidi at the expense of wale wanaojimudu.

Mwisho,ili Tanzania ijikomboe kutoka uchumi unaomilikiwa kwa zaidi ya asilimia 90 na wageni ni lazima siasa iwekwe kando,ushauri wa kitaalamu uzingatiwe,na kubwa zaidi,maslahi ya taifa yawekwe mbele ya maslahi binafsi.Vinginevyo,soko la pamoja la Afrika Mashariki litaishia kuwa soko la bidhaa na ajira kwa Wakenya,Waganda,Wanyarwanda na Warundi na sie "tukiishia kunufaika" kwa uwepo wa akina Mwapachu kama viongozi wa jumuiya ilhali uchumi wetu ukizidi kuelekea shimoni.

Categories

Unordered List

Sample Text

Blog Archive

Labels

Follow Us on FaceBook

Popular Posts

Recent Posts

Recent Comments

Recent Premium Themes

Your Links

Flickr

Powered by Blogger.

Blog Archive

Followers

Download

Your Links

Blogger Tricks

Popular Posts

Recent Posts

Text Widget